Category: STORY

MPANZU KINARA WA KUPIKA MABAO YA LIGI KUU YA NBC.

 

Kiungo mshambuliaji wa Simba, Elie Mpanzu, ameendelea kuthibitisha ubora wake katika Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2025/26 baada ya kuongoza orodha ya wachezaji wenye pasi nyingi za mabao kufikia sasa akiwa ametoa tisa (9).

Mpanzu amekuwa mhimili muhimu katika safu ya ushambuliaji ya Simba , akichangia si tu kwa ubunifu wa kutengeneza nafasi za mabao bali pia kwa ushirikiano mzuri na washambuliaji wa timu hiyo, jambo lililoifanya Simba kuendelea kuwa na ushindani mkubwa katika mbio za ubingwa.

Anayemfuatia kwa karibu ni kiungo wa Azam, Feisal Salum mwenye pasi nane (8).

Feisal ameendelea kuonyesha kiwango cha juu msimu huu kwa kuwa miongoni mwa wachezaji wanaotengeneza nafasi nyingi za kufunga kwa wenzake.

Katika nafasi ya tatu kuna kundi la wachezaji wanne wenye saba (7) kila mmoja, hawa ni Allan Okello wa Young Africans, Iddi Selemani wa Azam , Clatous Chama wa Simba na Zabona Mayombya wa Pamba Jiji.

Orodha hiyo inakamilishwa na wachezaji wawili wa Young Africans ambao ni Duke Abuya na Maxi Nzengeli wenye sita kila mmoja.

MOSSI, FEISAL HAPATOSHI VITA YA UFUNGAJI BORA

VITA ya ufungaji bora wa Ligi Kuu ya NBC imeanza upya baada ya mshambuliaji wa Singida Black Stars Mossi Ndumumwe kufikia idadi ya mabao aliyokuwa nayo kiungo wa Azam,Feisal Salum.

Mossi Ndumumwe anaekipiga kunako Singida Black Stars amecheza michezo 20 sawa na dakika 1622 huku akifanikiwa kuingia nyavuni mara 14 pasipo kuwa na bao lolote la mkwaju wa penati.

Feisal Salum wa Azam amefanikiwa kucheza michezo 26 ya Ligi Kuu ya NBC sawa na dakika 2095 huku akiingia nyavuni mwa wapinzani wake mara 14.

Methew Tegisi wa Pamba Jiji ameshacheza michezo 22 sawa na dakika 1567 amefanikiwa kutikisa nyavu mara 11.

Allan Okello wa Young Africans amecheza michezo 22 ya Ligi Kuu ya NBC mpaka sasa sawa na dakika 1567 huku akitikisa nyavu za wapinzani mara 11.

Fabrice Ngoy wa Namungo amecheza michezo 27 sawa na dakika 1720 ambapo amefanikiwa kufunga mabao 11.

Mudathir Yahya wa Young Africans nae hayuko mbali amecheza michezo 20 sawa na dakika 1253 na kufanikiwa kufunga mabao tisa.

Pacome Zouzoua wa Young Africans ameshacheza michezo 20 ya Ligi Kuu ya NBC sawa na dakika 1422 amefanikiwa kufunga mabao tisa.

Selemani Mwalimu wa Simba amecheza michezo 23 sawa na dakika 1102 amefanikiwa kuingia golini mara tisa huku.

Prince Dube wa Young Africans amefanikiwa kucheza michezo 24 ya Ligi Kuu ya NBC sawa na dakika 1742 na kufunga mabao tisa.

YOUNG AFRICANS,SIMBA ZATAMBA MZUNGUKO 28 LIGI KUU YA NBC.

MZUNGUKO wa 28 wa Ligi Kuu ya NBC umetamatika ambapo mechi zote nane zimechezwa majira ya saa kumi jioni huku ikisalia mizunguko miwili Ligi hiyo kutamatika.

Young Africans ilikuwa mwenyeji wa timu ya Azam katika uwanja wa Amaan Zanzibar ambapo iliishushia kipigo cha mabao 3-0 yalifungwa na Ibrahim Hamad, Laurindo Dilson na Pacome Zouzoua hivyo timu hiyo kujikita kileleni.

Mtibwa Sugar ilikuwa mwenyeji wa timu ya Simba katika uwanja wa Jamhuri Morogoro ambapo timu hiyo ilipoteza mchezo huo kwa 0-3 mabao ya Simba yakifungwa na Rushine De Reuck, Seleman Mwalimu na Anicet Aura.

Pamba Jiji iliialika timu ya Mbeya City katika uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza ambapo timu hiyo ilijikuta ikipokea kichapo cha 0-2 kwa mabao yaliyofungwa na nahodha wa Mbeya City Eliud Ambokile.

KMC ilicheza na Namungo ambapo ilikubali kichapo cha 2-3 huku mabao ya KMC yakifungwa na Erick Mwijage pamoja na Mohamed Abdallah huku mchezaji wa Namungo, Fabrice Ngoy akifunga yote matatu yaani (hat-trick).

Singida Black Stars ilicheza na Tanzania Prisons katika uwanja wa Airtel Singida ambapo timu hiyo iliibuka na ushindi wa 3-1 huku mabao ya Singida yakifungwa na Mossi Nduwumwe (2) na Kennedy Juma huku Kelvin Sangati akiifungia Prisons bao moja.

Fountain Gate ilikubali kichapo cha 0-1 kutoka kwa timu ya Mashujaa katika mchezo uliochezwa kwenye uwanja wa Black Rhino, Karatu Arusha na bao la Mashujaa likifungwa na Hussein Juma.

TRA ilikuwa mwenyeji wa timu ya Coastal Union katika uwanja wa Sheikh Amri Abeid Arusha ambapo mpaka mchezo unatamatika matokeo yalikuwa sare ya 1-1, bao la TRA lilfungwa na Nasri Kombo huku Maabad Maabad akiifungia Coastal bao la kusawazisha.

Mchezo wa mwisho ulikuwa Dodoma Jiji dhidi ya JKT Tanzania katika uwanja wa Jamhuri Dodoma ambapo mchezo huo ulitamatika kwa matokeo ya 0-0.

NANE ZA MOTO LIGI KUU YA NBC.

LIGI Kuu ya NBC itaendelea leo kwa michezo yote nane kupigwa saa 10:00 alasiri ikiwa mbashara katika chaneli mbalimbali za Azam Tv.

Visiwani Zanzibar katika uwanja wa New Amaan itapigwa ‘Dabi’ ya Dar es Salaam kati ya Young Africans itakayokuwa mwenyeji wa Azam.

Mchezo huo ndio mkubwa kwa leo ambapo wababe hao wapo katika mbio za ubingwa wa Ligi Kuu ya NBC hivyo watazisaka alama tatu muhimu kuhakikisha wanajiweka kwenye nafasi nzuri.

Timu ya Mtibwa Sugar itakuwa mwenyeji wa timu ya Simba katika uwanja wa Jamhuri mkoani Morogoro ikiwa Simba ipo katika mbio za ubingwa sambamba na Young Africans na Azam hivyo alama tatu zikiwa na maana kubwa ya kuendelea kusalia kwenye kupambania ubingwa.

TRA United itaikaribisha timu ya Coastal Union katika uwanja wa Sheikh Amri Abeid Arusha huku Fountain Gate ikichuana na Mashujaa katika uwanja wa Black Rhino uliopo Karatu, Arusha.

Kwa upande wa Dodoma Jiji itakuwa mwenyeji wa timu ya JKT Tanzania katka uwanja wa Jamhuri Dodoma huku Singida Black Stars ikichuana na Tanzania Prisons kwenye uwanja wa Airtel, Singida.

Nayo timu ya Pamba Jiji itakutana na timu ya Mbeya City katika uwanja wa CCM Kirumba huku KMC ikichuana na timu ya Namungo katika uwanja wa KMC Complex ambapo KMC tayari imeshuka daraja na hivyo haitakuwa sehemu ya Ligi akuu ya NBC msimu wa 2026/27.

NBC CHAMPIONSHIP 2025/26 YAFIKA TAMATI.

 

TAMATI ya msimu wa NBC Championship 2025/26 imefika jana huku Geita Gold wakitangazwa mabingwa wa ligi hiyo baada ya kumaliza msimu wakiwa na alama 77 yakiwa mafanikio yaliyowawezesha pia kupanda kushiriki Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2026/27.

Sambamba na Geita Gold, Kagera Sugar pia wamefanikiwa kurejea Ligi Kuu ya NBC baada ya kumaliza msimu wakiwa na alama 72 na kupata tiketi ya kupanda daraja.

Kwa upande mwingine, Transit Camp, Mbuni, KenGold, Gunners , B19 na TMA wataendelea kushiriki NBC Championship katika msimu wa 2026/27 baada ya kushindwa kufuzu kupanda daraja lakini pia wakifanikiwa kuepuka kushuka daraja.

Hata hivyo, Barberian na Hausung wameshuka rasmi daraja na msimu ujao watashiriki First League.

Katika hatua nyingine, nafasi ya mwisho ya kupanda Ligi Kuu itaamuliwa kupitia michezo ya mchujo kati ya Mbeya Kwanza na Polisi Tanzania.

Mchezo wa kwanza utazikutanisha Mbeya Kwanza nyumbani dhidi ya Polisi Tanzania kabla ya marudiano kuchezwa nyumbani kwa Polisi Tanzania.

Vilevile, kutakuwa na michezo ya mchujo ya kuwania kusalia NBC Championship kwa msimu wa 2026/27.

Ratiba hiyo itaanza kwa michezo ya kwanza ambapo African Sports watawakaribisha BigMan, huku Stand United wakicheza dhidi ya Songea United.

Michezo ya marudiano itawakutanisha BigMan dhidi ya African Sports, na Songea United dhidi ya Stand United.

Mashabiki sasa wanaelekeza macho yao kwenye michezo hiyo ya mchujo ambayo itaamua timu zitakazokamilisha ramani ya NBC Championship na Ligi Kuu ya NBC kwa msimu wa 2026/27.