Category: STORY

HAWA HAPA VINARA WA TAKWIMU LIGI KUU NBC.

MZUNGUKO wa 13 Ligi Kuu NBC unatarajiwa kuanza leo Novemba 19 katika uwanja wa Benjamin Mkapa mkoani Dar es Salaam kwa mchezo kati ya timu ya Ruvu Shooting na timu ya Simba majira ya saa 1:00 usiku.

Tangu kuanza kwa Ligi Kuu msimu huu wachezaji wamekua wakichuana katika takwimu ili kujiweka katika nafasi nzuri ya kushinda tuzo za mwezi na mwisho wa msimu huu kwa vinara wa takwimu hizo.

Sixtus Sabilo wa timu ya Mbeya City anashikilia usukani katika orodha ya vinara wa mabao akiwa na mabao saba akifuatiwa na Idriss Mbombo(Azam), Moses Phiri(Simba), Fiston Mayele(Yanga) na Reliants Lusajo(Namungo) wenye mabao sita kila mmoja.

Takwimu za magolikipa zinaongozwa na Aishi Manula wa timu ya Simba mwenye michezo saba bila kuruhusu bao akifuatiwa na raia wawili kutoka Kisiwa cha Comoro Ally Ahamada wa Azam FC na Mahamoud Mroivil wa Coastal Union waliocheza mechi tano bila kuruhusu bao.

Wachezaji wenye pasi nyingi zilizozaa mabao wanaongozwa na Ayoub Lyanga wa timu ya Azam mwenye pasi tano sawa na Sixstus Sabilo wa Mbeya City wakifuatiwa na Saido Ntibazonkiza wa timu ya Geita Gold mwenye pasi nne za mabao.

Baada ya mchezo wa leo Ligi Kuu itaendelea tena kesho Novemba 20 kwa michezo mitatu, Ihefu wataikaribisha timu ya Coastal Union katika uwanja wa Sokoine majira ya saa 8:00 mchana huku Mbeya City wakiwakaribisha Geita Gold kwenye uwanja wa huo saa 10:00 alasiri baada ya mechi ya kwanza na mchezo wa mwisho utakaochezwa saa 1:00 usiku Namungo watakua nyumbani uwanja wa Majaliwa kujiuliza dhidi ya Azam FC.

YANGA ‘YAIZIMA’ SINGIDA, MBEYA CITY, KAGERA HAKUNA MBABE.

IKIENDELEA kuonyesha ubabe baada ya kufuzu hatua ya makundi Kombe la Shirikisho Afrika timu ya Yanga imeiadhibu Singida Big Stars mabao 4-1 katika mchezo wa mwisho wa kumaliza mzunguko wa 12 wa Ligi Kuu NBC.

Mchezo huo umeshuhudia mchezaji Fiston Mayele wa Yanga akiwa wa kwanza kufunga mabao matatu ‘Hat-trick’ katika Ligi Kuu NBC msimu huu huku bao lingine likifungwa na Kibwana Shomari dakika ya tatu baada ya kipindi cha pili kuanza.

Ushindi huu unaifanya Yanga kufikisha pointi 26 sawa na Azam huku Yanga akiongoza msimamo kwa tofauti ya mabao saba ya kufunga na kufungwa .

Mkoani Mbeya Klabu ya Mbeya City imelazimishwa sare ya mabao mawili dhidi ya Kagera Sugar ikiwa ni sare ya pili mfululizo katika uwanja wa nyumbani.

Bao la beki Hassan Muhamud raia wa Uganda dakika ya 85 akisawazisha mabao ya Anuary Jabir aliefunga dakika ya 18 na Mbaraka Yusuph dakika ya 48 limeipa alama moja timu ya Mbeya City huku bao lingine la timu hiyo likifungwa na Tariq Seif dakika ya 61.

Huu ni mchezo wa sita kwa Mbeya City bila kupoteza tangu septemba 13 walipofungwa na timu ya Azam kwa bao la Idris Mbombo.

Uwanja wa Highland Estate timu ya Ihefu imeshindwa kutamba nyumbani baada ya kuambulia kipigo cha mabao 2-1 kutoka kwa timu ya Polisi Tanzania.

Klabu ya Ihefu iliyotangulia kupata bao la kuongoza kupitia kwa Andrew Semchimba dakika ya 19 kipindi cha kwanza ilishindwa kuhimili mashambulizi ya Polisi waliopata bao la kusawazisha kupitia kwa Vitalisy Mayanga dakika ya 51 huku bao la ushindi likipatikana kupitia kwa Samwel Onditi aliejifunga dakika ya 78.

Mchezo huo wa tano kwa kocha Juma Mwambusi unaifanya Ihefu kuendelea kubaki mkiani katika msimamo wa Ligi Kuu NBC ikiwa na pointi tano huku Polisi wakifikisha pointi tisa sawa na Dodoma Jiji huku maafande hao wakicheza mchezo mmoja zaidi ya Dodoma.

Ligi Kuu itaendelea tena Novemba 19 kwa michezo miwili Mbeya City itawakaribisha Geita Gold yenye pointi 17 sawa na Mbeya city huku Ruvu Shooting ikiikaribisha timu ya Simba katika uwanja wa Mkapa mkoani Dar es Salaam.

SIMBA YANGURUMA DAR,GEITA YATAKATA MBEYA

TIMU ya Simba imefanikiwa kupata ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Namungo FC likifungwa na Moses Phiri dakika ya 32 kipindi cha kwanza baada ya kupokea pasi safi kutoka kwa Mohammed Hussein ‘Zimbwe Junior’.

Matokeo hayo yanaifanya Simba kufikisha pointi 24 na kukalia nafasi ya pili nyuma ya vinara Azam FC wenye alama 26 huku Namungo ikisalia nafasi ya saba na pointi 15.

Bao lililofungwa na Moses Phiri Linamfanya afikishe Mabao sita akizidiwa bao moja na kinara Sixtus Sabilo anaekipiga timu ya Mbeya City mwenye mabao saba.

Mkoani Morogoro majira ya saa nane mchana timu ya Mtibwa Sugar imefanikiwa kubaki na alama zote tatu nyumbani baada ya kuifunga Coastal Union ya Tanga mabao 2-1 mchezo uliopigwa uwanja wa Manungu.

Mabao ya Mtibwa yamefungwa na Adam Adam dakika ya pili na Juma Nyangi dakika ya 32 huku bao la Coastal likifungwa na Mubarack Amza dakika ya 13.

Matokeo hayo yanaifanya timu ya Mtibwa kufikisha pointi 18 na kupanda nafasi ya tano huku Coastal wakisalia na pointi 12 na kukamata nafasi ya 11 katika msimamo wa Ligi Kuu NBC.

Nayo timu ya Geita Gold imefanikiwa kupata karamu ya mabao mkoani Mbeya baada ya kuwafunga maafande wa Prisons mabao 4-2 mchezo uliopigwa uwanja wa kumbukumbu Sokoine.

Mabao ya Geita yamefungwa na Yusuph Kagoma, Danny Lyanga, Shown Oduro na Edmund John huku mabao ya Prisons yakifungwa na Oscar Paul pamoja na bao la kujifunga kwa Shawn Oduro.

Matokeo hayo yanaifanya Geita kukusanya pointi 17 na kukamata nafasi ya sita katika msimamo wa Ligi huku Prisons ikisalia na pointi 14 na kukamata nafasi ya 10 katika msimamo wa Ligi Kuu NBC.

Ligi hiyo itaendelea Leo kwa michezo mitatu katika mikoa miwili tofauti,Mkoani Mbeya Ihefu SC itaikaribisha Polisi Tanzania uwanja wa Highland Estate majira ya saa nane mchana huku majira ya saa 10 alasiri Mbeya City itaikaribisha Kagera Sugar uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine na mchezo wa saa moja usiku utakaopigwa uwanja wa Benjamin Mkapa timu ya Yanga itaikaribisha Singida Big Stars mchezo wa mwisho kukamilisha mzunguko wa 12 .

AZAM YAKWEA KILELENI,DODOMA JIJI YAZINDUKA

TIMU ya Azam FC imefanikiwa kupanda kileleni katika msimamo wa Ligi Kuu NBC baada ya kupata ushindi dhidi ya Ruvu Shooting kwa bao 1-0.

Bao la Azam limefungwa na Idriss Mbombo dakika ya 72 kwa mkwaju wa penati baada ya Ayoub Lyanga kufanyiwa faulo ndani ya eneo la Penati.

Huu unakua ushindi wa tano mfululizo kwa Azam takribani mwezi mmoja baada ya kumtangaza Kali Ongala kama kaimu kocha mkuu.

Kwa matokeo hayo Azam inafikisha alama 26 na kushika usukani wa Ligi kwa alama tatu zaidi ya Yanga inayoshika nafasi ya pili katika msimamo.

Nayo timu ya Dodoma jiji mapema alasiri ilipata ushindi wa bao 2-1 dhidi ya KMC ya Dar es Salaam mchezo uliochezwa uwanja wa Uhuru mkoani hapa.

Dodoma ilifanikiwa kumaliza mchezo mapema ndani ya dakika 20 za kwanza kwa kufunga mabao mawili kupitia kwa Seif Karihe dakika ya nane na 18.

Kwa Matokeo hayo Dodoma inafikisha alama tisa na kushika nafasi ya 14 huku mchezo unaofuata wakiwa nyumbani Novemba 22 katika uwanja wa Liti Singida kuwaalika Yanga.

AZAM KUISHUSHA YANGA KILELENI LEO?

 

MZUNGUKO wa 12 wa Ligi Kuu NBC unatarajia kuanza leo Novemba 15,kwa michezo miwili itakayopigwa mkoani Dar es Salaam katika viwanja vya Uhuru na Azam Complex.

Mchezo wa saa 10 alasiri utakaochezwa uwanja wa Uhuru KMC watakua wenyeji wa Dodoma Jiji iliyopoteza mchezo dhidi ya Azam huku kwenye uwanja wa Azam Complex timu ya Azam itaikaribisha Ruvu Shooting ya mkoani Pwani.

Azam inaelekea katika mchezo wake ikiwa katika fomu nzuri ya kupata alama tatu kwenye kila mchezo chini ya Kaimu kocha mkuu Kali Ongala baada ya kushinda katika michezo minne mfululizo dhidi ya Simba,Ihefu,Dodoma Jiji na Mtibwa na kufikisha alama 23 sawa na vinara wa msimamo Yanga.

“Jambo muhimu kwetu kwa sasa ni kupata alama tatu muhimu katika kila mchezo kwani kila mechi ya ligi kuu ni mgumu kutokana na kila timu kuwa na maandalizi ya kushindana”alisema Kali.

Naye kocha msaidizi wa Ruvu Shooting Rajab Mohammed amesema kuwa timu yake imejiandaa vizuri na wamefanyia marekebisho makosa yote yaliyojitokeza michezo ya nyuma hivyo wanaamini wataenda kupata matokeo chanya dhidi katika mchezo wa leo.

“Azam ni timu bora iliyokamilika kila idara,tumeawaona ubora na madhaifu yao na tumewaelekeza vijana namna ya kucheza dhidi yao hivyo tunaamini tutapata matokeo chanya katika mchezo wetu dhidi yao.”alisema Rajab.