Category: STORY

PRISONS MBEYA CITY KUISIMAMISHA MBEYA LEO

Wakazi wa jiji la Mbeya na viunga vyake leo  Septemba 9, 2022 wanakwenda kushuhudia ‘derby’ ya pili ndani ya msimu huu wa 2022/2023 na ya kwanza jijini hapo, ‘Mbeya Derby’ inayozikutanisha Tanzania Prisons na Mbeya City.

Timu hizi zimekutana mara 14 kwenye michezo ya Ligi Kuu ambapo Tanzania Prisons wameshinda mara nne, Mbeya City wakishinda mara tatu huku wakienda sare michezo saba.

Mara ya kwanza kwa timu hizi kukutana ilikuwa ni msimu wa 2015/2016 ambapo mchezo huu ulimalizika kwa Tanzania Prisons kuibuka na ushindi wa bao 1-0.

Katika michezo mitano ya mwisho ya Ligi Kuu timu hizi zilipokutana, Mbeya City wameonekana kuwa wababe kwa Tanzania Prisons, baada ya kuibuka na ushindi mara mbili na kwenda sare mara tatu.

Kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC msimu huu wa 2022/2023 Mbeya City wapo nafasi ya saba wakiwa na alama tatu huku Tanzania Prisons wakiwa nafasi ya tisa na alama zao tatu utofauti ukiwa katika mabao ya kufunga na kufungwa.

KMC WAVUNJA MWIKO KWA SIMBA

Baada ya kusubiri kwa takribani misimu minne ya Ligi kuu bila kupata alama yoyote mbele ya Simba, KMC wamevunja mwiko huo baada ya kupata sare ya mabao mawili jana Septemba 7, 2022 kwenye uwanja wa Benjamin Mkapa.

Kabla ya mchezo wa jana, KMC tangu walipopanda daraja msimu wa 2018/2019 walicheza jumla ya michezo nane ya Ligi Kuu na Simba bila kupata alama yoyote.

Mchezo wa kwanza kuzikutanisha timu hizi ulikua ni Desemba 19, 2018 ambapo mchezo huo ulimalizika kwa Simba kuibuka na ushindi wa mabao 2-1, tangu hapo Simba iliweza kupata matokeo ya ushindi katika michezo saba mfululizo, mechi ya mwisho kwa timu hizi kukutana ilikua ni Juni 19, 2022 katika uwanja wa Benjamin Mkapa na Simba kuifunga KMC kwa Mabao 3-1.

Kwa matokeo hayo KMC wamepanda kwa nafasi mbili kutoka nafasi ya 13 kwenye msimamo hadi nafasi ya 11.

Mchezo unaofuata KMC watakuwa wenyeji wa Ihefu kwenye uwanja wa Uhuru Septemba 17, 2022 saa 10:00 Alasiri

RAUNDI YA TATU IKIENDELEA, KWA MKAPA MOTO KUWAKA TENA LEO

Raundi ya tatu ya Ligi Kuu ya NBC inaendelea tena leo kwa michezo miwili, Mtibwa Sugar watawakabili Ihefu SC kwenye uwanja wa Manungu, Morogoro saa 10:00 Alasiri huku saa 1:00 usiku Simba SC wakicheza na KMC FC kwenye uwanja wa Benjamin Mkapa.

Wakizungumza na waandishi wa habari makocha wa Simba na KMC wamesema hali ya vikosi vyao ipo vizuri kuelekea mchezo huo.

“hatuna majeruhi yoyote ndani ya kikosi chetu wachezaji wote wapo tayari kwa mchezo isipokua Josh Onyango ambaye hakufanya mazoezi na timu “. alisema Selemani Matola Kaimu Kocha Mkuu wa Simba.

Naye Kocha Msaidizi wa KMC Ahmad Alli alisema ” Tunawaheshimu Simba kwasababu ni timu bora, licha ya kutokua na rekodi nzuri mbele yao ila tunakwenda kutafuta alama dhidi yao ‘.

KMC hawajawahi kupata alama yoyote mbele ya Simba katika michezo yote nane ya Ligi Kuu ya NBC tangu walipopanda msimu wa 2018/2019.

Hapo jana mchezo wa kwanza wa ‘Derby’ Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2022/2023 kati ya Yanga SC na Azam FC ulimalizika kwa sare ya mabao mawili kwenye uwanja wa Benjamin Mkapa, mabao yote mawili ya Yanga yalifungwa na Feisal Salum dakika ya 56 na 76 huku yale ya Azam yakifungwa na Daniel Amoah na Malickou Ndoye katika dakika ya 24 na 65.

Yanga wanaendeleza rekodi yao ya kucheza michezo mingi ya Ligi Kuu ya NBC bila kufungwa wakifikisha michezo 40.

Mapema saa 10:00 alasiri kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza Geita Gold walikua wenyeji wa Kagera Sugar na mchezo huo ulimalizika kwa sare ya bao moja, bao la Geita Gold lilifungwa na Seleman Ibrahim dakika ya 74 wakati lile la Kagera Sugar likifungwa na Abeid Athuman dakika ya 44.

 

HAPATOSHI KWA MKAPA LEO

Dar es Saalam na viunga vyake itasimama kwa dakika 90 kupisha mchezo wa kwanza wa ‘derby’ ndani ya msimu huu wa 2022/2023 ukizikutanisha Yanga SC na Azam FC katika uwanja wa Benjamin Mkapa leo Septemba 6, 2022 saa 1:00 usiku.

Mara ya mwisho  timu hizi zilikutana Aprili 6, 2022 katika uwanja wa Azam Complex Chamazi na Yanga kuibuka na ushindi wa mabao 2-1, mabao ya Yanga yalifungwa na Djuma Shabani na Fiston Mayele huku lile la Azam likifungwa na Rodgers Kola.

Ni wachezaji wanne tu kwa kila timu ambao walishiriki katika mchezo wa mwisho timu hizi zilipokutana lakini hivi sasa hawapo na timu hizo, kwa upande wa Yanga wachezaji hao ni Deus Kaseke, Saido Ntibanzokiza, Balama Mapinduzi na Yassin Mustafa huku kwa upande wa Azam wakiwa ni Mudathir Yahya, Charles Zulu, Mathias Kigonya na Never Tigere.

Azam ndio timu ya mwisho kuifunga Yanga kwenye Ligi Kuu kwa bao 1-0, bao lake Prince Dube walipofanya hivyo kwenye msimu wa 2020/2021, baada ya hapo Yanga wamecheza michezo 39 kwenye Ligi Kuu bila kupoteza.

Je ni Yanga kuendeleza rekodi ya kutokufungwa   ama Azam kutibua rekodi hiyo?.

LIGI KUU YA NBC MWENDO MDUNDO

Ligi Kuu ya NBC raundi ya pili imetamatika jana Agosti 21, 2022 kwa michezo minne kuchezwa na kukamilisha jumla ya michezo minane katika raundi ya pili.

Mchezo wa mapema ulizikutanisha Mtibwa Sugar na Ruvu Shooting saa 8:00 mchana katika uwanja wa Manungu, Turiani mkoani Morogoro na Mtibwa Sugar kushinda kwa mabao 2-1. Michezo miwili ya saa 10:00 ilizikutanisha Polisi Tanzania na KMC FC kwenye uwanja wa Sheikh Amri Abeid, Arusha ukimalizika kwa sare ya mabao 2-2 huku ule wa Singida Big Stars na Mbeya City ukimalizika kwa Singida kuibuka na Ushindi wa mabao 2-1.

Mchezo wa Azam FC dhidi ya Geita Gold uliochezwa kwenye uwanja wa Azam Complex majira ya saa 1:00 usiku ndio ulikuwa mchezo wa mwisho kwa raundi ya pili na kumalizika kwa sare ya bao moja.

Simba SC inaendelea kubaki kileleni ikiwa na alama sita ikifuatiwa na Yanga SC yenye alama sita, nafasi ya tatu inashikiliwa na Singida BS ikiwa na alama sita huku utofauti ukiwa katika mabao ya kufunga na kufungwa.

Mabao 20 yamefungwa  katika raundi ya pili na kufanya jumla ya mabao 40 yawe yamefungwa hadi sasa ndani ya msimu huu wa 2022/2023, Reliants Lusajo ndiye anayeongoza mbio za ufungaji akiwa amefunga mabao matatu akifuatiwa na Salum kipemba, Fiston Mayele, Matheo Anthony, Moses Phiri, Nassor Kiziwa, Sixtus Sabilo na Tepsie Evance wakiwa na mabao mawili kila mmoja.

Mpaka hivi sasa ni Ihefu SC pekee ndio ambao hawajafunga bao lolote huku Simba SC ikiwa ndio timu pekee ambayo haijaruhusu bao.

Ligi Kuu ya NBC imesimama hadi Septemba 6, 2022 kupisha mechi za timu ya taifa kuwania kufuzu michuano ya Afrika kwa wachezaji wanaocheza ligi za ndani.