Category: STORY

MZUNGUKO WA PILI LIGI KUU YA NBC

Ligi Kuu ya NBC inaendelea hii leo kwa mchezo mmoja kuchezwa baina ya Ihefu SC na Namungo FC katika uwanja wa Uhuru kuanzia saa 10:00 alasiri.

Ihefu wanatumia uwanja wa Uhuru kama uwanja wao wa nyumbani baada ya uwanja wao wa Highland Estates kufungiwa kutokana na kutokidhi vigezo vya kikanuni na sheria za mpira wa miguu.

Wakiongea na waandishi wa habari kocha wa makipa na nahodha wa kikosi cha Namungo wamesema wapo tayari Kwenda kuwakabili Ihefu SC kwa kuwa wamejiandaa vya kutosha.

“Mchezo wa mwanzo ulikuwa mgumu lakini kwavile tushajua Ligi iko vipi tumejipanga vizuri kuhakikisha tunaondoka na alama tatu,” alisema Faruk Ramadhani Kocha wa makipa wa Namungo.

Wakati huo huo nahodha wa timu hiyo Reliants Lusajo alisema malengo waliyoyapanga msimu uliopita hayakufanikiwa lakini msimu huu wanaamini watafanya vizuri na kuweza kushika nafasi nne za juu.

Kocha na nahodha wa Ihefu SC walishindwa kutokea katika mkutano huo kutokana na kupata changamoto za usafiri wakiwa safarini kuja Dar es saalam.

Raundi ya pili itaendelea tena kesho Agosti 20,2022 kwa michezo mitatu, michezo miwili  ya mapema itazikutanisha Coastal Union na Yanga SC katika uwanja wa Sheikh Amri Abeid, Arusha wakati Dodoma Jiji wakiwakabili Tanzania Prisons kwenye uwanja wa Liti mkoani Singida kuanzia saa 10:00 alasiri.

Mchezo wa mwisho kesho utachezwa saa 1:00 usiku kati ya Simba SC na Kagera Sugar katika uwanja wa Benjamin Mkapa.A

KIVUMBI CHA LIGI KUU YA NBC KUANZA LEO

Pazia la Ligi kuu ya NBC msimu wa 2022/2023 linafunguliwa rasmi  hii leo Agosti 15, 2022 kwa timu nne za Ihefu SC, Ruvu Shooting FC, Namungo FC na Mtibwa Sugar FC  kushuka katika viwanja viwili kuzisaka alama tatu.

Mchezo wa kwanza wa ufunguzi utazikutanisha Ihefu  dhidi ya Ruvu Shooting majira ya saa 10:00 alasiri katika dimba la Highland Estate, Mbarali  Mkoani Mbeya wakati mchezo wa pili utazikutanisha  Namungo dhidi ya Mtibwa Sugar katika dimba la Benjamin Mkapa kuanzia saa 1:00 usiku.

Timu ya Namungo  inatumia uwanja wa Benjamin Mkapa kama uwanja wake wa nyumbani baada ya uwanja wao wa Majaliwa, Lindi kuwa  katika maboresho.

Msimu huu wa 2022/2023 unashirikisha jumla ya timu 16 ambapo kila timu itacheza jumla ya michezo 30 kwa mtindo wa nyumbani na ugenini na  kufanya jumla ya  michezo 240 sawa na michezo 120 nyumbani na 120 ugenini kwa timu zote.

KLABU LIGI KUU ZINAVYOVUNA KUTOKA SEMINA YA UEFA

SEMINA ya Maendeleo ya Ligi inayoendeshwa na UEFA chini ya mradi wao wa UEFA Assist imeingia siku ya nne leo kwenye Hotel ya Golden Tulip iliyopo Dar es Salaam.

Leo washiriki wa semina hiyo inayotarajiwa kukamilika Januari 15, 2022, wamepata nafasi ya kujifunza masuala mbalimbali zikiwemo mbinu za kuziongezea kipato klabu zao.

Mkufunzi wa UEFA Assist, Kenneth Macleod akitoa somo la namna ya kuongeza kipato kwa klabu.

Semina hiyo inashirikisha viongozi na maafisa wa TFF na Bodi ya Ligi, viongozi na maafisa wa Klabu zinazoshiriki Ligi Kuu ya NBC, wajumbe wa Kamati ya Utendaji ya TFF na wajumbe wa Kamati ya Uongozi ya Bodi ya Ligi.

KLABU, TFF, TPLB KUNUFAIKA NA MAFUNZO YA UEFA ASSIST

Tanzania imepata bahati ya kufikiwa na Programu ya UEFA ya Maendeleo ya Mpira wa Miguu (UEFA Assist) ambapo imeandaliwa semina maalum yenye lengo la kuboresha Ligi za Tanzania na Uendeshaji wa Mashindano nchini.

Programu hiyo ilianza Novemba 2021 kwa zoezi la kukusanya maoni ya wadau mbalimbali wakiwemo makocha, wachezaji, Wanahabari, viongozi wa Shirikisho na Bodi ya Ligi, viongozi wa klabu, wadhamini na washabiki.

Hatua ya pili ya Programu hiyo ni semina ambayo itaendeshwa na maafisa wa UEFA Assist kwenye hoteli ya Golden Tulip mkoani Dar es salaam kuanzia Januari 10 hadi 15, 2022.

Washiriki wa semina hiyo ni viongozi na maafisa wa TFF na Bodi ya Ligi, viongozi na maafisa wa klabu za Ligi Kuu (Mwenyekiti/Rais, Katibu/CEO, Mkurugenzi wa Ufundi na Afisa wa Fedha na Mipango).

Baada ya semina hiyo, Programu itaingia katika hatua ya tatu ambapo maafisa wa UEFA Assist watasimamia utekelezaji wa mapendekezo ya maboresho Ligi na Uendeshaji wa Mashindano nchini.