MSIMU wa First League 2025/26 umeendelea kutoa ushindani mkubwa baada ya kila timu kucheza mechi tisa huku vita ya kusaka nafasi ya kupanda Ligi ya NBC Championship ikizidi kupamba moto katika makundi yote mawili.
Kwenye kundi A timu ya Bandari Tanzania inaonekana kuwa na kasi kubwa zaidi baada ya kujikusanyia alama 20, wakiongoza msimamo mbele ya Nyumbu yenye alama 18 huku tofauti ya alama mbili pekee kati ya timu hizo ikionyesha wazi kuwa mbio za kileleni bado hazijaamuliwa na kila mchezo uliosalia utakuwa na uzito mkubwa.
Takwimu za Bandari zinaonyesha uimara mkubwa, wakiwa na ushindi kwenye michezo sita, sare mbili na kupoteza mchezo mmoja pekee, huku safu yao ya ushambuliaji ikiwa tayari imefunga mabao 17.
Nafasi ya tatu inashikiliwa na Cosmopolitan ambayo haipo mbali baada ya kufikisha alama 16, jambo linalofanya kundi A kuwa moja ya makundi yenye ushindani mkali zaidi ambapo tofauti ndogo ya alama kati ya timu tatu za juu ikiashiria kuwa mzunguko wa pili unaweza kubadili kabisa ramani ya msimamo.
Kwa upande wa kundi B timu ya Rhino Rangers imekuwa bora zaidi hadi sasa ikiwa na alama 24 baada ya mechi 9 ikionyesha ubora mkubwa kwa kushinda michezo minane na kupoteza mmoja pekee.
Safu ya ushambuliaji ya ‘maafande’ hao imefunga jumla ya mabao 21, idadi kubwa zaidi kwenye makundi yote mawili ya First League huku wakiruhusu mabao saba pekee huku hii ikiwa sababu kubwa ya kuwa kwenye nafasi kubwa ya kumaliza kileleni na kukata tiketi ya moja kwa moja kuelekea NBC Championship.
Timu za IAA na Endument bado wapo kwenye mbio hizo wakishika nafasi ya pili na tatu ingawa wanalazimika kuongeza kasi ili kuzuia Rhino Rangers wasiweke uwiano mkubwa wa alama zaidi kileleni.
VITA YA MTOANO NA JANGA LA KUSHUKA DARAJA.
Mbali na vita vya juu, pambano la kujiokoa kushuka daraja pia limeanza kuchangamka sana.
Katika kundi A, Dar City inaonekana kuwa kwenye kipindi kigumu zaidi baada ya kubaki mkiani na alama 4 pekee, huku ikiwa tayari imeruhusu mabao 24 na kuwa na rekodi mbaya ya safu ya ulinzi ambayo imekuwa sababu kubwa ya timu hiyo kuwa katika hatari kubwa ya kushuka daraja.
Kwa kundi B hali ni mbaya zaidi kwa ‘Wanajeshi wa mpakani’ timu ya Biashara United ambayo hadi sasa ina deni la alama -1lililotokea baada ya kushindwa kufika uwanjani kwenye michezo miwili na kupokwa alama na mamlaka za soka kitu kinachoonyesha wazi namna walivyoanza msimu vibaya na jinsi kila mchezo uliosalia utakavyokuwa wa kama fainali kwao.
MICHEZO IJAYO KUAMUA HATMA.
Ratiba ya michezo ijayo inaweza kubadilisha kabisa sura ya misimamo yote miwili hasa kwa kundi A ambapo Bandari bado wanakabiliwa na mechi ngumu dhidi ya Nyumbu, Green Warriors na Cosmopolitan.
Kwa kundi B macho yote yataelekezwa kwa Rhino Rangers kuona kama watakuwa na muendelezo mzuri au wapinzani wao wataanza kupunguza ‘pengo’ la alama.
Kwa ujumla, First League msimu huu imeonyesha ushindani wa hali ya juu, mabao mengi, na presha kubwa kuanzia nafasi za juu hadi chini ya msimamo na endapo kasi hii itaendelea mzunguko wa pili unaweza kuwa mmoja wa misimu yenye utofauti mkubwa zaidi kuwahi kushuhudiwa.
Kazi nzuri safi sana
Ilove you my daer
$imba sc