LIGI Kuu ya NBC itaendelea tena mkoani Dar es Salaam leo ambapo timu ya Simba itaikaribisha timu ya Coastal Union katika uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo saa 1:00 usiku.
Kila timu imejiandaa vyema ikizitaka alama zote tatu ili kujiweka katika nafasi nzuri ambapo Simba inataka kujihakikishia iko kwenye mbio za ubingwa huku Coastal Union ikitaka kujiweka katika nafasi nzuri ya kusalia kwenye ligi hiyo msimu ujao.

Simba inashika nafasi ya tatu katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC ikiwa imecheza michezo 14, kushinda michezo tisa sare nne na kupoteza mchezo mmoja na kukusanya alama 31.

Kwa upande wa Coastal Union inashika nafasi ya 13 kwenye msimamo ikiwa na alama 15 katika michezo 16 iliyocheza ikishinda michezo mitatu, sare sita na kupoteza michezo saba.