Kiungo mshambuliaji wa Simba, Elie Mpanzu ameendelea kuthibitisha ubora wake katika Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2025/26 baada ya kuongoza kwenye orodha ya wachezaji wenye pasi nyingi za mabao ambapo hadi sasa amepiga tisa (9).
Mpanzu amekuwa mhimili muhimu katika safu ya ushambuliaji ya Simba, akichangia si kwa ubunifu wa kutengeneza nafasi za mabao pekee bali pia kwa ushirikiano mzuri na washambuliaji wa timu hiyo jambo lililoifanya Simba kuendelea kuwa na ushindani mkubwa katika mbio za ubingwa.
Anayemfuatia kwa karibu ni kiungo wa Azam, Feisal Salum mwenye asisti nane (8).
Feisal ameendelea kuonyesha kiwango cha juu msimu huu kwa kuwa miongoni mwa wachezaji wanaotengeneza nafasi nyingi za kufunga kwa wenzake.
Katika nafasi ya tatu kuna kundi la wachezaji wanne wenye pasi saba (7) kila mmoja.
Hawa ni Allan Okello wa Young Africans, Iddi Selemani wa Azam, Clatous Chama wa Simba na Zabona Mayombya wa Pamba Jiji.
Orodha hiyo inakamilishwa na wachezaji wawili wa Young Africans ambao ni Duke Abuya na Maxi Nzengeli wenye pasi sita (6).
Kwa ushindani unaoendelea katika hatua za mwisho za msimu huu mbio za kinara wa pasi nyingi za mabao bado zipo wazi huku tofauti ya pasi chache ikiwatenganisha vinara hao, Swali ni nani atamaliza msimu akiwa kinara wa ubunifu katika Ligi Kuu ya NBC 2025/26.