Ligi ya NBC Championship imetimiza mzunguko wa 21 huku ushindani ukizidi kupamba moto, timu zikionyesha wazi dhamira ya kupigania kupanda daraja kwenda Ligi Kuu ya NBC msimu ujao na nyingine zikipambana kusalia ligi hiyo msimu ujao.
Katika hatua hii ya ligi, kila alama imekuwa ya thamani kubwa, huku timu za juu ambazo ni Geita Gold, Kagera Sugar,Mbeya Kwanza na Transit Camp zikionekana kuongeza kasi ili kujihakikishia nafasi za moja kwa moja za kupanda daraja na mapambano hayo yameifanya ligi kuwa na mvuto mkubwa zaidi, ambapo matokeo ya kila wiki yamekuwa yakibadilisha mwelekeo wa msimamo wa ligi hiyo.
Kwa upande wa katikati ya msimamo penye timu za Bigman yenye alama yenye alama 27 ikishika nafasi ya saba, KenGold inafuata ikiwa na alama 26 sawa na Songea United na Gunners inayoshika nafasi ya 10 ikiwa imekusanya alama 23 hali inaendelea kuwa ngumu kwa timu hizo ambazo zinajikuta zikihitaji ushindi mfululizo ili kuepuka kuingia kwenye hatari ya kushuka daraja na jambo hil limeongeza ushindani mkali, kwani tofauti ya pointi kati ya timu hizo ni ndogo sana.
Wakati huo huo, timu za ‘mkiani’ ambazo ni African Sports inayoshika nafasi ya 15 na Barberian inayoshika nafasi ya 16 zinapambana kwa nguvu zote kujiokoa, hali inayofanya kila mechi kuwa ya ushindani wa hali ya juu na presha imekuwa kubwa kwa wachezaji na benchi la ufundi, huku makosa madogo yakigharimu matokeo makubwa.
Ligi hiyo pia imeendelea kuwa jukwaa muhimu kwa wachezaji kuonyesha viwango vyao, ambapo baadhi yao kama Obrey Chirwa anayekipiga kwenye timu ya Kagera Sugar anayeongoza mbio za ufungaji na Ramadhan Karanje wa B19 aliyeibuka mchezaji bora wa mwezi Februari wameanza kuvutia macho ya klabu kubwa kutokana na kiwango wanachoonyesha uwanjani.
Kadri msimu unavyozidi kusonga mbele, wachambuzi wa soka wanaamini kuwa ushindani utaongezeka zaidi, hasa katika nafasi za juu zinazoongozwa na kinara Geita Gold zinazotoa tiketi ya kupanda Ligi Kuu ya NBC pamoja na zile za mkiani zinazohusisha mapambano ya kuepuka kushuka Ligi ya First League.
Kwa sasa, macho ya wadau wa soka yameelekezwa kwenye hatua zijazo za ligi hiyo iliyosimama kwa takribani mwezi mmoja, wakisubiri kuona ni timu zipi zitafanikiwa kuhimili presha na kuandika historia ya kupanda daraja mwishoni mwa msimu na zipi zitaweza kuamka na kusalia kwenye ligi msimu ujao.