TIMU za Singida Big Stars ya mkoani Singida na Simba SC ya Dar es Salaam zimeshindwa kutambiana kwenye uwanja wa CCM Liti baada ya kutoka sare ya bao moja.
Katikati ya watazamaji Zaidi ya elfu 11 waliofurika uwanjani kutazama mchezo huo wa Ligi Kuu NBC, Singida ilikuwa ya kwanza kupata bao lililowapeleka mapumziko kifua mbele kupitia kwa Deus Kaseke dakika ya 11, akiunganisha krosi ya mchezaji wa zamani wa Simba, Said Ndemla.
Simba walipata bao lao la kusawazisha dakika ya 58 kupitia kwa Peter Banda aliyeingia kipindi cha pili kuchukua nafasi ya Jonas Mkude.
Matokeo hayo yanaifanya Simba kufikisha alama 18 na kushika nafasi ya pili kwenye msimamo sawa na Singida waliopo nafasi ya tatu wakitofautiana kwa mabao ya kufunga na kufungwa.
Azam FC imepata ushindi wa tatu mfululizo katika Ligi Kuu NBC baada ya kuifunga timu ya Dodoma Jiji mabao 2-1 kwenye uwanja wa Azam Complex, Dar es Salaam.
Mabao ya Azam katika mchezo huo yamefungwa na Ismael Aziz Kader dakika ya 37 na Idris Mbombo dakika ya 89 huku bao pekee la Dodoma likifungwa na Collins Opare dakika 41.
Matokeo hayo yanaifanya Azam kufikisha alama 20 sawa na vinara wa Ligi Yanga wakitofautiana kwa magoli ya kufunga na kufungwa huku Dodoma ikisalia na alama sita katika nafasi ya 14 ya msimamo wa ligi ya NBC.
Ligi Kuu NBC itaendelea tena Novemba 10 katika uwanja wa Sokoine Jijini Mbeya kwa mchezo kati ya Tanzania Prisons na Coastal Union ya Tanga.