Tag: #championship

TRANSIT YAFUKUZA ‘MWIZI’ KIMYA, BIGMAN, GEITA HAKUNA MBABE NBC CHAMPIONSHIP.

TIMU ya Transit Camp imerejea katika matokeo ya ushindi baada ya kuifunga KenGold bao moja kwenye uwanja wa nyumbani na kufanikiwa kusalia na alama zote tatu.

Mchezo huo uliopigwa uwanja wa TFF Center Kigamboni ulishuhudia Adam Uledi wa Transit Camp akiibuka shujaa kwa kuifungia Transit bao pekee kipindi cha pili kwa mkwaju wa penati huku likiwa bao la 11 kwake akiendelea kuongoza kwenye vinara wa mabao katika ligi ya Championship ya NBC.

Ushindi huo unaifanya Transit kufikisha alama 33 na kupanda hadi nafasi ya tatu ya msimamo ikiwa nyuma ya kinara wa ligi hiyo Geita Gold kwa alama nne pekee.

Mkoani Lindi kwenye uwanja wa Ilulu timu ya Bigman ilikuwa mwenyeji wa Geita Gold na kushuhudia mchezo huo ukikamilika kwa timu hizo kutoka sare ya bao moja.

Geita inayoongoza msimamo wa ligi hiyo kwa alama 37 imeshindwa kukusanya alama zote nyumbani kwa Bigman ambayo imeizidi alama 17 huku timu hiyo (Bigman) ikishika nafasi ya saba kwenye msimamo.

Hii ni sare ya pili mfululizo kwa timu ya Bigman kwenye uwanja wa nyumbani baada ya mchezo uliopita kulazimishwa sare na timu ya African Sports kutoka Tanga.

MTIBWA WABABE WA NAMBA NBC CHAMPIONSHIP MPAKA SASA.

JUMLA ya Michezo 136 kati ya 240 imeshachezwa kwenye Ligi ya Championship ya NBC msimu wa 2024/2025 na kushuhudia jumla ya mabao 297 yakifungwa kwenye michezo hiyo huku Mtibwa Sugar ikiwa kinara kwa kufunga mabao mengi.

Mtibwa imefunga jumla ya mabao 31 kwenye michezo 17 mengi zaidi kuliko timu yeyote kwenye Ligi ya Championship ya NBC hadi sasa huku ikiruhusu kufungwa mabao saba pekee machache zaidi kuliko timu yeyote kwenye Ligi hiyo.

Mtibwa inaongoza msimamo wa Ligi ya Championship ya NBC ikiwa na alama 44 baada ya michezo 17 ikishinda michezo 14 ikipata sare michezo miwili na kufungwa mchezo mmoja pekee.

 

MZUNGUKO WA 17 NBC CHAMPIONSHIP KUKAMILIKA LEO.

MZUNGUKO wa 17 wa Ligi ya Championship ya NBC unatamatika leo kwa mchezo kati ya Transit Camp ya Dar es salaam na Stand United ya Shinyanga saa 10:00 alasiri katika uwanja wa Mabatini Mkoani Pwani.

Transit Camp ipo nafasi ya 13 kwenye msimamo wa Ligi ya Championship ya NBC ikiwa na alama 10 sawa na Kiluvya iliyo nafasi ya 14 zikitofautiana kwenye mabao ya kufunga na kufungwa huku Stand United ikiwa nafasi ya nne (4) na alama 32.

Mpaka sasa Mtibwa Sugar inaongoza kwenye msimamo wa Ligi ya Championship ya NBC ikiwa na alama 44 kwenye michezo 17 wakati Biashara United ikishika nafasi ya mwisho ikiwa na alama nne (4) pekee kwenye michezo 17

NBC CHAMPIONSHIP MZUNGUKO WA 16 KUPIGWA MIKOA MITATU LEO.

MZUNGUKO wa 16 wa Ligi ya Championship ya NBC unaanza kuchezwa leo Januari 24 kwa michezo mitatu kuchezwa kwenye mikoa mitatu tofauti.

Mchezo wa kwanza utazikutanisha Mbeya Kwanza dhidi ya Songea United kwenye uwanja wa Nangwanda Sijaona Mkoani Mtwara kuanzia saa 10:00 alasiri.

Mchezo wa pili utazikutanisha African Sports dhidi ya Cosmopolitan kwenye uwanja wa TFF Center, Mnyanjani – Tanga kuanzia saa 10 alasiri.

Mkoani Pwani Green Warriors itaikaribisha Mtibwa Sugar kwenye uwanja wa Mabatini mchezo ambao utachezwa kuanzia saa 10:00 alasiri.

Mtibwa Sugar ndio kinara wa Ligi ya Championship ya NBC mpaka sasa ikiwa na alama 38 kwenye michezo 15 ya kwanza huku Biashara United ikiburuza mkia ikiwa na alama moja baada ya michezo 15.