Tag: #LIGIKUU #NBCPL #AZAM #YANGA #SIMBA #KMC #JKT #MASHUJAA #KENGOLD #DODOMAJIJI #PAMBAJIJI #KAGERASUGAR #SINGIDABLACKSTARS #FOUNTAINGATE #NAMUNGO

YOUNG AFRICANS, SIMBA ‘HAWAFUNGIKI’ UGENINI LIGI KUU YA NBC.

KLABU za Simba na Young africans ni timu pekee za Ligi Kuu ya NBC ambazo hazijafungwa kwenye mchezo wowote wa ugenini msimu huu zikicheza michezo 27 kila moja.

Young Africans katika msimu huu wa Ligi Kuu imefanikiwa kucheza michezo 14 viwanja vya ugenini na kufanikiwa kushinda michezo 13 huku ikipata sare moja na ikivuna alama 40 ikiweka ‘kimiani’ mabao 35 na kuruhusu mabao mawili pekee.

Kwa upande wa timu ya Simba imefanikiwa kucheza michezo 13 ugenini ikishinda michezo 12, sare moja na kuvuna alama 37 baada ya kufunga mabao 25 na kuruhusu mabao manne pekee.

Ligi Kuu ya NBC itaendelea juni 15 kwa mchezo wa dabi ya Kariakoo ambapo timu ya Young Africans itakuwa mwenyeji wa timu ya Simba katika uwanja wa Benjamin Mkapa mkoani Dar es Salaam saa 11:00 jioni.

HAWA HAPA WAKALI WA KUPIKA MABAO LIGI KUU YA NBC.

KIUNGO wa Simba Jean Ahoua ameendeleza ubabe akihusika katika mabao mengi zaidi kuliko wachezaji wengine wa Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2024/2025 hadi sasa.

Ahoua ambaye amejiunga na Simba mwanzoni mwa msimu amefanikiwa kufunga mabao 15 na kutoa pasi za mabao nane hivyo kuhusika katika mabao 23.

Prince Dube wa Young Africans anashika nafasi ya pili baada ya kuhusika katika mabao 21 akifanikiwa kutikisa nyavu za wapinzani mara 13 na kutoa pasi za mabao nane ikiwa ni msimu wake wa kwanza ndani ya timu hiyo akitokea Azam FC.

Pacome Zouzoua wa Young Africans nae hajabaki nyuma akiwa amefanikiwa kuhusika katika mabao 18 baada ya kufunga mabao 9 na kutoa pasi za mabao 9.

Kwa upande wake Feisal Salum wa timu ya Azam amehusika katika mabao 17 akiwa ametoa pasi za mabao 13 na kufunga mabao 6 huku akiwa kinara wa kutoa pasi za mabao.

MUKWALA MCHEZAJI BORA MEI, FADLU HASHIKIKI LIGI KUU NBC.

MSHAMBULIAJI wa timu ya Simba, Steven Mukwala amechaguliwa kuwa Mchezaji Bora wamwezi Mei wa Ligi Kuu ya NBC msimu wa mwaka 2024/25, huku Fadlu Davids akichaguliwa Kocha Bora wa ligi hiyo kwa mwezi huo.

Mukwala alionesha kiwango kizuri chenye mwendelezo akiwashinda Jean Charles Ahoua pia wa Simba na Jafari Kibaya wa Mashujaa, alioingia nao fainali katika mchakato waTuzo za Mwezi uliofanywa na Kamati ya Tuzo za Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania(TFF).

Mchezaji huyo alitoa mchango mkubwa kwa timu yake katika michezo minne aliyocheza mwezi huo na kufunga mabao matatu na kuhusika na lingine moja kwa dakika 233 alizocheza.

Kwa upande wa Fadlu aliyeingia fainali na Miloud Hamdi wa Yanga na Rachid Touassi wa Azam, aliiongoza Simba kushinda michezo yote mitano iliyocheza mwezi huo na

kuendelea kushika nafasi ya pili kwenye msimamo wa ligi. Simba ilizifunga Singida Black Stars (1-0), KMC (1-2), Pamba Jiji (5-1), Mashujaa (2-1) na JKT Tanzania (0-1).

Pia Kamati ya Tuzo imemchagua Meneja wa Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, Ashraf Omar kuwa Meneja Bora wa Uwanja kwa mwezi Mei kutokana na kufanya vizuri katika menejimenti ya matukio ya michezo pamoja na masuala yanayohusu miundombinu uwanjani.

Wakati huohuo Kamati ya Tuzo za TFF, imemchagua Frank Edmund Rutha wa African Sports kuwa Mchezaji Bora wa Mwezi Mei wa Ligi ya NBC Championship 2024/25, huku Malale Hamsini wa Mbeya City akichaguliwa Kocha Bora wa mwezi huo.

Frank aliyeingia fainali na Kilaza Mazoea na Eliud Ambokile wote wa Mbeya City,alionesha kiwango kizuri ikiwa ni pamoja na kufunga mabao manne kwa dakika 170 alizocheza za michezo miwili.

Kwa upande wa Malale aliyeingia fainali na Kessy Abdallah wa African Sports na Abdul Mingange wa Songea United, aliiongoza timu yake kushinda michezo yote miwili iliyocheza na kuiwezesha kupanda Ligi Kuu ya NBC msimu 2025/2026.

CAMARA ‘ANG’ANG’ANIA’ KILELENI HATI SAFI LIGI KUU YA NBC.

GOLIKIPA wa timu ya Simba Moussa Camara ameendeleza ubabe wake kwa kuendelea kukaa kileleni kwa kuwa na hati safi (Cleansheet) nyingi (17) kuliko magolikipa wenzake wa Ligi Kuu ya NBC kwa msimu 2024/2025.

Camara ambaye ni msimu wake wa kwanza kwenye Ligi Kuu ya NBC amefanikiwa kukusanya hati safi hizo katika michezo 25 ya Ligi Kuu aliyocheza mpaka sasa huku akifanikiwa kuendelea kuwa juu ya msimamo wa hati safi huku Djigui Diarra wa Young Africans akiwa nafasi ya pili baada ya kukusanya hati safi 15.

Patrick Munthali wa Mashujaa anashikilia nafasi ya tatu akiwa na hati safi 12 huku Mohamed Mustapha wa Azam na Yona Amos wa Pamba Jiji wakiwa nazo 10 kila mmoja.

Yakoub Suleiman wa JKT Tanzania nae hayuko mbali akiwa amefanikiwa kukusanya hati safi 8 huku Metacha Mnata wa Singida Black Stars na Ngaleka Katembua wa Dodoma Jiji wakiwa wamefanikiwa kukusanya hati safi 7 kila mmoja huku ikisalia mizunguko miwili kutamatika kwa msimu wa 2024/25.

YOUNG AFRICANS YASHIKILIA ‘USUKANI’ LIGI KUU YA NBC.

LIGI Kuu ya NBC inazidi kushika kasi Iikielekea ukingoni huku timu ya Young Africans ikiendelea ilipoishia baada ya kuichapa Namungo 3-0 kwenye uwanja wa KMC Complex mkoani Dar es Salaam.

Ilimchukua dakika 27 kiungo wa Young Africans Aziz Ki kufungua ukurasa wa mabao na dakika nne baadae mshambuliaji wa timu hiyo raia wa Zimbabwe Prince Dube aliipatia timu yake bao la pili hivyo kwenda mapumziko ikiongoza 2-0.

Kipindi cha pili kilianza kwa kasi timu ya Namungo ikionekana kusaka namna ya kupata bao ambapo juhudi zao hazikuzaa matunda na dakika ya 74 mchezaji wa Young Africans Maxi Nzegeli aliipatia timu yake bao la tatu na mpaka dakika 90 zinatimia ubao wa matokeo ulikuwa unasoma 3-0.

Matokeo hayo yanaifanya Young Africans kufikisha alama 73 na kuendelea kuongoza Ligi Kuu ya NBC huku timu hiyo ikisaliwa na michezo mitatu kuhitimisha Ligi hiyo.

Mchezaji wa Young Africans Maxi Nzegeli alichaguliwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo kutokana na kiwango kizuri alichoonyesha katika mchezo huo akifunga bao na kutoa pasi ya bao la Stephane Aziz Ki.