TIMU ya Azam yenye maskani yake kwenye uwanja wa Azam Complex imekuwa moto wa kuotea mbali msimu huu ikiwa haijapoteza mchezo wowote wa Ligi Kuu ya NBC hadi sasa.
Mchezo uliopita Azam ilishinda dhidi ya Coastal Union kwenye uwanja wa nyumbani kwa mabao 3-0 yaliyofungwa na Yahya Zayd, Feisal Salum na Jephte Kitambala huku mabao yote yakifungwa kipindi cha kwanza na kudumu kwa dakika zote 90.
Azam imefunga mabao 9 na kuruhusu mabao mawili pekee huku ikiwa imetoka sare michezo mitatu hadi sasa kwenye Ligi Kuu ya NBC.
Timu hiyo inaingia mawindoni kulisaka taji la Ligi Kuu ya NBC baada ya kulikosa kwa miaka 13 wakiwa na matumaini ya kufanya hivyo msimu huu chini ya kocha Florent Ibenge ambaye hadi sasa amewasaidia kufuzu hatua ya makundi ya mashindano ya Afrika kwa mara ya kwanza kuanzia timu hiyo ianzishwe.
Mara ya mwisho timu ya Azam kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu ilikuwa mwaka 2013 na walitwaa bila kupoteza mchezo wowote.