Tag: #NBCCL#STORY

AZAM YA IBENGE NI MOTO WA KUOTEA MBALI LIGI KUU YA NBC.

TIMU ya Azam yenye maskani yake kwenye uwanja wa Azam Complex imekuwa moto wa kuotea mbali msimu huu ikiwa haijapoteza mchezo wowote wa Ligi Kuu ya NBC hadi sasa.

Mchezo uliopita Azam ilishinda dhidi ya Coastal Union kwenye uwanja wa nyumbani kwa mabao 3-0 yaliyofungwa na Yahya Zayd, Feisal Salum na Jephte Kitambala huku mabao yote yakifungwa kipindi cha kwanza na kudumu kwa dakika zote 90.

Azam imefunga mabao 9 na kuruhusu mabao mawili pekee huku ikiwa imetoka sare michezo mitatu hadi sasa kwenye Ligi Kuu ya NBC.

Timu hiyo inaingia mawindoni kulisaka taji la Ligi Kuu ya NBC baada ya kulikosa kwa miaka 13 wakiwa na matumaini ya kufanya hivyo msimu huu chini ya kocha Florent Ibenge ambaye hadi sasa amewasaidia kufuzu hatua ya makundi ya mashindano ya Afrika kwa mara ya kwanza kuanzia timu hiyo ianzishwe.

Mara ya mwisho timu ya Azam kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu ilikuwa mwaka 2013 na walitwaa bila kupoteza mchezo wowote.

NBC CHAMPIONSHIP YAFIKA PATAMU.

IKIKAMILISHA mizunguko 15 Ligi ya NBC Championship imepamba moto timu zote zikiwa zimecheza michezo 15 huku zikisaliwa na michezo 15 kufunga msimu.

Geita Gold inaongoza mbio za ubingwa ikiwa na alama 37 baada ya kushinda michezo 11 huku ikiwa timu pekee ambayo haijapoteza mchezo wowote hadi sasa.

Kagera Sugar inashika nafasi ya pili ikiwa na alama 36 ikipoteza mchezo mmoja pekee kwenye mzunguko wa 15 dhidi ya ‘wababe’ wa mkoa wa Tabora timu ya Mbeya Kwanza inayokamata nafasi ya tatu ikiwa na alama 34.

Transit Camp inashika nafasi ya nne ikiwa na alama 33 ikizidiwa alama nne pekee na vinara wa ligi hiyo timu ya Geita Gold, Transit ikiwa imeshinda michezo 10 hadi sasa, ikipoteza miwili na kutoa sare mitatu.

Bingwa wa ligi ya Championship ya NBC atapata Kikombe na kupanda daraja moja kwa moja hadi Ligi Kuu ya NBC, mshindi wa pili akipanda daraja huku mshindi wa tatu na wa nne wakicheza mchezo wa mtoano na timu itakayoshinda kwenye matokeo ya jumla itacheza na timu ya Ligi Kuu ya NBC ili kupata timu moja itakayoshiriki ligi hiyo ya nne kwa ubora Afrika msimu wa 2026/27.

TRANSIT YAFUKUZA ‘MWIZI’ KIMYA, BIGMAN, GEITA HAKUNA MBABE NBC CHAMPIONSHIP.

TIMU ya Transit Camp imerejea katika matokeo ya ushindi baada ya kuifunga KenGold bao moja kwenye uwanja wa nyumbani na kufanikiwa kusalia na alama zote tatu.

Mchezo huo uliopigwa uwanja wa TFF Center Kigamboni ulishuhudia Adam Uledi wa Transit Camp akiibuka shujaa kwa kuifungia Transit bao pekee kipindi cha pili kwa mkwaju wa penati huku likiwa bao la 11 kwake akiendelea kuongoza kwenye vinara wa mabao katika ligi ya Championship ya NBC.

Ushindi huo unaifanya Transit kufikisha alama 33 na kupanda hadi nafasi ya tatu ya msimamo ikiwa nyuma ya kinara wa ligi hiyo Geita Gold kwa alama nne pekee.

Mkoani Lindi kwenye uwanja wa Ilulu timu ya Bigman ilikuwa mwenyeji wa Geita Gold na kushuhudia mchezo huo ukikamilika kwa timu hizo kutoka sare ya bao moja.

Geita inayoongoza msimamo wa ligi hiyo kwa alama 37 imeshindwa kukusanya alama zote nyumbani kwa Bigman ambayo imeizidi alama 17 huku timu hiyo (Bigman) ikishika nafasi ya saba kwenye msimamo.

Hii ni sare ya pili mfululizo kwa timu ya Bigman kwenye uwanja wa nyumbani baada ya mchezo uliopita kulazimishwa sare na timu ya African Sports kutoka Tanga.

PAZIA LA NBC CHAMPIONSHIP KUFUNGWA LEO.

KILELE cha ligi ya Championship ya NBC msimu wa 2024/25 kinatarajiwa kufikiwa leo kwa mchezo wa kukabidhi ubingwa kati ya Mtibwa Sugar na Mbeya City utakaopigwa leo kwenye uwanja wa Azam Complex, Dar es Salaam saa 2:00 usiku.

Ligi hiyo ilifika tamati Mei 11, kwa michezo nane kupigwa na Mtibwa Sugar kumaliza bingwa na kupanda daraja akifikisha jumla ya alama 71 huku Mbeya City ikimaliza nafasi ya pili na kujihakikishia nafasi ya kushiriki Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2025/26 sambamba na Mtibwa.

Mtibwa Sugar imerejea Ligi Kuu ya NBC ikiwa ni msimu mmoja pekee tangu kushuka daraja huku Mbeya City ikitumia misimu miwili kurejea ligi hiyo.

Mchezo wa leo utarushwa mubashara TV3 na utakuwa sambamba na sherehe za kukabidhi ubingwa kwa timu ya Mtibwa Sugar baada ya kumaliza nafasi ya kwanza kwenye msimamo wa ligi ya Championship ya NBC.

TABORA, KMC KUFUNGA MZUNGUKO WA 28 LIGI KUU YA NBC.

MZUNGUKO wa 28 unatarajiwa kukamilika leo kwa mchezo mmoja utakaozikutanisha timu za Tabora United kutoka mkoani Tabora dhidi ya KMC ya Dar es Salaam saa 10:00 alasiri kwenye uwanja wa Ali Hassan Mwinyi, Tabora.

KMC itashuka ugenini ikiwa na kumbukumbu mbaya ya kupoteza mchezo wake uliopita dhidi ya Simba kwa mabao 1-2 kwenye uwanja wake wa nyumbani.

Hadi sasa ikicheza viwanja vya ugenini KMC imeshinda mchezo mmoja pekee, kufungwa michezo saba huku ikitoka sare minne na kukusanya alama saba pekee.

Tabora inashuka uwanjani ikiwa haijafanikiwa kupata ushindi kwenye michezo mitano mfululizo ya Ligi Kuu ya NBC na mara ya mwisho kushinda ilikuwa kwenye mchezo dhidi ya Dodoma Jiji kwa bao moja lililofungwa na Offen Chikola kwenye uwanja wa Ali Hassan Mwinyi, Tabora.