TIMU ya Azam imeonyesha ubora na ukomavu mkubwa baada ya kuibuka na ushindi muhimu wa mabao 2-1 dhidi ya Singida Black Stars kwenye mchezo wa Ligi Kuu ya NBC uliopigwa Airtel Stadium, Singida.
Baada ya kutoka sare mbili mfululizo bila kufungana, kikosi hicho cha kocha Florent Ibenge kilirejea kwa nguvu na kuonyesha dhamira ya kupambania nafasi za juu kwenye msimamo wa ligi hiyo.
Bao la kwanza la Azam lilifungwa mapema kipindi cha pili kupitia kwa nahodha Lusajo Mwaikenda aliyemalizia kwa ustadi mpira wa krosi uliotengenezwa na Iddy Seleman ‘Nado’.
Dakika chache baadaye, staa wa timu hiyo Feisal Salum “Fei Toto” aliandika bao la pili kwa shuti la utulivu baada ya kupokea pasi safi kutoka kwa ‘Nado’ bao ambalo liliongeza presha kubwa kwa wenyeji Singida.
Singida Black Stars walijitahidi kurejea mchezoni na kufanikiwa kupata bao moja kupitia kwa Ayubu Lyanga dakika ya 71, lakini juhudi zao za kusawazisha ziligonga mwamba mbele ya safu imara ya ulinzi ya ‘Matajiri wa chamazi’.
Matokeo hayo yanaifanya Azam kuendelea kuwepo kwenye mbio za ubingwa msimu huu ikikwea hadi nafasi ya pili baada ya kukusanya alama 32 huku ikionyesha kuwa bado ni tishio kubwa kwa vigogo wengine wa ligi, hasa kuelekea ‘duru’ la mwisho la Ligi Kuu ya NBC.