DODOMA JIJI, MBEYA CITY ZAWASHA MOTO LIGI KUU YA NBC.

LIGI Kuu NBC imeendelea jana kwa michezo miwili iliyotoa burudani ya viwango ambapo Dodoma Jiji iliichapa Fountain Gate mabao 3-0, huku Mbeya City ikiibuka na ushindi wa kusisimua wa 3-2 dhidi ya KMC.

Katika mchezo uliopigwa Airtel Stadium, Singida, wenyeji Dodoma Jiji walionyesha ubora mkubwa hasa kipindi cha pili na kuondoka na alama tatu muhimu mbele ya Fountain Gate baada ya kipindi cha kwanza kumalizika wakiwa kifua mbele kwa bao moja kupitia kwa nahodha Augustino Nsata aliyefunga dakika ya 38.

Iddi Kipagwile aliongeza bao la pili dakika ya 69 na dakika za nyongeza Yasin Mgaza alihitimisha ushindi huo kwa bao la tatu dakika ya 90+1 na kuifanya Dodoma kushinda kwa kishindo 3-0.

Ushindi huo unaifanya Dodoma kuendelea kuimarisha nafasi yao katikati ya msimamo wa ligi ikikaa nafasi saba ikiwa imekusanya alama 24.

Kwa upande mwingine, katika mchezo uliochezwa Tanzanite Kwaraa, Manyara, mashabiki walishuhudia moja ya mechi tamu zaidi za wiki hii baada ya Mbeya City kuifunga KMC 3-2.

KMC ilikuwa ya kwanza kupata bao kupitia kwa Oscar Paul dakika ya 44, na kwenda mapumziko wakiwa mbele.

Kipindi cha pili Mbeya City walibadilika kabisa, wakisawazisha kupitia Riphat Msuya dakika ya 64, kabla ya Adili Buha kufunga kwa penalti dakika ya 76 na kuwapa uongozi wenyeji.

Hata hivyo, KMC hawakukata tamaa na walifanikiwa kusawazisha dakika ya 78 kupitia Juma Shemvuni, jambo lililoongeza presha kubwa kwa wenyeji Mbeya City.

Wakati mchezo ukionekana kuelekea sare, Said Naushad alitokea kuwa shujaa wa Mbeya City kwa kufunga bao la ushindi dakika ya 86, na kuamsha shangwe kubwa Tanzanite Kwaraa. 

Matokeo hayo yana maana kubwa kwenye mbio za msimamo wa ligi, hasa kwa Mbeya City ambao walikuwa wanahitaji sana ushindi huo kujinasua kutoka maeneo ya hatari ya msimamo wa Ligi Kuu ya NBC.

Kwa ujumla, jana ilikuwa siku ya mabao 8 kwenye michezo miwili, ushindi wa kishindo kwa Dodoma Jiji na ushindi wa jasho kwa Mbeya City, matokeo ambayo yanaongeza ushindani mkubwa zaidi msimu huu.

Start a Conversation

Your email address will not be published. Required fields are marked *