VIWANJA vitatu vya Ligi Kuu NBC vinaendelea kutoa burudani leo kwa ratiba ya michezo mitatu inayotarajiwa kuwa na ushindani mkubwa huku kila timu ikihitaji alama kwa malengo tofauti msimu huu.
Macho mengi yataelekezwa katika viwanja vya Lake Tanganyika, Kigoma, KMC Complex, Dar es Salaam na Majaliwa, Lindi ambako mapambano ya kibingwa yanayohusisha vita ya nafasi za juu pamoja na presha ya kushuka daraja kupamba moto.
Katika mchezo wa mapema utakaochezwa saa 10:00 jioni kwenye Uwanja wa Lake Tanganyika, Mashujaa FC watawakaribisha Pamba Jiji kwenye mechi inayobeba uzito mkubwa kwa timu zote mbili.
Mashujaa wakiwa nyumbani watataka kutumia faida ya mashabiki wao kutafuta ushindi muhimu baada ya kushindwa kupata matokeo mchezo uliopita dhidi ya Fountain Gate huku Pamba Jiji wakisaka matokeo chanya yatakayowaweka kwenye nafasi salama zaidi kwenye msimamo wa ligi.
Mechi hii inatarajiwa kuwa ya nguvu nyingi katikati ya uwanja kutokana na timu zote kupenda kucheza kwa presha huku wakitumia zaidi viungo wa kati kuliko viungo wa pembeni.
Mchezo mwingine mkubwa wa leo utakuwa kati ya Young Africans watakapowakaribisha Tanzania Prisons katika uwanja wa KMC Complex, Dar es Salaam saa 12:30 jioni.
Young Africans wakiwa kwenye mbio za kuwania ubingwa hawana nafasi ya kupoteza alama na ushindi wa leo unaweza kuongeza presha kwa wapinzani wao kwenye kilele cha msimamo.
Tanzania Prisons nao wanakuja na morali ya kutafuta matokeo ya kushtua wakifahamu kupata alama dhidi ya timu kubwa kunaweza kubadili kabisa mwenendo wao wa msimu huu.
Usiku wa leo saa 3:00 usiku timu ya Namungo FC itawakaribisha JKT Tanzania kwenye uwanja wa Majaliwa katika pambano jingine linalosubiriwa kwa hamu.l kukamilisha burudani za siku ya leo.
Namungo wamekuwa timu ngumu sana inapocheza nyumbani jambo linalowapa nguvu dhidi ya JKT Tanzania ambao nao mara nyingi huonekana kuwa na nidhamu kubwa ya kiuchezaji chini ya kocha Ahmad Ally ambaye pia ni kocha msaidizi wa timu ya Taifa ya Tanzania.
Hii inaweza kuwa moja ya mechi ngumu zaidi ya leo kutokana na ubora unaokaribiana kwa pande zote mbili.
Kwa ujumla, ratiba ya leo inaweza kuleta mabadiliko makubwa kwenye msimamo wa ligi hasa kwa timu zinazowania ubingwa, nafasi za juu na zile zinazokwepa hatari ya kushuka daraja.
Mashabiki wanatarajia kuona mabao, ushindani mkali na matokeo yatakayoongeza joto la NBC Premier League kuelekea hatua za mwisho za msimu huku kila timu ikitaka kumaliza kwa furaha na mafanikio.