Author: Cynthia Michael

SINGIDA, FOUNTAIN, AZAM ZATAMBA LIGI KUU YA NBC.

LIGI Kuu ya NBC imeendelea kwa michezo iliyochezwa katika mikoa ya Arusha,Singida na Dar es salaam.

Katika dimba la Singida, timu ya Singida Black Stars waliwakaribisha Pamba Jiji katika mchezo uliokuwa na kasi na ushindani mkubwa ulioshuhudia wenyeji wakionyesha ubora wao kwa kupata ushindi wa 3-1.

Mabao mawili yaliwekwa kambani na Ndumumwe Mossi aliyefunga dakika ya 21 na kuongeza lingine dakika ya 53 huku Horso Malanga akijiunga kwenye orodha ya wafungaji kwa bao la dakika ya 70 na kuhakikisha Singida wanakusanya alama zote tatu.
Bao pekee la Pamba Jiji lilifungwa na Henry Lutonja dakika ya 90 ingawa haikutosha kuzuia ushindi wa Singida.

Wakati huo huo, katika Uwanja wa Sheikh Amri Abeid jijini Arusha, Fountain Gate walikuwa na kibarua kigumu dhidi ya Coastal Union walioanza mchezo kwa kasi wakiandika bao la mapema dakika ya 2 kupitia kwa Shiza Kichuya.

Hata hivyo, Fountain Gate walirudi na kusawazisha kupitia Chukwunonye Obasi dakika ya 14 kabla ya kuongeza la pili dakika ya 33 huku Henry David akifunga bao la tatu dakika ya 70 na kufanya matumaini ya ushindi kuwa makubwa kwa wenyeji.

Coastal Union hawakukata tamaa, wakipata bao la pili dakika za nyongeza (90+3) kupitia Meshack Mwamita, lakini juhudi zao hazikutosha kubadili ubao wa matokeo.

Katika Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Azam FC walikuwa wenyeji wa Namungo katika mchezo uliokuwa wa ushindani mkubwa huku timu zote zikionesha nidhamu ya hali ya juu.

Azam walifanikiwa kupata bao pekee la mchezo dakika ya 41 kwa njia ya penalti iliyofungwa kwa utulivu na Feisal Salum aliandika bao lake la kumi msimu huu lililodumu hadi mwisho na kuwapatia ushindi muhimu.

Kwa ujumla, michezo hiyo imeendelea kuonyesha ushindani mkubwa ndani ya ligi, huku timu zikionyesha nia ya kupambana hadi dakika ya mwisho kusaka alama tatu muhimu.

HAKUNA MBABE WA KARIAKOO MSIMU WA 2025/26.

 

LIGI Kuu ya NBC iliendelea jana kwa mchezo wa ‘Derby’ ya Kariakoo kati ya Simba na Yanga iliyochezwa Mej. Jenerali isamuhyo na kumalizika kwa sare ya kusisimua ya mabao 2-2, katika pambano lililovuta hisia za mashabiki wengi.

Simba walikuwa wa kwanza kupata bao kupitia kwa Libasse Gueye dakika ya tatu kwa pasi safi ya Clatous Chama ambaye dakika saba baadae aliiandikia Simba ‘chuma’ ya pili baada ya kupokea pasi kutoka kwa Elie Mpanzu.

Dakika ya 17 Prince Dube alirudisha matumaini kwa Yanga na kufanya mchezo huo kwenda mapumziko Simba ikiongoza 2-1.

Dakika tano baada ya kipindi cha pili kuanza nahodha wa Yanga Bakari Mwamnyeto alisawazisha na kurejesha matumaini ya wananchi.

Mchezo huo uliendelea kwa kasi kubwa huku kila timu ikitafuta bao la ushindi, lakini uimara wa safu za ulinzi na makipa ulihakikisha matokeo yanabaki kuwa sare ya 2-2.

hii imeendelea kuthibitisha ushindani mkubwa uliopo kwenye Kariakoo Derby huku kila upande ukionyesha ubora na mapambano makali hadi dakika ya mwisho.

Mchezaji wa Simba Claotus Chama alichaguliwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo baada ya kufunga bao moja na kutoa pasi moja ya bao.

CHIRWA KINARA WA MABAO NBC CHAMPIONSHIP. 

 

 

LIGI ya Championship ya NBC msimu wa 2025/26 inaendelea kushika kasi huku vita ya ufungaji ikizidi kupamba moto huku wachezaji mbalimbali wakionyesha uwezo wao wa kutikisa nyavu.

Kinara wa orodha hiyo anaekipiga katika kikosi cha Kagera sugar Obrey Chirwa tayari ameweka kambani mabao 14 na kuwa kileleni mwa wafungaji.

 

Akifuatiwa na Adam Uledi wa Transit Camp ambaye amehamia KMC inayoshiriki Ligi Kuu ya NBC mwenye mabao 11 sawa na Ramadhani Hashimu kutoka timu ya B19 inayopambana vikali kusalia Ligi ya Championship ya NBC.

 

Nafasi ya tatu inashikwa na Boniface Brown wa Mbeya Kwanza mwenye mabao 10 sambamba na Abdereheman Mussa wa Transit Camp na Maulid Shaban kutoka Geita Gold wote wakiwa na idadi hiyo ya mabao.

 

Ushindani huu unaonyesha wazi kuwa msimu huu ni wa ushindani mkubwa ambapo kila mchezaji anapambana kuisaidia timu yake pamoja kuwania kiatu cha ufungaji bora.

SIMBA YAICHAPA NAMUNGO LIGI KUU YA NBC.

LIGI Kuu ya NBC imeendelea kwa mchezo mmoja ambapo Namungo walikuwa wenyeji wakiikaribisha Simba katika mchezo uliochezwa majira ya saa kumi jioni katika uwanja wa Majaliwa mkoani Lindi.

Mchezo huo ulimalizika kwa Simba kupata ushidi wa mabao 3-1 huku wakionyesha ubora wao hasa katika kipindi cha kwanza walipofanikiwa kupata bao la mapema kupitia kwa Libasse Gueye dakika ya 12 kabla ya kuongeza bao la pili kupitia kwa Anicet Oura dakika ya 25.

Namungo walijaribu kurejea mchezoni na kufanikiwa kupata bao lao dakika ya 33 kupitia Haritier Makambo aliyefunga kwa mkwaju wa penati lakini juhudi zao hazikutosha kuizuia timu ya Simba.

Kipindi cha pili Simba waliendelea kuwa hodari kwenye mchezo huo mbele ya mashabiki wao wa mkoa wa Lindi na kuongeza bao la tatu dakika ya 74 kupitia Elie Mpanzu aliyehitimisha ushindi huo Muhimu kwa ‘Mnyama’.

Ushindi huo unaifanya Simba kuwa na alama 42 ikishika nafasi ya pili huku Namungo wakiwa nafasi ya 10 na alama 22.

Katika mchezo huo winga wa Simba Anicet Oura alichaguliwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo.

 

SIMBA, COASTAL ZAGAWA ‘DOZI’ LIGI KUU YA NBC.

LIGI Kuu ya NBC imeendelea kwa michezo iliyochezwa katika mikoa miwili tofauti ambapo Simba ilikuwa ugenini dhidi ya Fountain gate mchezo uliochezwa uwanja wa Sheikh Abeid mkoani Arusha na ‘Mnyama’ kusibuka na ushindi wa mabao 3-0.

Simba walidhibiti mchezo kuanzia mwanzo hadi mwisho wakionyesha ubora mkubwa wa kushambulia na bao la kwanza lilifungwa mwishoni mwa kipindi cha kwanza na Clatous Chama ambaye aliwapa Simba mwanzo mzuri.

Kipindi cha pili kilianza kwa kasi Libase Gueye akiongeza bao la pili dakika ya 53 akitumia vizuri pasi ya Selemani Mwalimu.

Bao la tatu kilifungwa dakika ya 71 kwa mchezaji wa Fountain Gate Shaban Mgunda kujifunga baada ya kushindwa kuokoa krosi iliyopigwa na Elie Mpanzu.

Ushindi huu unaimarisha nafasi ya Simba katika msimamo wa ligi kuu wakiwa nafasi ya Pili na alama 39 huku Fountain Gate wakiendelea kupambana kujinasua katika eneo hatari wakiwa nafasi 14 baada ya kukusanya alama 16.

Mchezo wa Pili Coastal union iliibuka na ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya Dodoma jiji kwenye uwanja wa Mkwakwani, Tanga.

Coastal union ilifungua ukurasa wa mabao dakika ya 15 kupitia kwa Greyson Gwalala kwa shuti kali kabla ya Maabad Maulid kuongeza bao la pili dakika ya 32 na kuwapa wenyeji uongozi mzuri wa 2-0 kipindi cha kwanza.

Kipindi cha pili kilishuhudia ushindani ukiendelea huku Dodoma jiji wakijitahidi kurejea mchezoni na matumaini yalirejea baada ya kupata bao dakika ya 90+1 kupitia kwa Waziri Junior ambalo lilidumu kwa dakika tatu pekee kabla ya Geofrey Manyac kuzima matumaini ya Dodoma kusawazisha bao kwa kuandika la tatu kwa Coastal.

Ushindi huo unaifanya Coastal union kufikisha alama 19 wakikwea hadi nafasi ya 12 huku Dodoma wakisalia na alama 24 kwenye nafasi ya nane.