Author: Cynthia Michael

HAKUNA MBABE KMC COMPLEX LIGI KUU YA NBC.

 

LIGI Kuu ya NBC imeendelea kwa mchezo uliochezwa uwanja wa KMC majira ya saa Moja jioni Mkoani Dar es Salam uliozikutanisha KMC dhidi ya Tanzania Prisons na kumalizika
kwa Sare ya bao 1-1.

Kipindi cha kwanza kilianza kwa kasi huku Tanzania Prisons wakitangulia kupata bao la mapema dakika ya tano kupitia kwa Jeremiah Juma.

Hata hivyo KMC walirejea mchezoni dakika ya 38 baada ya Adam Uledi kusawazisha kwa shuti lililowapa matumaini mashabiki wao.

Kipindi cha Pili kilikuwa na ushindani mkali kutoka pande zote mbili,kila timu ikitafuta bao la ushindi lakini safu za ulinzi zilisimama imara kuzuia mashambulizi ya timu pinzani.

Matokeo haya yanaacha hali ngumu kwa timu zote mbili katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC, KMC ikiongeza alama moja muhimu lakini bado haitoshi kuwatoa kwenye presha ya kushuka daraja wakiwa nafasi ya 16 na alama tisa huku wakihitaji ushindi katika michezo ijayo ili kujiweka salama.

Tanzania Prinsons nao wapo kwenye nafasi mbaya kwenye nafasi ya 15 baada ya kukusanya alama 14 katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC.

Kwa matokeo hayo hakuna timu ambayo ipo salama na vita ya kuepuka kushuka daraja inaendelea kuwa kali kadri msimu unavyoelekea ukingoni huku michezo iliyosalia ikiwa na umuhimu mkubwa kwa timu hizo.

VITA YA MABAO YA NJE YA BOKSI INAVYOKWENDA LIGI KUU YA NBC.

 

MSIMU wa Ligi Kuu ya NBC unaendelea huku ushindani wa mabao ya nje ya boksi ukishika kasi na wachezaji wakionyesha uwezo mkubwa wa kupiga mashuti ya mbali na kufunga mabao ya kuvutia.

Kinara wa orodha hiyo ni Ismail Mhesa kutoka Mtibwa Sugar akiwa amefunga mabao matatu nje ya boksi na kuonyesha ubora mkubwa wa kupiga mbali na kuwa tegemeo kwa timu yake akifunga mabao hayo walipokutana na timu za Prisons, Young Africans na TRA.

Sambamba naye ni Iddi Selemani wa Azam ambaye pia ana mabao 3 huku akiendelea kuwa na mchango mkubwa kwa timu yake ya Azam akitumia ubunifu na uwezo wa kufunga akiwa nje ya eneo la hatari na akifanya hivyo mara mbili alipokutana na KMC huku bao moja akiwafunga TRA.

Nafasi ya tatu inashikiliwa na Ibrahim Imoro anayekipiga Singida Black Stars akiwa na mabao matatu ambayo aliyapata walipokutana dhidi ya Prison na Mbeya City huku akinyesha uthabiti mkubwa katika mashuti ya mbali na kuongeza nguvu safu ya ushambuliaji ya timu yake ingawa yeye ni mlinzi.

Wakati huo huo Libase Gueye wa Simba SC ana mabao mawili ya nje boksi akionyesha ubora wake wa kushambulia kwa kutumia nafasi chache anazopata na mabao hayo akiyapata dhidi ya Mashujaa na KMC.

Orodha hiyo inakamilishwa na Kelvin Nashon kutoka KMC mwenye mabao mawili aliyofunga walipokutana na Mbeya City na Singida black star na kumfanya kiungo huyo raia wa Tanzania kuwa tishio kwa timu pinzani.

Kwa ujumla wachezaji wa Ligi Kuu wanazidi kuboresha uwezo wa kufunga mabao ya mbali jambo linaloongeza burudani na ushindani mkubwa ndani ya Ligi.

SINGIDA YATAMBA UGENINI, DAR ‘DERBY’ HAKUNA MBABE LIGI KUU YA NBC.

 

LIGI Kuu ya NBC imeendelea kwa timu ya Singida Black Stars kupata ushindi mnono wa mabao 4–1 dhidi ya Mbeya City ugenini katika mchezo uliochezwa mkoani Manyara kwenye uwanja wa Tanzanite Kwaraa, Manyara.

Mbeya City ilianza vizuri mchezo na kupata bao la kuongoza dakika ya 14 kupitia kwa mshambuliaji Vitalis Mayanga.

Hata hivyo, Singida Black Stars walirudi kwa nguvu na kusawazisha dakika ya 31 kupitia kwa Emmanuel Keyeh kupitia mkwaju wa penati na kufanya timu hizo kwenda mapumziko zikiwa sare.

Kipindi cha pili kilikuwa cha Singida Black Stars ambapo iliongeza kasi ya mashambulizi na dakika ya 69 Mosi Ndumumwe aliifungia timu yake bao la pili kabla ya beki Ibrahim Imoro kufunga mabao mawili mfululizo dakika ya 72 na 86 na kuhitimisha karamu hiyo ya mabao kwa Singida.

Ushindi huo unaifanya Singida Black Stars kuendelea kujiweka kwenye hali nzuri katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC huku Mbeya City wakilazimika kujipanga upya kwa ajili ya michezo ijayo.

Mchezo mwingine ulipigwa saa 2 :30 usiku katika uwanja wa Benjamin william Mkapa ambapo mabigwa watetezi Young africans waligawana alama na Azam baada ya kutoka sare katika mchezo uliokuwa na ushindani mkubwa na kasi kutoka kwa timu zote mbili

Katika mchezo huo kiungo mahiri wa Azam Feisal Salum aliibuka kuwa mchezaji bora wa mchezo huo kufuatia kiwango chake kizuri alichokionyesha uwanjani.

SINGIDA YATAKATA, PAMBA IKIBANWA NYUMBANI LIGI KUU YA NBC.

 

LIGI Kuu ya NBC imeendeleza burudani ya aina yake huku mashabiki wakishuhudia ushindi mwembamba wa bao moja kwa Singida Black Stars dhidi ya Coastal na sare ya kusisimua ya mabao 2-2 kwa Pamba Jiji dhidi ya Azam FC.

Katika mchezo uliopigwa kwenye uwanja wa airtel mkoani singida, Singida Black Stars waliikaribisha Coastal union na iliibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Coastal Union huku shujaa wa mchezo huo akiwa mshambuliaji Joseph Guede aliyefunga bao pekee dakika ya 72 kwa umakini mkubwa akimalizia shambulizi lililowapa furaha mashabiki wa Singida.

Coastal walijitahidi kusaka bao la kusawazisha lakini uimara wa safu ya ulinzi ya Singida ulihakikisha wanatoka bila alama wala bao.

Wakati huo huo jijini Mwanza kwenye Uwanja wa CCM Kirumba saa kumi kamili jioni kulishuhudiwa pambano kali kati ya Pamba Jiji FC na Azam lililomalizika kwa sare ya mabao 2-2.

Pamba Jiji walianza kuonyesha makali kwa bao la Himid Mao aliyejifunga dakika ya 45 kabla ya John Nakibinge kuongeza la pili dakika ya 48.

Hata hivyo Azam hawakukata tamaa wakarejea kwa nguvu kupitia Jean Ngita dakika ya 56 na baadaye Feisal Salum kufunga kwa penalti dakika ya 59 na kuifanya mechi kuwa ya kusisimua hadi dakika ya mwisho.

Mchezo huo ulishuhudia Feisal akionyeshwa kadi nyekundu baada ya kumchezea mchezaji wa Pamba rafu mbaya na hivyo feisal kukosa mchezo unaofuata wa Dar es Salaam derby utakaoikutanisha Azam dhidi ya Young Africans.

Kwa matokeo hayo, Singida Black Stars wanaondoka na alama tatu muhimu, huku Azam na Pamba Jiji wakigawana alama mojamoja.

COASTAL, PAMBA ZATAMBA LIGI KUU YA NBC.

 

TIMU ya Coastal Union imeonyesha ubabe ugenini katika Uwanja wa Sokoine mkoani Mbeya baada ya kuichapa Tanzania Prisons mabao 4-1. 

Mchezo ulianza kwa kasi Coastal Union wakipata bao la mapema zaidi kwenye Ligi Kuu ya NBC msimu huu lililofungwa sekunde ya 58 kupitia kwa Bakari Msimu na dakika tatu kabla ya mchezo kwenda mapumziko Shiza Kichuya aliongeza jingine kwa kichwa akipokea pasi safi kutoka kwa Bakari Msimu. 

Tanzania Prisons haikukata tamaa na kuendelea kushambulia jitihada zilizozaa matunda dakika ya 45+2 kupitia kwa George Mpole aliyewafungia bao lililowapa matumaini kabla ya mapumziko.

Dakika ya 51 Bakari Msimu aliongeza bao lake la pili katika mchezo huo na kuifanya Coatal kuongoza 3-1 kabla ya Cleophace Mkandala kuhitimisha karamu ya mabao kwa kufunga dakika ya 90+5 na kuhitimisha ushindi mnono wa mabao 4-1.

Mchezo mwingine uliochezwa kwenye Uwanja wa CCM Kirumba mkoani Mwanza na Pamba Jiji kuibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Namungo.

Bao pekee la mchezo huo lilifungwa dakika ya 55 kupitia kwa Mathew Tegisi lililodumu hadi mwisho wa dakika 90 na kuwapa Pamba Jiji alama tatu muhimu.