Author: Cynthia Michael

LIGI KUU YA NBC YAENDELEA KUTIMUA ‘VUMBI’.

Ligi Kuu ya NBC imeendelea kutoa ushindani mkubwa huku timu mbalimbali zikipigania nafasi za juu na kujinusuru kwenye maeneo ya hatari na kumalizia msimu huu.

 

Mkoani Morogoro, Mtibwa Sugar iliwakaribisha JKT katika dimba la Jamhuri mkoani Morogoro na mchezo huo kumalizika kwa sare ya mabao 2-2.

 

Mtibwa ilipata mabao yake kupitia Haroun Lwawatwa na Magata Fredrick huku JKT Tanzania ikiandika yake kupitia kwa Paul Peter aliyefunga yote mawili.

 

Mkoani Arusha uwanja wa Sheikh Amri Abeid TRA iliwakaribisha Fountain gate na kupoteza kwa mabao 2-1.

 

TRA ilikuwa ya kwanza kuandika bao kupitia kwa John Lazarus dakika ya 35 lakini dakika ya 44 Ismail Aziz aliwapatia bao la kusawazisha Fountain Gate na kuongeza lingine dakika moja kabla ya mapumziko lililohakikisha alama tatu muhimu kwa Fountain.

 

Kwa upande mwingine katika uwanja wa KMC jijini Dar es salaam Simba iliendelea kusalia kwenye mbio za ubingwa baada ya kuifunga Dodoma Jiji kwa bao 1-0 lililofungwa na Elie Mpanzu dakika ya 62.

 

Coastal Union ilikutana na Mashujaa kwenye uwanja wa Mkwakwani mkoani Tanga na kupata ushindi mwembamba wa bao 1-0 kupitia bao la Maabad Maabad dakika ya 65.

 

Matokeo haya yanaendelea kufanya msimamo wa Ligi Kuu ya NBC kuwa wa ushindani zaidi huku Simba ikishikilia usukani kwenye msimamo na timu za katikati pamoja na za chini zikisaka alama muhimu kuelekea mwisho wa msimu.

LIGI KUU YA NBC YAZIDI KUSHIKA KASI.

LIGI Kuu ya NBC imeendelea kwa michezo mitatu iliyotoa ushindani mkubwa huku Simba pekee ikifanikiwa kuondoka na alama tatu muhimu na michezo mingine kutamatika kwa sare. 

 

Katika Uwanja wa Mej. Jen Isamuhyo, Dar es Salaam, mchezo wa mapema ulikuwa kati ya JKT Tanzania na Fountain Gate uliomalizika kwa sare ya mabao 2-2 kwenye mchezo uliokuwa wa kukata na shoka.

 

Fountain Gate walionyesha makali mapema baada ya Juma Abushiri kufungua ukurasa wa mabao dakika ya 3 kabla ya Ismail Kader kuongeza la pili dakika ya 45 na kuwapa wageni uongozi wa mabao mawili kipindi cha kwanza. 

 

Kipindi cha pili JKT Tanzania walirudi kwa nguvu ambapo Salehe Karabaka alipunguza pengo dakika ya 54 kabla ya Paul Peter kuisawazishia timu hiyo dakika ya 86 kwa moja ya bao ‘kali’ la msimu huu na kufanya mchezo kumalizika kwa sare ya mabao 2-2. 

 

Mkoani Tanga katika Uwanja wa Mkwakwani, Simba iliondoka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Coastal Union.

 

Coastal Union walikuwa wa kwanza kupata bao kupitia Maabad Maulid dakika ya 8, lakini Simba waligeuza matokeo kupitia Libase Gueye dakika ya 37 kabla ya Anicet Oura kufunga bao la ushindi dakika ya 44 na kuipa Simba alama tatu muhimu ugenini.

 

Mkoani Lindi katika mchezo wa saa tatu usiku, Namungo na Mbeya City waligawana alama baada ya sare ya bao 1-1.

 

Namungo walitangulia kupitia Hassan Kabunda dakika ya 6 huku Mbeya City wakisawazisha kupitia Eliud Ambokile dakika ya 28.

 

Matokeo hayo yanaendelea kuongeza ushindani katika hatua za mwisho za msimu wa Ligi Kuu ya NBC na kufanya kila mchezo kuwa mgumu na wenye ushindani mkali.

ISAMUHYO, MKWAKWANI, MAJALIWA ‘KUWAKA MOTO’ LIGI KUU YA NBC.

Ligi Kuu ya NBC inaendelea kwa michezo mitatu muhimu ambayo inaweza kubadilisha nafasi za timu kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC.

 

Mchezo wa kwanza utaanza saa 10:00 alasiri katika Uwanja wa Mej. Jen. Isamuhyo ambapo JKT Tanzania watakuwa wenyeji wa Fountain Gate.

 

JKT Tanzania wanaingia kwenye mchezo huu wakiwa nafasi ya 6 kwenye msimamo huku Fountain Gate ikiwa nafasi ya 11, alama tatu zina umuhimu mkubwa kwa pande zote mbili huku JKT wakisaka kusogea juu zaidi na Fountain Gate kujinasua kwenye eneo la chini. 

 

Saa 12:30 jioni, macho yatahamia Uwanja wa Mkwakwani mkoani Tanga ambapo Coastal Union wataikaribisha Simba katika mchezo mwingine wa ushindani mkubwa.

 

Simba wanaingia wakiwa nafasi ya 2 kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC wakisaka kuendelea kupunguza tofauti ya alama kileleni, huku Coastal Union wakiwa nafasi ya 12 wakihitaji matokeo mazuri kujiweka salama zaidi. 

 

Mchezo wa mwisho leo utachezwa saa 3:00 usiku katika Uwanja wa Majaliwa mkoani Lindi ambapo Namungo watacheza dhidi ya Mbeya City ambayo haijapata matokeo ya kufurahisha hivi karibuni.

 

Mbeya city wakiwa katika nafasi ya 14 kwenye ya msimamo na Namungo wakiwa nafasi ya 13 wakisaka alama muhimu mbele ya mashabiki wao wa nyumbani ili kuboresha nafasi zao kuelekea mwisho wa msimu. 

 

Michezo ya leo ina uzito mkubwa kwa timu zinazowania nafasi za juu pamoja na zile zinazopambana kujinasua kwenye maeneo ya chini ya msimamo wa Ligi Kuu ya NBC.

CLATOUS CHAMA NA REKODI MPYA LIGI KUU YA NBC.

 

‘STAA’ wa Simba, Clatous Chama ameendelea kuandika historia ndani ya LIGI KUU NBC baada ya kuwa mchezaji wa kwanza kushinda tuzo ya Mchezaji bora wa mchezo(Man of the Match) mara nne mfululizo katika msimu wa 2025/2026.

Kiungo huyo raia wa Zambia ameonyesha kiwango cha juu katika mechi za hivi karibuni, akiongoza safu ya ushambuliaji ya Simba kwa pasi za mwisho, mabao muhimu na uwezo wake wa kutawala mchezo katikati ya uwanja.

Chama alianza mfululizo huo kwenye Kariakoo Derby kati ya Young Africans na Simba iliyomalizika kwa sare ya mabao 2-2, ambapo alionyesha kiwango bora na kuwa mhimili mkubwa wa Simba katika mchezo huo mkubwa wa watani wa jadi.

Baada ya derby hiyo, aliendelea kung’ara katika ushindi wa mabao 4-0 dhidi ya Tanzania Prisons, kabla ya kuiongoza Simba kushinda 1-0 dhidi ya JKT Tanzania na alikuwa nyota katika ushindi mwingine wa mabao 3-0 dhidi ya Mashujaa FC.

Katika mechi zote nne, Chama aliondoka na tuzo ya Mchezaji Bora wa Mechi, jambo lililoonyesha ubora wake wa kipekee na mchango mkubwa ndani ya kikosi cha Simba msimu huu.

Ubora wa Chama umeendelea kuwa silaha muhimu kwa Simba katika mbio za ushindi, huku mashabiki wakizidi kuvutiwa na mchango wake kila anapoingia uwanjani.

Uchezaji wake wa kujiamini, uzoefu na uwezo vimemfanya kuwa mmoja wa nyota wanaong’ara zaidi kwenye Ligi Kuu ya NBC msimu huu.

LIGI KUU YA NBC KUPAMBA MOTO LEO.

 

LIGI Kuu ya NBC itaendelea leo kwa michezo minne muhimu itakayochezwa ikiwa ni muendelezo wa mzunguko wa 23 katika viwanja tofauti huku kila timu ikisaka alama muhimu kuelekea mwisho wa msimu.

Timu za juu zinapigania ubingwa huku zile za chini zikihangaika kujinasua kwenye hatari ya kushuka daraja na kucheza Ligi ya Championship ya NBC.

Mchezo wa kwanza utawakutanisha Mtibwa Sugar dhidi ya KMC katika uwanja wa Jamhuri Mkoani Morogoro Majira ya saa nane mchana ambapo Mtibwa Sugar wanaingia wakiwa nafasi ya 11 kwenye msimamo huku KMC wakiwa nafasi ya mwisho.

Katika mchezo mwingine Tanzania Prisons watawakaribisha Fountai Gate kwenye uwanja wa Sokoine Mkoani Mbeya majira ya saa nane mchana katika pambano litakalokuwa na ushindani mkubwa.

Tanzania Prisons wanashika nafasi ya 15 huku Fountain Gate wakiwa nafasi ya 10 na alama 25 wakisaka kuendelea kubaki kwenye nafasi za juu za msimamo ili kuepuka kushuka daraja.

Mashujaa watakuwa na kazi ngumu dhidi ya timu ya Simba inayosaka taji la Ligi Kuu ya NBC baada ya misimu minne huku Mashujaa ikiwa nafasi ya tisa kwenye msimamo ikipambana kujihakikishia nafasi ya kushiriki Ligi Kuu ya NBC msimu ujao.

Mchezo huo utachezwa Uwanja wa Lake Tanganyika Mkoani Kigoma majira ya saa 10 :15 jioni na unatarajiwa kuwa na ushindani mkubwa kutokana na ubora wa timu zote mbili msimu huu.

Katika mchezo mwingine wa kusisimua Azam FC watachuana na Pamba Jiji Katika uwanja wa Azam complex jijini Dar es salaam majira ya saa 12:30 jioni.

Azam wanaingia wakiwa nafasi ya tatu kwenye msimamo huku Pamba Jiji wakiwa nafasi ya saba, kila mmoja akihitaji ushindi ili kutimiza malengo yake msimu huu.