Author: Loveness Bernard

STAND UNITED, FOUNTAIN GATE NI VITA YA KUCHEZA LIGI KUU YA NBC.

 

HATUA ya mtoano wa nani kusalia ama kupanda Ligi Kuu ya NBC inaendelea kesho kwa mchezo mmoja kati ya Stand United ya mkoani Shinyanga itakayokuwa mwenyeji wa timu ya Fountain Gate kwenye uwanja wa Kambarage mkoani Shinyanga.

Mchezo huo utakaopigwa saa kumi alasiri utakuwa muhimu kwa timu zote ili kujihakikishia kucheza kwenye ligi namba nne kwa ubora barani Afrika.

Stand United ambao msimu wa 2024/2025 imecheza Ligi ya championship ya NBC inapaswa kupata ushindi wa matokeo ya jumla ya michezo ya nyumbani na ugenini ili kupanda Daraja huku timu ya Fountain Gate nayo ikipaswa kufanya hivyo ili kuhakikisha inabaki Ligi Kuu ya NBC msimu ujao.

Stand imepata nafasi ya kucheza hatua ya mtoano baada ya kuitoa timu ya Geita Gold kwa matokeo ya jumla huku Fountain ikicheza baada ya kupoteza kwenye matokeo ya jumla dhidi ya Tanzania Prisons.

Tatu Malogo kutoka Tanga ndiye mwamuzi atakaesimamia mchezo huo wa kwanza akisaidiwa na Hamdan Said kutoka Mtwara, Zawadi Yusuph kutoka Dar es Salaam na Shija Shurugwai kutoka mkoani Shinyanga.

PRISONS UHAKIKA LIGI KUU NBC 2025/26.

TIMU ya Tanzania Prisons imefanikiwa kusalia Ligi Kuu ya NBC baada ya kuifunga timu ya Fountain Gate 3-1 katika mchezo uliochezwa uwanja wa Sokoine mkoani Mbeya.

Ilimchukua dakika saba mchezaji wa Tanzania Prisons,Beno Ngasa kufungua ukurasa wa mabao huku mchezaji wa Fountain Gate Laurian Makame akisawazisha dakika ya 27 kabla ya Ezekiel Mwashilindi kuiongezea Prisons bao dakika ya 45 hivyo maafande hao Kwenda mapumziko wakiongoza 2-1.

Kipindi cha pili kilianza kwa kasi ambapo dakika ya 47 ya mchezo huo mchezaji wa Prisons Oscar Mwajanga aliongeza bao la tatu kwa timu hiyo na matokeo yakisalia hivyo mpaka mwisho wa mchezo .

Tanzania Prisons wamesalia Ligi Kuu ya NBC kwa uwiano wa mabao 4-2 katika michezo yote miwili ambayo timu hiyo na Fountain Gate zimecheza.

NI VITA YA NANI KUBAKI LIGI KUU YA NBC SOKOINE LEO.

MCHEZO wa pili wa hatua ya mtoano kati ya Tanzania Prisons dhidi ya Fountain Gate unatarajiwa kupigwa leo kwenye uwanja wa Sokoine, Mbeya kutafuta timu itakayosalia kwenye Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2025/2026.

Huu ni mchezo wa mwisho kwa timu zinazoshiriki Ligi Kuu ya NBC kukutana msimu huu baada ya kumaliza kwenye nafasi ya 13 na 14 ya msimamo zikiwa nafasi za kucheza michezo ya mtoano.

Mchezo huo wa mkondo wa pili utachezwa leo majira ya saa 10:00 alasiri ambapo mchezo wa kwanza uliochezwa uwanja wa Tanzanite Kwaraa mkoani Manyara ulimalizika kwa sare ya 1-1.

Mshindi wa mchezo wa leo atakuwa amekata tiketi ya kusalia katika Ligi Kuu ya NBC huku atakayeshindwa atacheza mchezo wa mtoano dhidi ya timu ya Stand United inayoshiriki Ligi ya Championship ya NBC.

YOUNG AFRICANS MABINGWA LIGI KUU YA NBC 2024/2025

PAZIA la Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2024/2025 limefungwa rasmi jana katika mchezo wa dabi ya Kariakoo ambapo timu ya Young Africans iliibuka na ushindi.

Katika mchezo ulichezwa majira ya saa kumi na moja jioni uwanja wa Benjamin Mkapa timu ya Yanga iliifunga timu ya Simba mabao 2-0 yaliyofungwa na wachezaji Pacome Zouzoa na Clement Mzize kipindi cha pili cha mchezo huo.

Mara baada ya mchezo huo Young Africa ilikabidhiwa kombe la ubingwa wa Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2024/2025 na kuweka historia ya kulibeba kombe hilo mara 31 huku timu hiyo ikikusanya alama 82 na mtani wao Simba akibaki nafasi ya pili na alama 78.

timu zote zimekata tiketi kushiriki Ligi ya mabingwa barani Afrika (CAF Champions League) kwa msimu wa 2025/2025 huku Azam na Singida Black Stars wakishiriki Kombe la Shirikisho(CAF Confederation Cup)

‘PILATO’ WA DABI YA KARIAKOO HUYU HAPA.

RAIA wa Misri Amin Mohamed Amin ndiye atakayechezesha mchezo wa Young Africans dhidi ya Simba maarufu kama ‘Kariakoo Dabi’ Juni 25 kwenye uwanja wa Mkapa, Dar es Salaam.

Ikiwa Yanga itashinda mchezo huo au kutoa sare ya aina yoyote itaibuka mshindi wa kombe la ubingwa wa Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2024/2025 na ikiwa Simba itafanikiwa kushinda itaibuka mabingwa wapya wa kombe hilo.

Amin atasaidiwa na Mahmoud El Regal,Samir Gamal Mohamed na Ahmed Mahrous Elghandour wote kutoka nchini Misri huku mtathimini waamuzi akiwa ni Alli Mohamed kutoka nchini Somalia.

Hii ni mara ya kwanza kwa mchezo wa Ligi Kuu ya NBC kusimamiwa na waamuzi wa mchezo kutoka nje ya Tanzania.

Mchezo huo ambao mwenyeji ni timu ya Young Africans yenye alama 79 huku ikiwa kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu ya NBC dhidi ya Simba yenye alama 78 ikishika nafasi ya pili utapigwa saa kumi na moja jioni.