Author: Loveness Bernard

LIGI KUU NBC ‘KUCHANJA MBUGA’ VIWANJA VITATU,CHAMPIONSHIP MAMBO YAZIDI KUWA MOTO.

MZUNGUKO wa 24 wa Ligi Kuu ya NBC utaendelea kushika kasi  ambapo michezo mitatu itachezwa katika mikoa ya Kagera,Dar es Salaam na Mbeya hivyo kufanya mbio za ubingwa kuzidi kufikia mahali patamu zaidi kwani mmoja anapambana angalau apate alama  ili aweze kubeba ubingwa ama aendelee kubaki msimu ujao .

JKT Tanzania ambayo ipo nafasi ya sita kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC itakuwa mwenyeji wa Dodoma Jiji  iliyopo nafasi ya nane katika uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo  uliopo Mbweni Dar es Salaam majira ya saa kumi jioni.

KenGold iliyopo nafasi ya 16   katika msimamo wa Ligi Kuu  ya NBC itakawakaribisha timu ya Azam katika uwanja wa Sokoine mkoani Mbeya majira ya saa kumi jioni huku Kagera Sugar atakuwa mwenyeji wa Coastal Union katika uwanja wa Kaitaba mkoani Kagera majira ya saa moja usiku.

Kwa upande wa Ligi ya Championship ya NBC timu ya Songea United itaikaribisha timu Biashara United katika uwanja wa Majimaji mkoani Ruvuma majira ya saa kumi jionI ikiwa ni mzunguko wa 25 wa Ligi hiyo.

Ratiba ya Ligi Kuu ya NBC 2025/2026

LIGI KUU YA NBC KUWAKA VIWANJA VINNE LEO

LADHA za Ligi namba nne kwa ubora barani Afrika zinarejea rasmi leo kwa michezo minne itakayopigwa kwenye viwanja tofauti nchini ikiwa ni baada ya mapumziko ya michuano ya kufuzu Kombe la Dunia 2026.

Mchezo wa kwanza utakuwa jijini Mwanza ambapo timu ya Pamba Jiji itakuwa mwenyeji wa timu ya Namungo katika uwanja wa CCM Kirumba majira ya saa nane mchana.

KMC itacheza dhidi ya timu ya Tanzania Prisons katika uwanja wa KMC Complex uliopo mkoani Dar es Salaam huku Tabora United itakuwa mwenyeji wa Young Africans katika uwanja wa Ali Hassan Mwinyi mkoani Tabora na mchezo wa mwisho utakuwa kati ya Fountain Gate itakayoialika Singida Black Stars katika uwanja wa Tanzanite Kwaraa mkoani Manyara huku michezo yote mitatu ikichezwa saa 10:15 alasiri.

HAWA HAPA WABABE WA UWANJA WA NYUMBANI LIGI YA CHAMPIONSHIP YA NBC.

LIGI ya Championship ya NBC inazidi kushika kasi ikiwa ni mzunguko wa 24 huku timu nyingi zikionyesha uwezo ambapo kila timu inataka kufuzu kwenda Ligi Kuu ya NBC msimu 2025-26 huku  timu za Mtibwa Sugar, Mbeya City, Geita Gold, Mbeya Kwanza na Songea United zikiwa hazijapoteza mchezo wowote nyumbani hadi sasa.

Mtibwa Sugar ipo nafasi ya kwanza kwenye msimamo ikiwa na alama 57 ikicheza michezo 12 kwenye uwanja wake wa Manungu Complex na kufanikiwa kushinda michezo yote.

Mbeya City iko nafasi ya pili kwenye msimamo wa Ligi ya Championship ikishinda michezo tisa na kupata sare tatu katika michezo 12 waliyocheza uwanja wao wa nyumbani.

Geita Gold ipo nafasi ya nne katika  msimamo ikishinda michezo 11 na kupata sare mchezo mmoja katika michezo 12 iliyocheza ikiwa uwanja wao wa Nyankumbu.

Mbeya Kwanza ipo nafasi ya sita katika msimamo ikicheza michezo 11 nyumbani ikishinda michezo saba na kupata sare michezo minne.

Songea United  ipo nafasi ya nane katika msimamo ikicheza michezo 10 nyumbani na kushinda michezo sita huku ikipata sare michezo minne na kukamilisha idadi ya timu ambazo hadi sasa hazijapoteza mchezo wowote nyumbani.

LADHA ZA LIGI KUU YA NBC KUREJEA APRIL MOSI

LIGI Kuu ya NBC inatarajia kurejea mapema mwezi ujao baada ya mapumziko ya takribani wiki mbili  kupisha michezo ya kufuzu Fainali za Kombe la Dunia 2026.

Kurejea kwa Ligi Kuu ya NBC ni mwanzo wa mzunguko wa  24  huku ikibaki mizunguko takribani sita ligi hiyo kutamatika.

April mosi Tabora United  itawakaribisha ‘watoto wa Jangwani’ Young Africans kwenye uwanja wa Ali Hassan Mwinyi  mkoani Tabora mchezo utakaochezwa majira ya saa kumi alasiri.

April mbili itapigwa michezo mitatu Pamba Jiji itaikaribisha Namungo majira ya saa 8:00 mchana katika  uwanja wa CCM Kirumba huku KMC ikiwaalika Tanzania Prisons kwenye uwanja wa KMC Complex mkoani Dar es Salaam majira ya saa 10:15 na mchezo wa mwisho utapigwa Tanzanite Kwaraa kati ya Fountain Gate itakayoikaribisha Singida Black Stars saa 10:15 alasiri.

April tatu itaanzia katika uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo JKT Tanzania ikiwakaribisha Dodoma Jiji, Ken Gold ikiwaalika Azam katika uwanja wa Sokoine michezo yote ikichezwa saa 10:00 alasiri huku Kagera Sugar ikiwaalika Coastal Union katika uwanja wa Kaitaba majira ya saa 1:00 usiku.

Mchezo wa Simba na Mashujaa utachezwa Mei mbili kutokana na timu ya Simba kukabiliwa na michuano ya Kombe la Shirikisho barani Afrika ambayo kwa sasa ipo katika batua ya robo fainali.

AHOUA ‘HACHEKI NA WOWOTE’ LIGI KUU NBC.

JEAN Ahoua wa timu ya Simba ameendelea kuwa na msimu bora wa Ligi Kuu ya NBC hadi sasa baada ya kuhusika kwenye mabao 19 huku timu yake ikisalia na michezo nane kutamatisha msimu.

Ahoua aliyesajiliwa na Simba akitokea Asec Mimosa mpaka sasa amehusika katika mabao 19  baada ya kufanikiwa  kufunga mabao 12 kutoa pasi zilizozaa mabao saba hivyo kufanya kuwa mchezaji aliyehusika katika mabao mengi kuliko mchezaji yeyote.

Prince Dube  ambaye amesajiliwa  na timu ya Young Africans akitokea Azam  anashikilia nafasi ya pili akiwa amehusika katika mabao 17 baada ya kufunga mabao 10 na kutoa pasi za mabao saba.

Mpinzani wa karibu wa Dube ni Feisal Salum wa Azam akiwa amefanikiwa kutoa pasi za mwisho 12 na kufunga mabao manne  hivyo kuhusika katika mabao 16.

Kwa upande wake Aziz Ki wa Young Africans amefanikiwa kufunga mabao saba na kutoa pasi za mabao saba hivyo kuhusika katika mabao 14.

Pacome Zouzoua na Clement Mzize wa Young Africans wote wamehusika katika mabao 13 kila mmoja  huku Pacome akifunga mabao saba na kutoa pasi za mwisho sita huku Mzize akifunga mabao 10 na kutoa pasi za mwisho tatu.