Author: Loveness Bernard

DODOMA JIJI KUMALIZA ‘KIPORO’ CHA LADHA ZA LIGI KUU YA NBC KESHO.

LIGI Kuu ya NBC inatarajiwa kuendelea kesho kwa mchezo namba 148 ambapo timu ya Simba itaikaribisha timu  ya Dodoma jiji katika uwanja wa KMC Complex mkoani Dar es Salaam majira ya saa kumi jioni.

Simba ipo nafasi ya pili katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC ikiwa  na alama 54 ikifunga mabao 46 na kuruhusu mabao 8 katika michezo 22 timu hiyo iliyocheza mpaka sasa.

Dodoma Jiji iko nafasi ya nane  kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya  NBC  huku ikiwa na alama 27 ikifunga mabao 22 na kuruhusu 27 katika michezo 22 iliyocheza mpaka sasa.

Mechi hiyo ya Simba na Dodoma Jiji iliahirishwa kutokana na ajali iliyopata timu ya Dodoma Jiji ikitokea Ruangwa mkoani Lindi  kwenye mchezo wa Ligi Kuu ya NBC dhidi ya  timu ya Namungo

 

 

KYARUZI,SIMCHIMBA WANG’ARA TUZO ZA NBC CHAMPIONSHIP

BEKI wa Mtibwa Sugar  Erick Kyaruzi amechaguliwa kuwa Mchezaji Bora wa Mwezi Januari wa Ligi ya NBC Championship 2024/25, huku Awadh Juma wa Mtibwa Sugar akichaguliwa Kocha Bora wa mwezi huo.

Kyaruzi aliyeingia fainali katika mchakato huo na Raizin Hafidh wa Mtibwa Sugar na Boniface Maganga wa Mbeya Kwanza, alionesha kiwango chenye mwendelezo katika safu ya ulinzi, huku pia akisaidia timu yake kwa kufunga mabao mawili katika dakika 270 za michezo mitatu aliyotumika.

Kwa upande wa Awadh aliyeingia fainali na Zuberi Katwila wa Bigman na Emmanuel Massawe wa Mbeya Kwanza, aliiongoza timu yake kupata ushindi katika michezo yote mitatu iliyocheza ikivuna pointi tisa na kuendelea kuongoza ligi hiyo.

Pia kamati imemchagua Andrew Simchimba wa Geita Gold kuwa Mchezaji Bora wa Mwezi Februari wa Ligi ya NBC Championship 2024/25, huku Mohamed Muya pia wa Geita Gold akichaguliwa Kocha Bora wa mwezi huo.

Simchimba aliyeingia fainali katika mchakato huo na Oscar Tarimo wa Mbeya Kwanza na Mwisho Yangson wa Polisi Tanzania alionesha kiwango chenye mwendelezo ikiwa ni pamoja na kufunga mabao manne katika michezo mitatu kwa dakika 253 alizocheza.

Kwa upande wa Muya aliyeingia fainali na Zuberi Katwila wa Bigman na Juma Hussein wa Stand United, aliiongoza timu yake kushinda michezo minne kati ya mitano iliyocheza mwezi huo.

DUBE MCHEZAJI BORA FEBRUARI LIGI KUU YA NBC

MSHAMBULIAJI wa timu ya Young Africans (Yanga) ya Dar es Salaam, Prince Dube, amechaguliwa kuwa Mchezaji Bora wa mwezi Februari wa Ligi Kuu ya NBC msimu wa mwaka 2024/25, huku Miloud Hamdi pia wa Yanga akichaguliwa Kocha Bora wa ligi hiyo kwa mwezi huo.

Dube alionesha kiwango kizuri chenye mwendelezo akiwashinda Aziz Ki wa Yanga na Selemani Bwenzi wa KenGold, alioingia nao fainali katika mchakato wa Tuzo za Mwezi uliofanywa na Kamati ya Tuzo za Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF).

Mchezaji huyo alitoa mchango mkubwa kwa timu yake katika michezo saba ambayo Yanga ilicheza mwezi huo na kufunga mabao matano na kuhusika na mengine matano kwa dakika 562 alizocheza. Yanga ilishinda michezo sita na kutoka sare mmoja.

Kwa upande wa Hamdi aliyeingia fainali katika mchakato huo na Fadlu Davids wa Simba na Fred Minziro wa Pamba Jiji, aliiongoza Yanga kushinda michezo minne na sare moja, ambapo kwa mwezi huo Yanga ilicheza michezo saba.

Hamdi aliiongoza Yanga ilipotoka suluhu na JKT Tanzania, kisha ikazifunga KMC mabao 1-6, Singida Black Stars (2-1), Mashujaa (0-5) na Pamba Jiji (0-3). Mechi nyingine ambazo Yanga ilishinda mwezi huo lakini haikuwa chini ya Hamdi ni dhidi ya KenGold (6-1) na dhidi ya Kagera Sugar (4-0).

Pia Kamati ya Tuzo imemchagua Meneja wa Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo uliopo Dar es Salaam, Ashraf Omar, kuwa Meneja Bora wa Uwanja kwa mwezi Februari kutokana na kufanya vizuri katika menejimenti ya matukio ya michezo pamoja na masuala yanayohusu miundombinu uwanjani.

LIGI KUU NBC KUWAKA VIWANJA VITATU LEO.

LIGI Kuu ya NBC inaendelea leo kwa michezo mitatu itakayochezwa kwenye viwanja vitatu tofauti, miwili ikipigwa jijini Dar es salaam na mwingine mkoani Lindi.

Mchezo wa kwanza utazikutanisha timu za KMC dhidi ya Fountain Gate kwenye uwanja wa KMC Complex uliopo Dar es Salaam  saa 10:00 alasiri.

Fountain Gate inashika nafasi ya nane katika msimamo wa Ligi Kuu  ya NBC ikiwa na alama 24 huku KMC ikiwa nafasi ya11 na alama 24.

Mchezo mwingine utachezwa  saa 1:00 usiku kati ya Namungo ya mkoani Lindi na Singida Black Stars ya Singida kwenye uwanja wa Majaliwa mkoani Lindi.

Namungo ipo nafasi ya 12 katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC ikiwa na alama 23 na Singida BS ikishika nafasi ya nne baada ya kukusanya alama 41.

Mchezo wa tatu utachezwa saa 3:00 usiku kati ya Azam iliyotoka sare na Namungo kwenye mchezo uliopita dhidi ya Tanzania Prisons itakayokuwa ugenini kwenye uwanja wa Azam  Complex, Dar es Salaam.

Azam iliyoshindwa kupata ushindi kwenye michezo mitatu ya Ligi Kuu ya NBC mfululizo itajiuliza dhidi ya Prisons iliyopoteza mchezo wake uliopita ugenini dhidi ya Fountain Gate huku ‘Maafande’ hao wakiwa juu ya mstari wa kushuka daraja kwa nafasi moja pekee.

KENGOLD,MASHUJAA HAKUNA MBABE LIGI KUU NBC

MZUNGUKO wa 23 wa Ligi Kuu ya NBC umeendelea kwa mchezo mmoja uliochezwa uwanja wa Sokoine Mbeya majira ya saa kumi alasiri.

Mchezo ulianza kwa timu zote kusomana kwa kuwa zilikuwa zinahitaji kupata alama tatu mhimu ili kujiweka katika nafasi nzuri zaidi.

Iliwachukua dakika 21 kwa Mashujaa kupata bao la kwanza kupitia mchezaji Jafari Kibaya ambapo dakika  ya 26 mchezaji wa Mashujaa, Yusuf Dunia, alijifunga na kufanya mchezo kusomeka 1-1 matokeo yaliyobaki mpaka mwisho wa kipindi cha kwanza.

Kipindi cha pili kilianza kwa kasi kubwa ambapo dakika ya 47 mchezaji wa KenGold, Mishamo Daudi, aliiongezea timu yake bao la pili kabla ya Ally Nassor wa Mashujaa kuongeza bao la pili kwa mashujaa  hivyo ubao kusomeka 2-2 mpaka mwisho wa mchezo.

KenGold walifikisha alama 16 wakiwa nafasi ya 16 kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC huku Mashujaa wakifikisha alama 24 wakiwa nafasi ya 10.

Mchezaji wa Mashujaa,Ally Nassor ‘Ufudu’ alitangazwa kuwa nyota wa mchezo huo.Ligi Kuu ya NBC itaendelea leo kwa michezo mitatu.