Author: Yahaya Abushehe

CARGO, KAJUNA ZATAMBA NYUMBANI MTOANO FIRST LEAGUE.

Michezo ya mtoano (PlayOff) kubaki au kupanda ligi ya First League imechezwa Jana Mei 8 ikishuhudiwa timu zilizokuwa nyumbani Cargo ya Dar na Kajuna ya Kigoma zikiibuka na ushindi.

Mchezo wa kwanza katika uwanja wa TFF Center – Kigamboni uliishuhudia Cargo ikiibuka na ushindi wa mabao 3-2 dhidi ya Tunduru Korosho.

Mchezo wa pili mkoani Kigoma uliishuhudia Kajuna ikiifunga Copco ya Mwanza kwa mabao 2-0 kwenye uwanja wa Lake Tanganyika.

Michezo ya marudiano itapigwa Mei 12 ambapo Tunduru Korosho itaialika Cargo kwenye uwanja wa Majimaji mkoani Ruvuma huku Copco ikiialika Kajuna kwenye uwanja wa Nyamagana mkoani Mwanza.

NI VITA YA KUBAKI NA KUPANDA FIRST LEAGUE LEO.

Michezo ya mtoano (PlayOff) ya kubaki na kupanda First League inachezwa leo Mei 8 ikikutanisha timu mbili kutoka First League ambazo ni Tunduru Korosho ya Ruvuma na Copco ya Mwanza pamoja na timu mbili kutoka kwenye Fainali za mabingwa wa mikoa ambazo ni Cargo ya Dar es Salaam na Kajuna ya Kigoma.

Mechi ya kwanza itakutanisha timu ya Cargo dhidi ya Tunduru Korosho saa 10:00 alasiri kwenye uwanja wa TFF Center Kigamboni uliopo Dar.

Mechi ya pili itakutanisha timu ya Kajuna dhidi ya Copco kwenye uwanja wa Lake Tanganyika, Kigoma huku mchezo huo ukitarajiwa kupigwa saa 10:00 alasiri.

Ikumbukwe timu mbili kutoka First league ni zile zilizopoteza michezo ya Mtoano wa kushuka daraja (Relegation Playoffs) na kupata nafasi ya kupambania kubakia kwenye Ligi hiyo kwa msimu ujao.

Timu mbili kutoka Fainali za mabingwa wa mikoa ni zile zilizotolewa kwenye Nusu Fainali na kushika nafasi ya tatu na ya nne kwenye fainali hizo.

RAIS KARIA

RAIS KARIA AONGOZA UJUMBE WA TANZANIA VIENNA, AISHUKURU FIFA.

Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Wallace Karia ametoa shukrani kwa Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) kwa kuichagua Tanzania kuwa miongoni mwa washiriki wa Warsha ya kuimarisha maendeleo ya mpira wa miguu duniani inayohusisha Nchi Wanachama wa UEFA na CAF inayoendelea Vienna, Austria.

Rais Karia amesema ni heshima kwake na shirikisho kushiriki pamoja na mashirikisho mengine kutoka Afrika na Ulaya.

“Ni furaha kuwa miongoni mwa washiriki kwasababu mijadala mingi inasaidia sana na inatupa data za kuweza kuendeleza mpira wa miguu Nchini kwetu”

Amesema kuna haja ya warsha za aina hiyo kuendelea kutolewa zaidi ili kupata maarifa yanayoweza kusaidia katika shughuli za kila siku katika maendeleo ya mpira wa miguu.

Nchi zinazohudhuria kwenye Warsha hiyo ni Finland, Moldova, Wales, Austria, Georgia kutoka UEFA na Gabon, Morocco, Senegal, Tanzania na Cameroon kutoka CAF.

FIRST LEAGUE

HATMA YA KUBAKI FIRST LEAGUE KUAMULIWA LEO.

JIBU la timu gani itaendelea kusalia ligi ya First League msimu wa 2025/2026 litapatikana leo Aprili 30 kwenye michezo ya mzunguko wa pili wa mtoano wa kushuka daraja (Relegation Play Off).

Mapinduzi itaialika Tunduru Korosho kwenye uwanja wa Nyamagana, Mwanza huku Magnet ikiwa mwenyeji wa Copco kwenye uwanja wa Manungu mkoani Morogoro.

Kwenye michezo ya duru la kwanza Tunduru Korosho ilikuwa mwenyeji wa Mapinduzi kwenye uwanja wa Majimaji mkoani Songea mchezo uliomalizika kwa sare ya mabao 2-2 na Copco iliialika Magnet kwenye uwanja wa Nyamagana mkoani Mwanza mchezo uliomalizika kwa sare ya mabao 2-2.

Timu zitakazopoteza katika matokeo ya jumla (aggregate) zitapata nafasi ya kuendelea kujitetea kwa kucheza na timu mbili zitakazoshika nafasi ya tatu na ya nne kwenye Fainali za mabingwa wa mikoa.

MAFUNZO YA ‘VAR’ YAFUNGWA DAR ES SALAAM.

Kozi maalum ya Teknolojia ya Msaidizi wa Video (VAR) iliyofanyika kwa takribani siku 5 kwenye ukumbi wa uwanja wa Benjamin Mkapa Dar es salaam imefungwa rasmi Jana Aprili 18, 2025 ikijumisha waamuzi 20 kutoka Tanzania Bara na Visiwani ikiwa ni mwendelezo wa Kozi hiyo yenye jumla ya moduli 6 mpaka kutamatika.

Kozi hiyo ambayo ni sehemu ya mkakati wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kuhakikisha nchi inakuwa na waamuzi waliobobea kwenye matumizi ya teknolojia hiyo ya kisasa inayotumika kusaidia kutoa maamuzi sahihi uwanjani imefungwa rasmi Kwa awamu ya pili na Mkurugenzi wa Sheria, Habari na Masoko wa TFF Boniface Wambura ambaye pia ndiye msimamizi Mkuu wa Kozi hiyo inayowezeshwa na Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF).

Akizungumza baada ya kufunga rasmi awamu ya pili ya Kozi hiyo Mkurugenzi wa Sheria, Habari na Masoko wa TFF, Boniface Wambura aliwapongeza waamuzi waliomaliza mafunzo hayo na kuwataka kwenda kutumia vyema ujuzi walioupata kwa maendeleo ya soka la Tanzania.

Aidha Wambura alieleza kuwa Kozi hiyo ni muendelezo na kwamba TFF itaendelea kuwekeza kwenye teknolojia hiyo Kwa kutoa elimu Kwa waamuzi wengi zaidi na hata kuzalisha wakufunzi wazawa ili kuhakikisha usimamizi wa mechi nchini unaendana sawa na mabadiliko kulingana na wakati Kwa kufuata viwango vya kimataifa.

Ikumbukwe kozi hiyo ni hatua muhimu kuelekea maandalizi ya matumizi rasmi ya VAR katika mechi za ligi kuu ya NBC na mashindano mbalimbali yatakayofanyika ndani ya Tanzania.