Author: Yahaya Abushehe

MTIBWA KUREJEA LIGIKUU

ALAMA TANO KUIREJESHA MTIBWA LIGI KUU YA NBC.

VINARA wa Ligi ya Championship ya NBC Mtibwa Sugar inahitaji alama tano pekee kujihakikishia nafasi ya kurejea Ligi Kuu ya NBC kwa Mara nyengine tena msimu wa 2025/2026.

Mtibwa Sugar imekusanya jumla ya alama 63 kwenye michezo 26 ya Ligi ya Championship ya NBC ambapo alama tano zitamfanya kufikisha alama 68 huku ikiwa timu moja pekee yenye uwezo wa kufikia alama hizo (Mbeya City).

Ikumbukwe timu mbili za juu kwenye msimamo wa Ligi ya Championship ya NBC zinapanda moja kwa moja Ligi Kuu ya NBC.

Timu zinazoshika nafasi ya tatu na nne kwenye Ligi ya Championship ya NBC zinacheza mchezo wa mtoano kumtafuta mshindi mmoja wa kucheza mchezo wa mtoano wa kupanda (Promotion PlayOff) kwa timu ya Championship au kushuka (Relegation PlayOff) kwa timu ya Ligi Kuu.

‘MBUNGI’ TATU MIKOA MITATU NBC CHAMPIONSHIP LEO.

MICHEZO mitatu ya Ligi ya Championship ya NBC itachezwa leo Aprili 10 kwenye mikoa ya Songea, Pwani na Tanga ikichezwa kuanzia saa 10:00 alasiri.

Mkoani Songea, timu ya Songea United inaialika Stand United kwenye uwanja wa Majimaji.

Songea inashika nafasi ya saba kwenye msimamo wa Ligi hiyo ikiwa na alama 43 huku Stand United ikiwa nafasi ya tatu na alama 52.

Kiluvya ya mkoani Pwani itakuwa mwenyeji wa Mbeya Kwanza ya mkoani Mtwara kwenye uwanja wa Mabatini mkoani Pwani huku mchezo wa duru la kwanza Mbeya kwanza iliifunga kiluvya kwa mabao 2-1 mchezo uliopigwa kwenye uwanja wa Nangwanda Sijaona mkoani Mtwara.

Mchezo wa mwisho leo unazikutanisha African Sports dhidi ya TMA kwenye uwanja wa CCM Mkwakwani mkoani Tanga.

Hii ni kwa mara ya kwanza msimu huu African Sports inautumia uwanja wa CCM Mkwakwani kama uwanja wake wa nyumbani tangu ulipofanyiwa marekebisho makubwa.

Mapema wiki hii mzunguko wa 26 ulianza kwa mchezo kati ya Biashara United na Mbeya City ambapo mchezo huo ulimalizika kwa sare ya bao moja.

AZAM, YANGA NANI KUONDOKA NA ALAMA TATU LEO ?

USIKU wa deni haukawii kukucha ndivyo unavyoweza kusema, baada ya kusuburi wiki, Siku hatimaye yamesalia masaa kuelekea mchezo wa ‘Derby’ ya Dar es Salaam ambapo Azam FC itaialika Young Africans kwenye uwanja wa Azam Complex kuanzia saa 1:00 usiku.

Mara ya mwisho kukutana kwenye Ligi Kuu ya NBC Young Africans ilikubali kichapo cha bao 0-1 likifungwa na Gibril Sillah kwenye uwanja wa Azam Complex.

Young Africans inaingia kwenye mchezo huu ikiwa kinara wa Ligi Kuu ya NBC ikiwa na jumla ya alama 64 kwenye michezo 24 huku Azam FC ikiwa nafasi ya 3 na alama zake 51.

Viingilio vya mchezo huo ni 10,000 kwa mzunguko, 15,000 kwa VIP B na 20,000 kwa VIP A na zinapatikana kupitia wakala yeyote wa N-Card.

GUNNERS MABINGWA WA FIRST LEAGUE 2024/2025

TIMU ya Gunners kutoka mkoani Dodoma imefanikiwa kuwa Bingwa wa First League msimu wa 2024/2025 baada ya kuifunga Hausung mabao 3-0 kwenye mchezo wa Fainali uliochezwa jana Azam Complex, Dar es salaam.

Gunners ilimaliza kinara wa Kundi B ikiwa na alama 35 kwenye michezo 14 hivyo kupata nafasi ya kucheza mchezo wa Fainali ulioipa timu hiyo ubingwa.

Kwa upande wa Hausung ilimaliza kinara wa kundi A ikiwa na alama 25 kwenye michezo 14, alama ambazo ziliipa timu hiyo nafasi ya kucheza mchezo huo wa fainali kumtafuta bingwa wa jumla wa First League 2024/2025.

Timu zote mbili zimekata tiketi ya kushiriki Ligi ya Championship ya NBC msimu wa 2024/2025 baada ya kumaliza vinara wa makundi yao.

FAINALI YA FIRST LEAGUE KUPIGWA LEO CHAMANZI.

 

MCHEZO wa Fainali wa Ligi ya First League unapigwa leo April 5 kwenye uwanja wa Azam Complex, Dar es Salaam ukizikutanisha timu za Hausung kutoka Njombe na Gunners ya Dodoma.

Hii inafanyika kwa mara ya kwanza tangu maboresho ya kanuni ya First League kufanyika kwa msimu 2024/25 ambapo hapo awali Bingwa alikuwa akipatikana kwa timu nne za juu kila kundi kucheza shindano dogo la nane bora na timu zikipangwa kwenye makundi mawili yenye jumla ya timu nne na vinara wa kila kundi hucheza mchezo wa nusu fainali na fainali na hatimaye Bingwa kupatikana.

Ikumbukwe kuwa timu hizi tayari zimekwisha kata tiketi ya moja kwa moja kushiriki Ligi ya Championship ya NBC kwa msimu wa 2025/2026 kwa kuongoza makundi yao.