Category: STORY

AZAM, COASTAL WANA KIKAO LIGI KUU YA NBC LEO.

MATAJIRI wa Chamazi timu ya Azam leo itakuwa na kibarua cha kusaka alama tatu muhimu nyumbani dhidi ya Coastal Union kwenye uwanja wa Azam Complex, Dar es Salaam.

Ikiwa na kumbukumbu mbaya ya kuanza mwaka 2026 vibaya baada ya kupoteza kwenye fainali ya Kombe la Mapinduzi dhidi ya Young Africans Azam itavaana na Coastal inayoshika nafasi ya 12 kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC.

Azam inayoshika nafasi ya tisa bado haijapoteza mchezo wowote wa ligi hiyo msimu huu sawa na timu ya Young Africans ambayo pia haijapoteza mchezo.

Tayari Coastal Union imepoteza michezo mitatu msimu huu ikishinda miwili na kutoa sare mitatu ikiwa imekusanya jumla ya alama tisa hadi sasa.

Huu ni mchezo pekee wa Ligi Kuu ya NBC unaopigwa leo baada ya jana timu ya Dodoma Jiji kulazimishwa sare ya bao moja nyumbani na Singida Black Stars.

 

DODOMA, SINGIDA ZATOSHANA NGUVU LIGI KUU YA NBC.

UKIWA mchezo wa kwanza unaorejesha ladha za Ligi Kuu ya NBC baada ya kusimama kwa takribani wiki tano umeshuhudia timu za Dodoma Jiji na Singida Black stars zikimaliza kwa sare ya bao moja na kugawana alama kwenye uwanja wa Jamhuri, Dodoma.

Mchezo huo uliokuwa mkali na wa kusisimua ulishuhudia mabao ya timu zote mbili yakipatikana dakika za ‘jioni’ kwa mikwaju ya penati iliyopigwa na Yasin Mgaza (Dodoma) dakika ya 83 na Marouf Tchakei (Singida) dakika ya 96.

Hii ni sare ya nne kwa timu ya Dodoma Jiji msimu huu huku ikuwa sare ya tatu kwa timu ya Singida Black Stars inayoiwakilisha Tanzania na Ligi ya nne kwa ubora Afrika (NBC) kwenye mashindano ya kimataifa msimu huu.

Akizungumza baada ya mchezo kocha mkuu wa Dodoma Jiji Amani Josiah amesema kukosa umakini kwa wachezaji wake kumesababisha kupoteza alama tatu na kuipata alama moja ingawa amewasifu kwa kiwango walichoonyesha ingawa mpinzani wao (Singida BS) alikuwa mgumu.

”Tumepata bao kipindi cha pili japo kipindi cha kwanza tumetengeneza nafasi nzuri za kupata mabao na endapo tungezitumia vizuri tungepata ushindi, yote kwa yote nawasifu wachezaji wangu wamepambana sana na hii alama moja tuliyoipata itatusaidia kutujenga huko mbele tunapoelekea” alisema Josiah.

Naye kocha mkuu wa Singida BS David Ouma raia wa Kenya amewasifu Dodoma kwa matumizi ya mipira mirefu iliyowapa changamoto wachezaji wake ingawa amewasifu vijana wake pia kwa kuonyesha mchezo mzuri.

”Mbinu waliyokuja nayo Dodoma kupiga mipira mirefu ilivuruga wachezaji wangu nyuma na kuwapa faida wao na endapo tungefanikiwa kuzuia mipira hiyo kipindi cha kwanza ingetusaidia kupata matokeo bora zaidi leo. Naamini kurejea kwa ligi kutatusaidia kuendelea kujijenga na kuwa bora zaidi katika michezo inayokuja” Alisema Ouma.

 

TRANSIT YAFUKUZA ‘MWIZI’ KIMYA, BIGMAN, GEITA HAKUNA MBABE NBC CHAMPIONSHIP.

TIMU ya Transit Camp imerejea katika matokeo ya ushindi baada ya kuifunga KenGold bao moja kwenye uwanja wa nyumbani na kufanikiwa kusalia na alama zote tatu.

Mchezo huo uliopigwa uwanja wa TFF Center Kigamboni ulishuhudia Adam Uledi wa Transit Camp akiibuka shujaa kwa kuifungia Transit bao pekee kipindi cha pili kwa mkwaju wa penati huku likiwa bao la 11 kwake akiendelea kuongoza kwenye vinara wa mabao katika ligi ya Championship ya NBC.

Ushindi huo unaifanya Transit kufikisha alama 33 na kupanda hadi nafasi ya tatu ya msimamo ikiwa nyuma ya kinara wa ligi hiyo Geita Gold kwa alama nne pekee.

Mkoani Lindi kwenye uwanja wa Ilulu timu ya Bigman ilikuwa mwenyeji wa Geita Gold na kushuhudia mchezo huo ukikamilika kwa timu hizo kutoka sare ya bao moja.

Geita inayoongoza msimamo wa ligi hiyo kwa alama 37 imeshindwa kukusanya alama zote nyumbani kwa Bigman ambayo imeizidi alama 17 huku timu hiyo (Bigman) ikishika nafasi ya saba kwenye msimamo.

Hii ni sare ya pili mfululizo kwa timu ya Bigman kwenye uwanja wa nyumbani baada ya mchezo uliopita kulazimishwa sare na timu ya African Sports kutoka Tanga.

ILULU, KIGAMBONI KINAWAKA LEO NBC CHAMPIONSHIP.

LIGI ya Championship ya NBC inatarajiwa kuendelea leo kwa mzunguko wa 15 huku viwanja vya Ilulu, Lindi na TFF Center Kigamboni vikitarajiwa kutimua vumbi leo.

Bigman ya Lindi itakuwa mwenyeji wa Geita Gold inayoshika usukani wa Ligi ya Championship ya NBC kwenye uwanja wa Ilulu huku timu ya Bigman ikiwa na kumbukumbu mbaya ya kulazimishwa sare kwenye uwanja huo na timu ya African Sports katika mchezo uliopita.

Hadi sasa timu ya Bigman imepoteza michezo mitano ya ligi hiyo na inakutana na Geita Gold ambayo haijapoteza mchezo wowote hadi sasa huku ikitoka sare michezo mitatu pekee.

Kwenye uwanja wa TFF Center Kigamboni timu ya Transit Camp itakuwa mwenyeji wa ‘wababe’ kutoka mbeya timu ya Kengold iliyoshiriki Ligi Kuu ya NBC msimu uliopita.

Transit Camp iliyopoteza mchezo uliopita kwa kipigo kikali cha mabao 3-0 dhidi ya Mbuni ugenini itashuka uwanjani kupambana na Kengold iliyopoteza pia ugenini kwa mabao 2-1 dhidi ya B19 inayoshika nafasi ya 13 kwenye msimamo huku ikiifanya B19 kufikisha ushindi wa pili msimu huu.

Transit Camp inahitaji kushinda mchezo wa leo ili kuweka hai matumaini ya kupanda daraja na kushiriki Ligi Kuu ya NBC msimu ujao ikishika nafasi ya nne kwenye msimamo hadi sasa nyuma ya vinara Geita Gold, Kagera Sugar na Mbeya Kwanza.

 

Ratiba ya Ligi Kuu ya NBC 2025/2026

LIGI KUU YA NBC KUREJEA LEO.

BAADA ya kusimama kwa takribani wiki tano Ligi Kuu ya NBC inatarajiwa kurejea leo Januari 16 kwa mchezo utakaopigwa kwenye uwanja wa Jamhuri, Dodoma kati ya timu ya Dodoma jiji itakayokuwa mwenyeji wa Singida Black Stars.

Dodoma Jiji iliyoanza vibaya msimu huu imeshinda mchezo mmoja pekee wa Ligi Kuu ya NBC kwenye michezo nane iliyocheza huku ikishika nafasi ya 15 kwenye msimamo itaikaribisha Singida Black Stars inayoshika nafasi ya 15 ikishinda michezo miwili baada ya kucheza mitano.

Singida Black Stars inashuka uwanjani leo chini ya kocha mpya David Ouma baada ya kubadilisha majukumu ya aliyekuwa kocha mkuu wa kikosi hicho Miguel Gamondi mwenye nafasi mpya ya Mkurugenzi wa ufundi katika timu hiyo.

Hadi sasa usukani wa Ligi Kuu ya NBC unashikiliwa na timu ya JKT Tanzania yenye alama 17 huku timu ya KMC ikishika nafasi ya mwisho (16) ikikusanya alama nne pekee huku ikiwa imeshinda mchezo mmoja sawa na Dodoma Jiji inayoshika nafasi ya 15.

Mchezo wa leo utapigwa kwenye uwanja wa Jamhuri, Dodoma saa 1:00 usiku na ndio mchezo pekee wa Ligi Kuu ya NBC utakaopigwa leo na utarushwa mbashara kwenye chaneli ya Azam Sports.