MATAJIRI wa Chamazi timu ya Azam leo itakuwa na kibarua cha kusaka alama tatu muhimu nyumbani dhidi ya Coastal Union kwenye uwanja wa Azam Complex, Dar es Salaam.
Ikiwa na kumbukumbu mbaya ya kuanza mwaka 2026 vibaya baada ya kupoteza kwenye fainali ya Kombe la Mapinduzi dhidi ya Young Africans Azam itavaana na Coastal inayoshika nafasi ya 12 kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC.
Azam inayoshika nafasi ya tisa bado haijapoteza mchezo wowote wa ligi hiyo msimu huu sawa na timu ya Young Africans ambayo pia haijapoteza mchezo.
Tayari Coastal Union imepoteza michezo mitatu msimu huu ikishinda miwili na kutoa sare mitatu ikiwa imekusanya jumla ya alama tisa hadi sasa.
Huu ni mchezo pekee wa Ligi Kuu ya NBC unaopigwa leo baada ya jana timu ya Dodoma Jiji kulazimishwa sare ya bao moja nyumbani na Singida Black Stars.