Category: STORY

KARIAKOO DABI KUPIGWA MEJA JENERALI ISAMUHYO.

BODI ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) inatangaza mabadiliko ya uwanja wa mchezo namba 169 wa Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2025/2026, kati ya klabu ya Simba na klabu ya Young Africans, maarufu kama ‘Kariakoo Derby’.

Mchezo huo ambao hapo awali ulipangwa kufanyika kwenye uwanja wa Benjamin Mkapa, sasa utachezwa kwenye uwanja wa Mej. Jenerali Isamuhyo mkoani Dar es Salaam Mei 3, 2026 kuanzia saa 12:00 jioni.

Sababu ya mabadiliko hayo ni uwanja wa Benjamin Mkapa kuwa kwenye matengenezo.

Klabu za Simba na Yanga pamoja na wadau wengine wa Ligi Kuu ya NBC wamepatiwa taarifa zote kuhusiana na mabadiliko ya uwanja wa mchezo huo na maandalizi yake yanaanza mara moja ili kuhakikisha unafanyika katika kiwango cha juu kinachoendana na hadhi ya michezo mikubwa ya Ligi ya sita kwa ubora barani Afrika.

Bodi ya Ligi Kuu Tanzania inawatakia maandalizi mema wadau wote wa mchezo.

BODI YA LIGI KUU TANZANIA (TPLB) KUPOKEA MABORESHO YA KANUNI ZA LIGI

BODI ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) inautaarifu umma kuwa imeanza kupokea maoni ya maboresho ya Kanuni za Ligi kwa toleo la mwaka 2026. Maoni/mapendekezo hayo ya maboresho ya kanuni ni kwa ajili ya Ligi Kuu Ligi ya Championship na First League.

Lengo la zoezi hili ni kuboresha Kanuni za Ligi ili ziweze kutatua changamoto zilizojitokeza na zinazoweza kujitokeza katika msimu wa 2025/2026. Mchakato huu wa kupokea maoni utafanyika kwa kipindi cha majuma manne (4) na umefunguliwa rasmi Aprili 22, 2026.

Bodi inawakumbusha wadau wote kuwa kanuni bora ni msingi wa kuwa na ligi bora na maendeleo ya mpira wa miguu kwa ujumla, hivyo ushiriki wa kila mdau ni jambo la muhimusana.

Maoni ya maboresho ya kanuni yawasilishwe TPLB kabla ya Mei 22, 2026 kwa kupitia njia zifuatazo;

i. Barua pepe – maoni@ligikuu.co.tz

ii. Ujumbe mfupi wa maandishi (SMS) au WhatsApp +255 758 500 222

iii. Kuwasilisha kwa mkono katika ofisi za Bodi ya Ligi Kuu Tanzania zilizopo

ghorofa ya 14 kwenye jengo la NSSF (Mafao House), Ilala – Dar es Salaam.

CHIRWA KINARA WA MABAO NBC CHAMPIONSHIP. 

 

 

LIGI ya Championship ya NBC msimu wa 2025/26 inaendelea kushika kasi huku vita ya ufungaji ikizidi kupamba moto huku wachezaji mbalimbali wakionyesha uwezo wao wa kutikisa nyavu.

Kinara wa orodha hiyo anaekipiga katika kikosi cha Kagera sugar Obrey Chirwa tayari ameweka kambani mabao 14 na kuwa kileleni mwa wafungaji.

 

Akifuatiwa na Adam Uledi wa Transit Camp ambaye amehamia KMC inayoshiriki Ligi Kuu ya NBC mwenye mabao 11 sawa na Ramadhani Hashimu kutoka timu ya B19 inayopambana vikali kusalia Ligi ya Championship ya NBC.

 

Nafasi ya tatu inashikwa na Boniface Brown wa Mbeya Kwanza mwenye mabao 10 sambamba na Abdereheman Mussa wa Transit Camp na Maulid Shaban kutoka Geita Gold wote wakiwa na idadi hiyo ya mabao.

 

Ushindani huu unaonyesha wazi kuwa msimu huu ni wa ushindani mkubwa ambapo kila mchezaji anapambana kuisaidia timu yake pamoja kuwania kiatu cha ufungaji bora.

Ratiba ya Ligi Kuu ya NBC 2025/2026

TAARIFA YA KAMATI YA UENDESHAJI NA USIMAMIZI WA LIGI YA BODI YA LIGI KUU TANZANIA (TPLB).

Kamati ya Uendeshaji na Usimamizi wa Ligi ya Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) katika kikao chake cha Aprili 18, 2026 ilipitia mwenendo na matukio mbalimbali ya Ligi na kufanya maamuzi yafuatayo;

Ligi Kuu ya NBC

Mechi Namba 07: TRA United FC 0-0 Simba SC

Klabu za TRA United na Simba za Dar es Salaam zimetozwa faini Sh. 5,000,000 (milioni tano) kila moja kwa kosa la walinzi wa klabu hizo (Stewards) kupigana mara baada ya timu hizo kuwasili kwenye uwanja wa Sheikh Amri Abeid, Arusha. Adhabu hii ni kwa mujibu wa Kanuni ya 47:1 ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti kwa Klabu.

Mechi Namba 132: Pamba Jiji FC 0-3 Young Africans SC

Mchezaji Mudathir Yahya wa klabu ya Young Africans amefungiwa michezo mitatu (3) na kutozwa faini ya Sh. 1,000,000 (milioni moja) kwa kosa la kumpiga kiwiko mchezaji wa Pamba Jiji, Ibrahim Abraham wakati mchezo unaendelea kwenye uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza. Adhabu hii ni kwa mujibu wa Kanuni ya 41:5(5.2) ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti kwa Wachezaji.

Mechi Namba 146: Coastal Union FC 1-1 Mtibwa Sugar FC

Klabu ya Coastal Union ya mkoani Tanga imetozwa faini ya Sh. 5,000,000 (milioni tano) kwa kosa la mashabiki wake kurusha chupa za maji kiwanjani wakati mwamuzi wa kati na mwamuzi msaidizi namba moja wakiwa wanatuliza vurugu zilizokuwa zikiendelea baada ya mchezaji wa Mtibwa Sugar, Victor Collins kumsukuma mchezaji wa Coastal Union Athuman Makambo. Adhabu hii ni kwa mujibu wa Kanuni ya 47:1 ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti kwa Klabu.

 

Mechi Namba 151:  TRA United 2-0 Singida BS

Klabu ya Singida BS ya mkoani Singida imetozwa faini ya Sh. 5,000,000 (milioni tano) kwa kosa la viongozi wake wawili kuingia kiwanjani na kumwaga vimiminika. Viongozi hao walifanya tukio hilo lililotafsiriwa kama vitendo vinavyoashiria imani za kishirikina, kabla ya timu kutoka kwa ajili ya kupasha moto misuli. Adhabu hii ni kwa mujibu wa Kanuni ya 47:1 ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti kwa Klabu.

Mechi Namba 152: Azam FC 0-0 Simba SC

Klabu ya Azam ya mkoani Dar es Salaam imetozwa faini ya Sh. 5,000,000 (milioni tano) kwa kosa la viongozi wa benchi la ufundi pamoja na wachezaji kutumia mlango usio rasmi kuingia uwanjani kinyume na matakwa ya kanuni ya 17:21 ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo na makubaliano yaliyofanyika kwenye kikao cha maandalizi ya mchezo huo. Adhabu hii ni kwa mujibu wa Kanuni ya 17:62 ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.

 

Klabu ya Simba ya mkoani Dar es Salaam imetozwa faini ya Sh. 10,000,000 (milioni kumi) kwa kosa la mashabiki wake kumrushia chupa za maji mwamuzi msaidizi namba mbili wa mchezo huo, mara baada kunyoosha kibendera kuashiria mchezaji wa Simba kuotea.

Hili ni kosa la kujirudia kwa klabu ya Simba ambapo ndani ya msimu huu wa Ligi kuu ya NBC 2025/2026, mashabiki wa klabu hiyo walitenda kosa hilo katika michezo miwili tofauti na kusababisha klabu kuadhibiwa. Adhabu hii ni kwa mujibu wa Kanuni ya 47:1 ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti kwa Klabu.

‘WANANCHI’ WATIKISA KWA VIPIGO VIZITO LIGI KUU YA NBC.

KWENYE msimu huu wa Ligi Kuu ya NBC klabu ya Young Africans imejijengea heshima kubwa si tu kwa kushinda michezo yake bali namna inavyoshinda kwa mabao mengi na soka la kuvutia linaloacha alama kwa mashabiki na wapinzani wao.

Katika msimu huu, Young Africans imeonyesha ubora wa kipekee kwenye safu ya ushambuliaji kwa kutoa vipigo vizito kwa baadhi ya timu za Ligi Kuu ya NBC.

Moja ya matokeo yaliyotikisa ni ushindi wa mabao 6-0 dhidi ya Mashujaa ya Kigoma iliyoupata kwenye uwanja wa KMC, ambapo walionesha tofauti kubwa ya kiwango kuanzia mwanzo hadi mwisho wa mchezo ikiwa hadi kufika mapumziko ‘Wananchi’ walikuwa wanaongoza mabao matatu na kipindi cha pili kufunga matatu pia.

‘Mvua’ hiyo ya mabao ilishushwa na Mohamed Damaro, Duke Abuya, Pacome Zouzoua, Prince Dube, Mudathir Yahya na Laurindo Dilson huku golikipa aliyekuwa langoni Abutwalib Mshery akimaliza mchezo bila kuruhusu bao.

Bado ‘Wananchi’ waliongeza ushindi mwingine mkubwa wa mabao 5-0 dhidi ya JKT Tanzania, wakithibitisha kuwa ushindi wao mkubwa si tukio la bahati mbaya bali ni sehemu ya utambulisho wao msimu huu huku kila mchezo ukionekana kama fursa ya kuonyesha ubora zaidi, na Young Africans imekuwa ikipeleka presha kubwa kwa timu pinzani kwa mtindo wao wa kucheza soka la kasi, pasi nyingi, na umaliziaji mkali.

Katika ushindi huo Mohamed Hussein, Prince Dube, Laurindo Dilson, Mudathir Yahya na Sheikhan Hamis waliingia kambani na kupeleka kilio kwa timu ya Mashujaa.

Kana kwamba haitoshi, walirudia tena matokeo ya 6-0 dhidi ya Mbeya City, wakionyesha ukali kwenye ushambuliaji ambapo katika mechi hiyo, mfumo wa timu ulifanya kazi kwa ufanisi mkubwa kuanzia kiungo kinachotengeneza nafasi hadi washambuliaji wanaomalizia kwa umakini wa hali ya juu.

Pacome Zouzoua na Prince Dube walifunga mabao mawili kila mmoja huku Maxi Nzengeli na Mohamed Hussein wakifunga bao moja kila mmoja na kuendelea kuzamisha jahazi la Mbeya City iliyopo kwenye nafasi mbaya katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC.

Kinachovutia zaidi ni namna timu hii imeweza kudumisha njaa ya ushindi licha ya kuwa tayari kileleni mwa msimamo na wachezaji wao wanaonekana kuwa na maelewano mazuri uwanjani, jambo linalochangia kupatikana kwa nafasi nyingi za kufunga katika kila mchezo.

Kwa mashabiki, haya si matokeo tu bali ni burudani, ambapo mabao mengi yanakuwa sehemu ya furaha ya mashabiki walioko uwanjani na wale wanaofuatilia kupitia runinga ikiwa wazi kuwa msimu huu, Young Africans haichezi tu kushinda bali pia kutoa ujumbe kwa wapinzani wao.