Category: STORY

PAMBA, YANGA, PRISONS ZATEMBEZA ‘DOZI’ LIGI KUU YA NBC.

 

Michezo mitatu ya raundi ya 27 ya Ligi Kuu ya NBC imechezwa jana katika viwanja tofauti huku mechi zote zikichezwa muda mmoja wa saa 10:00 alasiri huku Pamba Jiji , Yanga na Tanzania Prisons zikiibuka na ushindi muhimu.

Katika uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza, Pamba Jiji imepata ushindi mnono kwa kuichapa Mtibwa Sugar mabao 4-0 huku mshambuliaji Methew Tegis akiwa nyota wa mchezo baada ya kufunga (hat-trick) katika dakika za 17, 46 na 48, na Shaphan Siwa akifunga bao lingine dakika ya 43.

Uwanja wa Sheikh Amri Abeid ulishuhudia Yanga ikiendeleza mwenendo wake mzuri kwa kuibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Fountain Gate.

Pacome Zouzou aliifungia Yanga bao la kwanza mapema kipindi cha pili kabla ya Laurindo Depu kuongeza la pili na kuhakikisha ‘Wananchi’ wanaondoka na Alama zote tatu.

Nako kwenye Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, Tanzania Prisons iliibuka na ushindi mwembamba wa bao 1-0 dhidi ya JKT Tanzania kwenye uwanja wa ugenini.

Bao pekee la mchezo lilifungwa na George Mpole dakika ya 45 kwa mkwaju wa penati.

Matokeo hayo yanaendelea kuongeza ushindani katika Ligi Kuu ya NBC huku kila timu ikisaka kutimiza malengo yake kabla ya msimu wa 2025/26 kufikia tamati.

PAZIA LA FIRST LEAGUE LAFUNGWA.

Pazia la First League limefungwa jana kwa timu ya Rhino Rangers ya Tabora kufanikiwa kutwaa ubingwa wa First League msimu wa 2025/26 baada ya kuibuka na ushindi wa mikwaju ya penalti 4-2 dhidi ya Bandari kufuatia sare ya mabao 2-2 ndani ya dakika 90 za mchezo wa fainali uliopigwa kwenye Uwanja wa Azam Complex, Dar.

 

Mchezo huo ulianza kwa kasi huku Rhino Rangers wakitangulia kupata bao kupitia Iddy Manyerere dakika ya 6.

 

Bandari walijibu dakika ya 10 kupitia Mussa Ally kabla Iddy Manyerere kuongeza tena la pili dakika ya 40 na kuirejeshea Rhino Rangers uongozi wa 2-1 kabla ya mapumziko.

 

Bandari walionyesha mapambano makubwa kipindi cha pili na kufanikiwa kusawazisha dakika ya 89 kupitia Benedicto Jacob na kuufanya mchezo kumalizika kwa sare ya 2-2 ndani ya muda wa kawaida.

 

Katika mikwaju ya penalti, Rhino Rangers walikuwa watulivu na makini zaidi wakishinda kwa mabao 4-2 na kutwaa taji la First League 2025/26 mbele ya mashabiki.

 

Ushindi huo unahitimisha msimu mzuri kwa Rhino Rangers ambao wameonyesha uimara, nidhamu na uthabiti katika safari yao ya kutwaa ubingwa wa First League.

MPANZU AIBEBA SIMBA,NDUMUMWE AKIWEKA REKODI MPYA LIGI KUU YA NBC.

Timu ya Simba imeendelea kuweka presha katika mbio za Ligi Kuu ya NBC baada ya kuibuka na ushindi mwembamba wa bao 1-0 ugenini dhidi ya Mbeya City katika mchezo uliochezwa jana mkoani Mbeya kwenye uwanja wa sokoine.

Bao pekee la mchezo lilifungwa na Elie Mpanzu dakika ya 43, akimalizia vyema shambulizi la Simba na kuwapa ‘Wekundu wa Msimbazi’ uongozi ambao waliulinda hadi filimbi ya mwisho.

Ushindi huo unaifanya Simba kuendelea kukusanya alama muhimu katika hatua za mwisho za msimu ikikusanya alama 64 na kukaa nafasi ya kwanza ikiwa mchezo mmoja mbele ya timu inayofuata ya Young Africans.

Mchezaji Bora wa mchezo Elie Mpanzu Simba alifunga bao la ushindi lililoamua matokeo ya mchezo na kuonyesha kiwango bora katika eneo la ushambuliaji na akiongoza Simba kupata alama zote tatu.

Katika mchezo mwingine uliokuwa ukichezwa mkoani Singida uwanja wa Airtel ambao Singida Black Stars iliibuka na ushindi mkubwa wa mabao 5-0 dhidi ya Dodoma Jiji .

Nyota wa mchezo huo alikuwa Ndumumwe Mossi, aliyefunga mabao matatu (hat-trick) akiiongoza Singida Black Stars kupata ushindi mnono mbele ya mashabiki wao.

Mabao mengine yalifungwa na Linda Mtange dakika ya 40 na Mishamo Daudi dakika ya 67 huku Singida Black Stars ikitawala mchezo kuanzia mwanzo hadi mwisho kwa kuonyesha ubora mkubwa katika umiliki wa mpira, utengenezaji wa nafasi na umaliziaji makini, huku safu yao ya ulinzi ikihakikisha Dodoma Jiji haipati nafasi ya kutikisa nyavu.

Ndumumwe Mossi aliyeonyesha kiwango bora aliibuka mchezaji bora wa mchezo akiichangia ushindi kwa kufunga mabao matatu (hat-trick) na kuwa nyota wa mchezo.

AZAM COMPLEX KUPAMBWA NA FAINALI YA FIRST LEAGUE LEO.

Mabingwa wa makundi ya Ligi ya First League kutoka kundi A na B msimu wa 2025/26, Rhino Rangers waliokuwa kundi B na Bandari Tanzania walikuwa kundi A , leo Juni 17, 2026, watashuka dimbani katika mchezo wa fainali wa kumtafuta bingwa wa jumla wa Ligi ya First League.

 

Mchezo huo utachezwa kwenye Uwanja wa Azam Complex jijini Dar es Salaam kuanzia saa 1:00 usiku, huku ukiwa na uzito mkubwa kwa timu zote mbili ambazo tayari zimefanikiwa kupanda daraja kwenda Ligi ya Championship ya NBC kwa msimu wa 2026/27 baada ya kutwaa ubingwa wa makundi yao. 

 

Mbali na kuwania taji la bingwa wa jumla wa First League mechi hiyo itakuwa ya heshima na kujivunia mafanikio ya msimu mzima ambapo mshindi atamaliza kampeni akiwa ndiye bingwa rasmi wa First League 2025/26.

 

Mashabiki wa soka wanatarajiwa kushuhudia pambano kali kati ya timu mbili zilizoonyesha ubora na uthabiti katika safari yao ya kupanda daraja ambapo Mchezo huo utarushwa mubashara kupitia Azam Sports 1 HD, huku sherehe za kukabidhi kombe la ubingwa zikifanyika mara baada ya filimbi ya mwisho kupulizwa.

HAKUNA MBABE RUANGWA, AZAM IKIJIIMARISHA LIGI KUU YA NBC.

 

 

Namungo na TRA United zimeshindwa kutambiana nguvu baada ya kutoka sare ya bila kufungana katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC uliochezwa leo majira ya saa 10: 00 alasiri uwanja wa Majaliwa mkoani Lindi.

 

Mchezo huo uliokuwa na ushindani mkubwa uliwashuhudia pande zote zikitengeneza nafasi kadhaa za kufunga, lakini uimara wa safu za ulinzi pamoja na walinda milango ulihakikisha hakuna timu iliyofanikiwa kuona lango la mwenzake hadi dakika 90 zinakamilika. 

 

Matokeo hayo yanaifanya kila timu kujiongezea alama moja muhimu katika hatua za mwisho za msimu huku TRA United ikiendelea kubaki ndani ya nafasi za juu zaidi kuliko Namungo kwenye msimamo wa ligi. 

 

Jofrey luzendaze wa TRA United alitajwa kuwa mchezaji bora wa mechi kutokana na mchango wake kwa timu kupata alama tatu.

 

Katika mchezo mwingine Azam imeendelea kuonyesha ubora wake katika mbio za kumaliza msimu wa Ligi Kuu ya NBC kwa ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Mashujaa katika mchezo uliochezwa leo saa 1:00 jioni kwenye uwanja wa Azam complex chamazi.

 

Mabao ya Azam yalifungwa na Sadio Kanoute dakika ya 39 kabla ya James Akaminko kuongeza la pili dakika ya 41 na kuwapa Wanalambalamba ushindi muhimu. 

 

Mchezaji Bora wa Mchezo James Akaminko ndie aliyeng’ara zaidi baada ya kufunga bao la kwanza na kuwa na mchango mkubwa katika ushindi wa timu ya Azam.