Category: STORY

Ratiba ya Ligi Kuu ya NBC 2025/2026

TAARIFA YA KAMATI YA USIMAMIZI WA LIGI YA BODI YA LIGI KUU TANZANIA (TPLB).

Kamati ya Uendeshaji na Usimamizi wa Ligi ya Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) katika kikao chake cha Mei 9, 2026 ilipitia mwenendo na matukio mbalimbali ya Ligi na kufanya maamuzi yafuatayo;

Ligi Kuu ya NBC

Mechi Namba 169: Simba SC 2-2 Young Africans

Klabu ya Young Africans imepewa Onyo Kali kwa kosa la kuchelewa kuwasili kwenye uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, Dar es Saalam kuelekea mchezo tajwa hapo juu Mei3, 2026. Young Africans iliwasili uwanjani saa 10:35 alasiri badala ya saa 10:30 alasiri jambo ambalo ni kinyume na matakwa ya Kanuni ya 17:15 ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa Kanuni ya 17:62 ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.

Young Africans imetozwa faini ya Sh. 30,000,000 (milioni thelathini) kwa kosa la wachezaji na maofisa wake wa ufundi kukataa kutumia chumba rasmi cha kuvalia kwenye uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, Dar es Salaam badala yake walitumia nyumba iliyo nje ya uwanja upande wa pili wa Barabara kinyume na matakwa ya kanuni ya 17:20 ya Ligi Kuu kuhusu Taratibu za Mchezo.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa Kanuni ya 27:7 ya Ligi Kuu kuhusu Vyombo vya Maamuzi.

Meneja wa Klabu ya Young Africans Walter Harson amefungiwa michezo mitatu na kutozwa faini ya Sh. 1,000,000 (milioni moja) kwa kosa la kumsukuma mchezaji wa Simba Clatous Chama kwenye mchezo tajwa hapo juu.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa kanuni ya 45:2(2.1) ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti kwa Makocha na Maofisa Wengine wa Ufundi.

Shabiki wa klabu ya Young Africans aliyetambulika kwa jina la Mohamed Ally Mposo ambae amekuwa akiambatana na maofisa wa ufundi wa klabu hiyo amefungiwa kuingia uwanjani kwa kipindi cha miezi 12 kwa kosa la kuingia kwenye eneo la kuchezea wakati wa mapumziko na kumwaga vimiminika kitendo kilichotafsiriwa kama imani za kishirikina.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa kanuni ya 47:2 ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti kwa Klabu.

 Mechi Namba 154: Mtibwa Sugar 0-1 Dodoma Jiji FC

Klabu ya Dodoma Jiji ya Dodoma imetozwa faini ya Sh. 5,000,000 (milioni tano) kwa kosa la kuchelewa kufika kwenye kikao cha maandalizi ya mchezo (MCM) huku wakiwa pungufu bila kuwa na vifaa vyote vinavyohitajika kikanuni, Dodoma Jiji iliwakilishwa na wawakilishi wawili pekee badala ya watano huku wakiwa hawana vifaa kamili kinyume na matakwa ya kanuni 17:2 (2.2).

Adhabu hii ni kwa mujibu wa kanuni ya 17:62 kuhusu Taratibu za Mchezo.

Ligi ya Championship ya NBC

Mechi Namba 172: Geita Gold 6-1 Hausung FC

Klabu ya Hausung ya Mkoani Njombe imetozwa faini ya Sh. 1,000,000 (milioni moja) kwa kosa la maofisa wake kuchelewa kufika kwenye kikao cha maandalizi ya mchezo (MCM) kwa dakika 20, maofisa hao walifika saa 1:35 usiku badala ya saa 1:15 usiku kinyume na matakwa ya kanuni ya 17:2 (2.2) ya Championship kuhusu Taratibu za Mchezo.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa kanuni ya 17:62 kuhusu Taratibu za Mchezo

Mechi Namba 182: TMA FC 2-0 Gunners FC

Mchezaji wa TMA Said Kulwa amefungiwa michezo mitatu (3) na kutozwa faini ya Sh. 500,000 (laki tano) kwa kosa la kuonekana na chupa yenye kimiminika na kumwaga kimiminika hicho kwenye upande wa timu ngeni wakati wa ukaguzi wa uwanja jambo lililotafsiriwa kama imani za kishirikina.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa Kanuni ya 41:5(5.5) ya Championship kuhusu Udhibiti kwaWachezaji.

Wachezaji Mohamed Lipangala na Joel Stephano wa TMA FC, wamefungiwa michezo mitatu (3) na kutozwa faini ya Sh. 500,000 (laki tano) kila mmoja kwa kosa la kuonekana wakichimbia vitu kwenye nguzo ya timu yao jambo lililo tafsiriwa kama imani za kishirikina.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa Kanuni ya 41:5(5.5) ya Championship kuhusu Udhibiti kwa Wachezaji.

Mechi Namba 190: Mbeya Kwanza vs Hausung FC

Klabu ya Hausung FC ya mkoani Njombe imepoteza mchezo tajwa hapo juu na Timu ya Mbeya Kwanza ya mkoani Tabora imepewa ushindi wa mabao matatu (3) na alama (3) kwa kosa la Hausung FC kushindwa kufika kwenye uwanja wa Ali Hassan Mwinyi, Tabora bila sababu za msingi na zinazokubalika hivyo kusababisha mchezo huo kushindwa kufanyika.

Sambamba na adhabu hiyo, Hausung FC imetozwa faini ya Sh. 10,000,000 (milioni kumi)na kutakiwa kulipa fidia ya maandalizi ya mchezo huo Pamoja na kupokwa alama tatu (3) katika msimamo wa Ligi ya Championship.Pia Mwenyekiti wa klabu ya Hausung FC, Erasto Haule amefungiwa kwa kipindi cha mwakammoja (1) kwa kosa la klabu yake kushindwa kufika uwanjani.

Adhabu hizi ni kwa mujibu wa Kanuni ya 31:1(1.1, 1.2, 1.3 & 1.4) ya Championship kuhusu Kutofika Uwanjani.

First League

Mechi Namba 37B: Alliance FC 0-3 IAA FC

Klabu ya Alliance ya mkoani Mwanza imetozwa faini ya Sh. 500,000 (laki tano) kwa kosa la maofisa wake kushindwa kuhudhuria kikao cha kitaalam cha maandalizi ya mchezo (MCM) kinyume na matakwa ya Kanuni ya 17:2(2.2) ya First League kuhusu Taratibu za Mchezo.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa Kanuni ya 17:62 ya First League kuhusu Taratibu za Mchezo.

Klabu ya Alliance ya mkoani Mwanza imetozwa faini ya Sh. 1,000,000 (milioni moja) kwakosa la shabiki wake kumvamia mwamuzi wa kati wa mchezo tajwa hapo juu, Julius Ottu na kumpiga ngumi usoni.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa kanuni ya 47:1 kuhusu Udhibiti kwa Klabu.

Mechi Namba 41A: Nyumbu FC 1-1 Moro Kids

Timu ya Moro Kids ya Mkoani Morogoro imepewa onyo kali kwa kosa la kuchelewa kufika kwenye uwanja wa mchezo Filbert Bayi Mkoani Pwani. Moro Kids ilifika saa 8:35 badala ya saa 8:30 mchana kinyume na matakwa ya kanuni ya 17:15 ya First League kuhusu Taratibu za Mchezo

Adhabu hii ni kwa mujibu wa Kanuni ya 17:62 ya First League kuhusu Taratibu za Mchezo.

Mechi Namba 43A: Magnet FC 0-2 Bandari Tanzania

Klabu ya Magnet ya mkoani Dar es Salaam imetozwa faini ya Sh. 2,000,000 (milioni mbili) kwa kosa la maofisa wake kushindwa kuhudhuria kikao cha kitaalam cha maandalizi yamchezo (MCM) kinyume na matakwa ya Kanuni ya 17:2(2.2) ya First League kuhusu Taratibu za Mchezo.

Maofisa hao ilipofika muda wa kikao waligoma kushiriki kikao hicho kwa madai wanamsubiri mwenye timu afike ndipo washiriki kikao hicho, hata alipofika kiongozi huyo (Tuntufye Mwambusi) bado maofisa hao hawakushiriki kikao hicho kwa madai ya kutojibiwa barua yao waliyoiwasilisha Bodi ya Ligi Kuu Tanzania.

Adhabu hii ni kwa mujibu wa Kanuni ya 17:62 ya First League kuhusu Taratibu za Mchezo.

Mechi Namba 46A: Green Warriors 1-5 Magnet

Timu ya Magnet ya Mkoani Dar es Salaam imepewa onyo kali kwa kosa la kuchelewa kufika kwenye uwanja wa mchezo Filbert Bayi Mkoani Pwani. Magnet ilifika saa 8:35 badala ya saa 8:30 mchana kinyume na matakwa ya kanuni ya 17:15 ya First League kuhusu Taratibu za Mchezo

Adhabu hii ni kwa mujibu wa Kanuni ya 17:62 ya First League kuhusu Taratibu za Mchezo

Imetolewa na;

Idara ya Habari na Mawasiliano

Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB)

 

SINGIDA, FOUNTAIN, AZAM ZATAMBA LIGI KUU YA NBC.

LIGI Kuu ya NBC imeendelea kwa michezo iliyochezwa katika mikoa ya Arusha,Singida na Dar es salaam.

Katika dimba la Singida, timu ya Singida Black Stars waliwakaribisha Pamba Jiji katika mchezo uliokuwa na kasi na ushindani mkubwa ulioshuhudia wenyeji wakionyesha ubora wao kwa kupata ushindi wa 3-1.

Mabao mawili yaliwekwa kambani na Ndumumwe Mossi aliyefunga dakika ya 21 na kuongeza lingine dakika ya 53 huku Horso Malanga akijiunga kwenye orodha ya wafungaji kwa bao la dakika ya 70 na kuhakikisha Singida wanakusanya alama zote tatu.
Bao pekee la Pamba Jiji lilifungwa na Henry Lutonja dakika ya 90 ingawa haikutosha kuzuia ushindi wa Singida.

Wakati huo huo, katika Uwanja wa Sheikh Amri Abeid jijini Arusha, Fountain Gate walikuwa na kibarua kigumu dhidi ya Coastal Union walioanza mchezo kwa kasi wakiandika bao la mapema dakika ya 2 kupitia kwa Shiza Kichuya.

Hata hivyo, Fountain Gate walirudi na kusawazisha kupitia Chukwunonye Obasi dakika ya 14 kabla ya kuongeza la pili dakika ya 33 huku Henry David akifunga bao la tatu dakika ya 70 na kufanya matumaini ya ushindi kuwa makubwa kwa wenyeji.

Coastal Union hawakukata tamaa, wakipata bao la pili dakika za nyongeza (90+3) kupitia Meshack Mwamita, lakini juhudi zao hazikutosha kubadili ubao wa matokeo.

Katika Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Azam FC walikuwa wenyeji wa Namungo katika mchezo uliokuwa wa ushindani mkubwa huku timu zote zikionesha nidhamu ya hali ya juu.

Azam walifanikiwa kupata bao pekee la mchezo dakika ya 41 kwa njia ya penalti iliyofungwa kwa utulivu na Feisal Salum aliandika bao lake la kumi msimu huu lililodumu hadi mwisho na kuwapatia ushindi muhimu.

Kwa ujumla, michezo hiyo imeendelea kuonyesha ushindani mkubwa ndani ya ligi, huku timu zikionyesha nia ya kupambana hadi dakika ya mwisho kusaka alama tatu muhimu.

HAKUNA MBABE WA KARIAKOO MSIMU WA 2025/26.

 

LIGI Kuu ya NBC iliendelea jana kwa mchezo wa ‘Derby’ ya Kariakoo kati ya Simba na Yanga iliyochezwa Mej. Jenerali isamuhyo na kumalizika kwa sare ya kusisimua ya mabao 2-2, katika pambano lililovuta hisia za mashabiki wengi.

Simba walikuwa wa kwanza kupata bao kupitia kwa Libasse Gueye dakika ya tatu kwa pasi safi ya Clatous Chama ambaye dakika saba baadae aliiandikia Simba ‘chuma’ ya pili baada ya kupokea pasi kutoka kwa Elie Mpanzu.

Dakika ya 17 Prince Dube alirudisha matumaini kwa Yanga na kufanya mchezo huo kwenda mapumziko Simba ikiongoza 2-1.

Dakika tano baada ya kipindi cha pili kuanza nahodha wa Yanga Bakari Mwamnyeto alisawazisha na kurejesha matumaini ya wananchi.

Mchezo huo uliendelea kwa kasi kubwa huku kila timu ikitafuta bao la ushindi, lakini uimara wa safu za ulinzi na makipa ulihakikisha matokeo yanabaki kuwa sare ya 2-2.

hii imeendelea kuthibitisha ushindani mkubwa uliopo kwenye Kariakoo Derby huku kila upande ukionyesha ubora na mapambano makali hadi dakika ya mwisho.

Mchezaji wa Simba Claotus Chama alichaguliwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo baada ya kufunga bao moja na kutoa pasi moja ya bao.

NYASI ZA MIKOA MITATU ‘KUWAKA MOTO’ LIGI KUU YA NBC.

LIGI Kuu ya NBC inarejea leo baada ya mapumziko ya takribani siku 10 ambapo mzunguko wa 22 utaanza leo katika mikoa ya Arusha, Mbeya na Dar es Salaam.

Mchezo wa kwanza utakuwa mkoani Arusha ambapo Fountain Gate itaikaribisha timu ya Pamba Jiji katika uwanja wa Sheikhe Amri Kaluta majira ya saa 8:00 mchana.

Fountain Gate inashika nafasi ya 13 katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC ikiwa imecheza michezo 19 ushindi mitano, sare nne na kupoteza michezo 10 huku ikikusanya jumla ya alama 19.

Pamba Jiji ipo nafasi ya saba ikiwa imeshinda michezo sita, sare nane na kufungwa michezo mitano ndani ya michezo 19 ambayo timu hiyo imecheza huku ikikusanya alama 26.

Mchezo wa pili utakuwa majira ya saa kumi na robo ambapo Mbeya City itaikaribisha timu ya Mashujaa katika uwanja wa Sokoine.

Mbeya City ipo nafasi ya 14 Kwenye msimamo wa Ligi Kuu ikiwa imecheza michezo 19 kushinda michezo minne, sare tano na kufungwa michezo 10 huku ikiweka kibindoni alama 17.

Mashujaa ipo nafasi ya 11 kwenye msimamo wa Ligi Kuu ikiwa imecheza michezo 19 ushindi nne, sare tisa na kufungwa michezo sita huku ikikusanya alama 21.

Mchezo wa mwisho utakuwa majira ya saa kumi na mbili jioni ambapo timu ya JKT Tanzania itakuwa mwenyeji wa KMC katika uwanja wa KMC Complex.

JKT Tanzania ipo nafasi ya tano katika msimamo wa Ligi Kuu ikiwa imecheza michezo 19, ushindi saba,sare nane na kupoteza michezo minne .

KMC ipo nafasi ya 16 ikiwa imecheza michezo 19 ushindi miwili, sare tatu na kufungwa michezo 14.

WIKI YA MAAMUZI, KUTOKA NEW AMAAN HADI MEJ. JEN ISAMUHYO.

SAFARI inaanza Aprili 29, visiwani Zanzibar ambapo macho yote yataelekezwa kwenye Uwanja wa New Amaan Complex timu za Simba na Young Africans (Yanga) zitakapokutana katika fainali ya Kombe la Muungano kwenye mchezo wenye uzito wa kipekee unaobeba heshima ya kitaifa na hadhi ya ushindani wa kihistoria kati ya timu hizi mbili.

Fainali hii si tu pambano la kutwaa taji, bali ni kipimo cha nguvu, mbinu na utayari wa kila kikosi kuelekea mechi nyingine kubwa zaidi inayofuata ya Ligi Kuu ya NBC timu hizo zitakapokutana.

Ndani ya dakika 90 (au zaidi), mshindi atajipatia faida ya kisaikolojia itakayoweza kuathiri moja kwa moja matokeo ya Kariakoo derby ya Mei 3 kwenye uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, Dar es Salaam unaotumiwa na timu ya Simba.

Kabla ya Kariakoo Derby ya Mei 3 ndani ya Dar es Salaam, hali ya msimamo wa Ligi Kuu ya NBC inaipa hadithi hii uzito wa kipekee kuelekea mchezo huo ambapo Yanga wanaongoza wakiwa na rekodi ya kuvutia.

‘Wananchi’ wamecheza michezo 19 bila kupoteza wakishinda 14, sare tano, mabao 44 ya kufunga na mabao matatu tu ya kufungwa huku ikikusanya alama 47 hadi sasa.

Kwa upande wa ‘Mnyama’ ameshinda 12, sare sita, ‘kichapo’ kimoja dhidi ya Azam, mabao 32 ya kufunga na saba ya kuruhusu huku ikikusanya jumla ya alama 42 hadi sasa.

Takwimu hizi zinaonyesha tofauti ndogo sana kwa ‘miamba’ hii inayotikisa Ligi Kuu ya NBC msimu huu huku Yanga wakionekana kuwa na uimara mkubwa hasa kwenye safu ya ulinzi na Simba wakibaki kuwa tishio lenye uwezo wa kubadilisha mchezo kwa haraka kwenye safu yao ya ushambuliaji inayoongozwa na Selemani Mwalimu.

Katika upande wa ushambuliaji, Yanga wanaonekana kuwa na mgawanyo mpana wa mabao, hali inayowafanya kuwa vigumu kuzuilika huku wachezaji wao Prince Dube raia wa Zimbabwe akifunga mabao nane, Pacome Zouzoua wa Ivory Coast akifunga saba na Mudathir Yahya raia wa Tanzania akifunga saba huku akitarajiwa kukosa mchezo huo wa jumapili kutokana na adhabu aliyopewa ya kufungiwa baada ya kumpiga kiwiko mchezaji wa Pamba Jiji Ibrahim Abraham.

Kwa upande wa ‘Mnyama’ mchezaji wa Wydad Casablanca ya Morocco raia wa Tanzania anayekipiga kwenye timu hiyo kwa mkopo Selemani Mwalimu hadi sasa amefunga mabao 6 huku Libasse Gueye wa Senegal akifunga manne akiwa na mchango mkubwa kwenye safu ya ushambuliaji ya Simba hadi sasa sambamba na Anicet Oura wa Ivory Coast aliyesajiliwa dirisha dogo la msimu huu.

Hii inaonyesha tofauti ya kimkakati ambapo Yanga wakitegemea mfumo wa timu nzima kushambulia, huku Simba wakitumia ufanisi na nidhamu ya kiufundi kupata matokeo ya ushindi.

Kwa miaka ya hivi karibuni, rekodi ya Kariakoo Derby imekuwa na ushindani mkali, lakini takwimu zinaipa Yanga nafasi ya kujiamini zaidi kutokana na mfululizo wa matokeo mazuri wanayopata wakikutana na wapinzani wao hao wa Kariakoo.

Hata hivyo, derby ina tabia ya kuvunja hesabu zote ndani ya dakika 90 ambapo historia inaweza kufutwa na kuandikwa upya kutokana na maandalizi na ufanisi wa kutumia nafasi kwa timu zote mbili.

Kinachofanya ratiba hii kuwa ya kipekee si tu ukubwa wa mechi, bali ukaribu wake kwani fainali ya Muungano inakuja siku chache kabla ya dabi ya Kariakoo ya Ligi Kuu ya NBC hali inayobadilisha kabisa maandalizi ya timu zote mbili.

Mshindi wa Zanzibar ataingia kwenye mchezo wa Ligi Kuu ya NBC akiwa na morali ya juu na ataweka presha kwa mpinzani kuelekea mchezo wa ligi huku anayeshindwa ataingia na hasira na atajaribu kulipiza kisasi hali inayofanya kuongeza joto la michezo hiyo hivyo basi mechi hizi mbili si matukio tofauti bali ni sura mbili za simulizi moja.

Kutoka visiwa vya Zanzibar hadi mitaa ya Kariakoo, Tanzania inajiandaa kushuhudia burudani ya kiwango cha juu, presha isiyo na mfano na historia mpya ikiandikwa kwa michezo miwili ya Kariakoo Derby kupigwa ndani ya wiki moja.

Swali linabaki kuwa moja tu:
Nani ataibuka kuwa mfalme wa wiki hii kati ya Simba au Yanga?