Category: STORY

GEITA GOLD HAISHIKIKI, LIGI YA CHAMPIONSHIP YA NBC IKIPAMBA MOTO.

LIGI ya Championship ya NBC msimu wa 2025/26 imezidi kupamba moto huku ushindani ukiwa mkali katika kila kona ya msimamo, wakati mzunguko wa 22 ukielekea kufungwa rasmi.

Vinara Geita Gold wameendelea kuthibitisha ubora wao baada ya kuichapa Hausung mabao 6-1 katika mchezo uliopigwa Uwanja wa Nyankumbu mkoani Geita huku ushindi huo wa kishindo ukiifanya Geita Gold kufikisha alama 55 baada ya michezo 22, wakizidi kujikita kileleni.

Wanaowafuatia kwa karibu ni majirani zao wa Kagera Sugar ambao hawakuachwa nyuma baada ya kupata ushindi muhimu wa mabao 2-0 dhidi ya B19 wakifikisha alama 52 na kuendelea kuweka presha kwa vinara Geita.

Katika mchezo mwingine, Mbeya Kwanza waliendeleza ubora wao wakiwa ugenini kwa kuichapa Kengold mabao 4-1 kwenye Uwanja wa Halmashauri ya Chunya, ushindi unaoifanya Mbeya Kwanza kujikita katika nafasi ya tatu kwa alama 48 wakiendelea kusalia kwenye mbio za kupanda daraja.

Nayo Polisi Tanzania ilionyesha uthabiti baada ya kuibuka na ushindi mgumu wa mabao 2-1 dhidi ya Transit Camp, ushindi uliowapandisha hadi nafasi ya nne wakifikisha alama 45.

Msimamo wa ligi kwa sasa unaonyesha vita kali, ambapo timu tano za juu zinaendelea kuwania nafasi za kupanda daraja moja kwa moja au kushiriki michezo ya mtoano (playoffs) huku Kila alama ikiwa na thamani ya dhahabu kadri ligi inavyoingia hatua za mwisho.

Hata hivyo, hali ni ya wasiwasi kwa timu za chini ya msimamo, Hausung na Barberian wanaoshika nafasi ya 15 na 16 wapo kwenye hatari kubwa ya kushuka daraja iwapo hawatabadilisha mwenendo wao haraka.

Mzunguko wa 22 unatarajiwa kukamilika leo kwa pambano kati ya Gunners na Mbuni litakalopigwa Uwanja wa Jamhuri, mkoani Morogoro kuanzia saa 10:00 jioni.

SIMBA YAICHAPA NAMUNGO LIGI KUU YA NBC.

LIGI Kuu ya NBC imeendelea kwa mchezo mmoja ambapo Namungo walikuwa wenyeji wakiikaribisha Simba katika mchezo uliochezwa majira ya saa kumi jioni katika uwanja wa Majaliwa mkoani Lindi.

Mchezo huo ulimalizika kwa Simba kupata ushidi wa mabao 3-1 huku wakionyesha ubora wao hasa katika kipindi cha kwanza walipofanikiwa kupata bao la mapema kupitia kwa Libasse Gueye dakika ya 12 kabla ya kuongeza bao la pili kupitia kwa Anicet Oura dakika ya 25.

Namungo walijaribu kurejea mchezoni na kufanikiwa kupata bao lao dakika ya 33 kupitia Haritier Makambo aliyefunga kwa mkwaju wa penati lakini juhudi zao hazikutosha kuizuia timu ya Simba.

Kipindi cha pili Simba waliendelea kuwa hodari kwenye mchezo huo mbele ya mashabiki wao wa mkoa wa Lindi na kuongeza bao la tatu dakika ya 74 kupitia Elie Mpanzu aliyehitimisha ushindi huo Muhimu kwa ‘Mnyama’.

Ushindi huo unaifanya Simba kuwa na alama 42 ikishika nafasi ya pili huku Namungo wakiwa nafasi ya 10 na alama 22.

Katika mchezo huo winga wa Simba Anicet Oura alichaguliwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo.

 

SIMBA, COASTAL ZAGAWA ‘DOZI’ LIGI KUU YA NBC.

LIGI Kuu ya NBC imeendelea kwa michezo iliyochezwa katika mikoa miwili tofauti ambapo Simba ilikuwa ugenini dhidi ya Fountain gate mchezo uliochezwa uwanja wa Sheikh Abeid mkoani Arusha na ‘Mnyama’ kusibuka na ushindi wa mabao 3-0.

Simba walidhibiti mchezo kuanzia mwanzo hadi mwisho wakionyesha ubora mkubwa wa kushambulia na bao la kwanza lilifungwa mwishoni mwa kipindi cha kwanza na Clatous Chama ambaye aliwapa Simba mwanzo mzuri.

Kipindi cha pili kilianza kwa kasi Libase Gueye akiongeza bao la pili dakika ya 53 akitumia vizuri pasi ya Selemani Mwalimu.

Bao la tatu kilifungwa dakika ya 71 kwa mchezaji wa Fountain Gate Shaban Mgunda kujifunga baada ya kushindwa kuokoa krosi iliyopigwa na Elie Mpanzu.

Ushindi huu unaimarisha nafasi ya Simba katika msimamo wa ligi kuu wakiwa nafasi ya Pili na alama 39 huku Fountain Gate wakiendelea kupambana kujinasua katika eneo hatari wakiwa nafasi 14 baada ya kukusanya alama 16.

Mchezo wa Pili Coastal union iliibuka na ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya Dodoma jiji kwenye uwanja wa Mkwakwani, Tanga.

Coastal union ilifungua ukurasa wa mabao dakika ya 15 kupitia kwa Greyson Gwalala kwa shuti kali kabla ya Maabad Maulid kuongeza bao la pili dakika ya 32 na kuwapa wenyeji uongozi mzuri wa 2-0 kipindi cha kwanza.

Kipindi cha pili kilishuhudia ushindani ukiendelea huku Dodoma jiji wakijitahidi kurejea mchezoni na matumaini yalirejea baada ya kupata bao dakika ya 90+1 kupitia kwa Waziri Junior ambalo lilidumu kwa dakika tatu pekee kabla ya Geofrey Manyac kuzima matumaini ya Dodoma kusawazisha bao kwa kuandika la tatu kwa Coastal.

Ushindi huo unaifanya Coastal union kufikisha alama 19 wakikwea hadi nafasi ya 12 huku Dodoma wakisalia na alama 24 kwenye nafasi ya nane.

MASHUJAA, SINGIDA ‘KUKINUKISHA’, YOUNG AFRICANS, MBEYA CITY VITA YA ALAMA TATU LIGI KUU YA NBC.

LIGI Kuu ya NBC inaendelea leo katika mikoa ya Kigoma na Dar es Salaam ambapo timu ya Mashujaa itaikaribisha timu ya Singida Black Stars katika uwanja wa Lake Tanganyika, Kigoma huku Young Africa ikiikabili Mbeya City katika uwanja wa KMC Complex, Dar.

Mchezo wa kwanza utaanza majira ya saa 10:00 alasiri kwa Mashujaa kuikaribisha timu ya Singida Black Stars mchezo huo ukiwa ni muhimu kwa timu hizo ili kufikia malengo waliyojiwekea ya kubeba ubingwa wa Ligi Kuu ya NBC.

Mashujaa ipo nafasi ya 11 kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC ikiwa imecheza michezo 18 ikishinda michezo minne, sare nane na kufungwa michezo sita huku ikifanikiwa kukusanya alama 20.

Wachezaji wa Singida

Singida ipo nafasi ya tano kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC ikicheza michezo 18 kushinda michezo 8 sare nne na kufungwa michezo sita huku ikikukusanya alama 28.

Kwa upande wa mchezo wa Young Africans na Mbeya City utachezwa majira ya saa 12:30 jioni ikiwa ni mchezo utakaokuwa na upinzani mkali baada ya timu hizo kutoka sare kwenye mchezo wao wa mzunguko wa kwanza.

Wachezaji wa timu ya Young Africans.

Young Africans ipo nafasi ya kwanza kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC ikicheza michezo 18 ushindi 13 na sare tano ikiwa ni moja ya timu ambazo hazijapoteza mchezo wowote sawa na Azam huku ikiweza kukusanya alama 44.

Wachezaji wa Mbeya City.

Mbeya City ipo nafasi ya 13 katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC ikiwa imecheza michezo 18, ikishinda michezo minne, sare tano na kufungwa michezo tisa huku ikiweza kukusanya alama 17.

HAKUNA MBABE KMC COMPLEX LIGI KUU YA NBC.

 

LIGI Kuu ya NBC imeendelea kwa mchezo uliochezwa uwanja wa KMC majira ya saa Moja jioni Mkoani Dar es Salam uliozikutanisha KMC dhidi ya Tanzania Prisons na kumalizika
kwa Sare ya bao 1-1.

Kipindi cha kwanza kilianza kwa kasi huku Tanzania Prisons wakitangulia kupata bao la mapema dakika ya tano kupitia kwa Jeremiah Juma.

Hata hivyo KMC walirejea mchezoni dakika ya 38 baada ya Adam Uledi kusawazisha kwa shuti lililowapa matumaini mashabiki wao.

Kipindi cha Pili kilikuwa na ushindani mkali kutoka pande zote mbili,kila timu ikitafuta bao la ushindi lakini safu za ulinzi zilisimama imara kuzuia mashambulizi ya timu pinzani.

Matokeo haya yanaacha hali ngumu kwa timu zote mbili katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC, KMC ikiongeza alama moja muhimu lakini bado haitoshi kuwatoa kwenye presha ya kushuka daraja wakiwa nafasi ya 16 na alama tisa huku wakihitaji ushindi katika michezo ijayo ili kujiweka salama.

Tanzania Prinsons nao wapo kwenye nafasi mbaya kwenye nafasi ya 15 baada ya kukusanya alama 14 katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC.

Kwa matokeo hayo hakuna timu ambayo ipo salama na vita ya kuepuka kushuka daraja inaendelea kuwa kali kadri msimu unavyoelekea ukingoni huku michezo iliyosalia ikiwa na umuhimu mkubwa kwa timu hizo.