Category: STORY

PAMBA JIJI YAONJA RAHA YA USHINDI, SIMBA, KMC HAPATOSHI LEO.

Ligi Kuu ya NBC jana iliendelea kwa mchezo mmoja uliochezwa katika Uwanja wa Tanzanite Kwaraa mkoani Manyara ambapo Fountain Gate waliwakaribisha timu ya Pamba Jiji kutoka Mwanza.

Iliwachukua dakika 28 Fountain Gate kufungua ukurasa wa mabao kupitia mchezaji wake Ellie Makono ambapo dakika ya 34 Pamba Jiji waliweka mzani sawa kwa kupata bao kupitia mchezaji wake James Mwashinga kabla ya kuongeza bao la pili katika dakika ya 45 ya mchezo huo kupitia mchezaji Salehe Masoud hivyo kwenda mapumziko wakiwa wanaongoza.

Kipindi cha pili kilianza kwa timu zote kushambuliana na dakika ya 85 ya mchezo huo mchezaji Ally Ramadhan aliiongezea Pamba Jiji bao la 3 hivyo kuifanya timu hiyo kupata ushindi wao wa kwanza tangu kupanda Ligi kuu ya NBC huku wakiwa wamecheza michezo 11.

Ligi Kuu ya NBC itaendelea leo mkoani Dar es Salaam ambapo timu ya Simba itakuwa mwenyeji wa KMC katika Uwanja wa KMC Complex, uliopo Mwenge majira ya alasiri.

KARIA AZITAKA KLABU LIGI KUU KUTOKA NA AZIMIO MOJA

Rais wa Shirikisho la Soka nchini (TFF), Wallace Karia amezitaka klabu za Ligi Kuu ya NBC kutoka na azimio moja mara baada ya mafunzo ya Weledi katika Uendeshaji wa klabu nchini kwa Watendaji Wakuu na Wenyeviti wa Klabu.

Akizungumza wakati wa kufunga mafunzo hayo Karia amesema kuwa Klabu zinapaswa kuwa na azimio moja kwa ajili ya ustawi wa soka letu hususani kwa upande wa matangazo wanayopata klabu.

“Ligi yetu imekua sana tunapaswa tuwe na azimio moja mfano kuhusu matangazo yanayoonekana wakati wa mechi zetu yanapaswa kuzinufaisha klabu zetu na sio wale wanaoandaa mabango hayo”alisema Karia na kuongeza,

“FIFA wameleta mafunzo haya kwa wakati muafaka nawashukuru sana natazamia kukaa na Bodi ya Ligi Kuu ili kuona namna ya kuongeza uwepo wa mafunzo kama haya kwa manufaa ya taifa letu na vizazi vijavyo vya soka hususani katika masuala ya utawala bora katika klabu za soka” alisema Karia.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Ligi, Steven Mnguto amewashukuru FIFA kwa mafunzo waliyopata kwani klabu nyingi zitanufaika na ujuzi waliopata.

“Nawashukuru sana FIFA sisi kama Klabu za Tanzania tumenufaika kwa hizi siku mbili na tunatamani tupate muda mwingi zaidi kuwa nanyi” alisema Mnguto.

Mafunzo hayo ya siku mbili yaliyoandaliwa na FIFA wakishirikiana na TFF na Bodi ya Ligi yamefanyika Dar es Salaam katika hoteli ya Johari Rotana.

MTINE, POPAT WAFUNGUKA SEMINA YA FIFA UENDESHAJI KLABU NCHINI.

Watendaji Wakuu wa Klabu za Yanga na Azam wameshukuru Shirikisho la Soka Duniani (FIFA) wakishirikiana na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) Pamoja na Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) kwa kuandaa semina ya siku mbili jijini Dar es salaam kuhusu Weledi katika Uendeshaji wa klabu nchini kwa Watendaji Wakuu na Wenyeviti wa Klabu zinazoshiriki Ligi Kuu ya NBC.

Akizungumza katika semina hiyo Mtendaji Mkuu wa Yanga Andre Mtine amesema kuwa semina hii ni muhimu kwani elimu haina mwisho na itawezesha viongozi wa klabu kutambua namna nzuri ya kuendesha klabu.

“Elimu ni jambo la muhimu kwa kila mtu na haina mwisho iwe kijana ama mzee bado anapaswa kujifunza hii ni nzuri kwetu kwani tunajifunza namna ya kuendesha klabu zetu kwa manufaa ya Ligi yetu ya NBC” Alisema Mtine.

Kwa upande waka Mtendaji Mkuu wa Azam Abdulkarim Amin ‘Popat’ amesema kuwa anashukuru kwa kupata fursa hii adimu kutoka FIFA wakishirikiana na TFF Pamoja na Bodi ya Ligi kwani itawajengea ujuzi na uzoefu mpya kwenye tasnia ya mpira.

“Nashukuru FIFA, TFF na Bodi ya Ligi kwa kuja na semina hii kwani ni fursa adimu naamini itatujengea uwezo na kutupa ujuzi mpya sisi kama watendaji wakuu wa klabu za Ligi Kuu ya NBC na kama Azam tunaahidi kwenda kufanyia kazi tulichojifunza na tutaenda kuwafundisha waliopo chini yetu ili nao wanufaike na haya”alisema Popat.

KARIA AFUNGUA SEMINA YA FIFA KUHUSU WELEDI KATIKA UENDESHAJI KLABU NCHINI.

Rais wa Shirikisho la Soka nchini (TFF), Wallace Karia amefungua semina ya siku mbili iliyoandaliwa na Shirikisho la Soka Duniani (FIFA) jijini Dar es salaam kuhusu weledi katika uendeshaji wa klabu nchini kwa wenyeviti na watendaji wakuu.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa semina hiyo Karia amewashukuru timu ya FIFA chini ya Mkuu wa Maendeleo ya Programu wa FIFA, Solomon Mudege kwa kuweka semina hii kwa wenyeviti na watendaji wakuu wa klabu za Ligi Kuu ya NBC.

Karia amesema kuwa uanzishwaji wa program hii kwa klabu hususani namna klabu zitakavyofanya biashara ya mpira kiueledi zaidi na pia wakati wa program hii wataelewa namna ya kushughulikia mipango mikakati ya klabu zao.

Aidha Karia amesema kuwa kama unataka klabu yako kuwa sahihi ndani nje ya uwanja unapaswa kuwa na mpango mkakati maalumu.

Programu hii itazisaidia klabu kubadilisha mtazamo katika kila Nyanja ili kwenda na wakati.

“Naamini baada ya programu hii klabu zetu zitabadili mtazamo kwa upande wa uongozi na mtafanya mambo yote kwa ufanisi mkuu nami sina budi kumshukuru Rais wa FIFA, Gianni Infantino kwa programu hii inayokidhi mazingira yetu ya kiafrika na tunatamani ziwepo nyingi zaidi” amesema Karia.

Karia amemaliza kwa kutoa nukuu maarufu isemayo kuwa malengo bila mpango ni sawa na matamanio hivyo amewaomba washiriki wa program hii kuweza kuwafundisha wenzao katika klabu ili hata kama ikitokea wameondoka wawepo watu kuendeleza mipango mikakati iliyowekwa na klabu.

AZAM YATAMBA UGENINI ,SINGIDA, COASTAL HAKUNA MBABE

Ligi Kuu ya NBC jana iliendelea kwa michezo miwili iliyochezwa jijini Dar es Salaam katika Uwanja wa Azam Complex na Uwanja wa Amaan Complex visiwani Zanzibar.

Timu ya Yanga ilikuwa mwenyeji wa Azam katika mchezo maarufu kama ‘dabi ya Dar es Salaam’ na kupoteza kwa bao moja huku beki wa Yanga Ibrahim Bacca akishindwa kumaliza mchezo baada ya kuonyeshwa kadi nyekundu baada ya kumfanyia rafu mshambuliaji wa Azam Nassoro Saadun.

Gibril Sillah ndiye aliyefunga bao pekee dakika ya 34 ya mchezo huo uliokuwa na upinzani mkali kwani timu zote zilikuwa zikishambuliana muda wote.

Mchezo wa pili uliochezwa saa mbili na nusu usiku mjini Zanzibar Singida Black Star walishindwa kutamba mbele ya timu ya Coastal Union baada ya kulazimishwa suluhu.

Ligi Kuu ya NBC leo itaendelea jijini Mbeya ambapo Tanzania Prisons watawakaribisha KenGold katika Uwanja wa Sokoine saa 10 alasiri.