Category: STORY

AFRICAN SPORTS BINGWA FIRST LEAGUE 2023/24.

TIMU ya African Sports ya Tanga imefanikiwa kuwa bingwa wa Ligi ya First League msimu wa 2023/24 baada ya kuifunga Kiluvya ya Dar es Salaam bao 1-0.

African Sports imefanikiwa kutwaa ubingwa huo bila kupoteza mchezo wowote katika mashindano ya First League Nane Bora yaliyofanyika Tanga kwenye uwanja wa Mkwakwani.

African Sports imefanikiwa kupanda daraja hadi Ligi ya Championship ya NBC baada ya kushuka msimu uliopita kwa kupoteza mchezo wa mtoano dhidi ya TMA ya Arusha.

Timu ya Kiluvya iliyopoteza fainali imefanikiwa kuibuka mshindi wa pili na kupanda Ligi ya Championship ya NBC msimu wa 2024/25.

Timu za Malimao iliyoibuka mshindi wa tatu na Mwadui iliyokuwa mshindi wa nne zitacheza michezo ya mtoano na timu zilizopoteza michezo yake ya mtoano kwenye ligi ya Championship ya NBC ili kutafuta nafasi ya kucheza ligi ya Championship ya NBC msimu wa 2024/25.

KILUVYA, AFRICAN SPORTS ZATINGA FAINALI YA FIRST LEAGUE NANE BORA.

TIMU za Kiluvya ya Dar es Salaam na African Sports ya Tanga zimefanikiwa kutinga fainali ya mashindano ya First League Nane Bora baada ya kushinda michezo yao ya nusu fainali.

Kiluvya iliyocheza dhidi ya Malimao ya Dar es Salaam imeshinda kwa mikwaju ya penati 4-2 baada ya kutoka suluhu katika dakika 120.

African Sports ilishinda mabao 2-1 dhidi ya Mwadui ya Shinyanga kwenye mchezo ulioshuhudia Mwadui wakionyeshwa kadi mbili nyekundu huku moja ikionyeshwa baada ya vurugu zilizotokea uwanjani dakika chache kabla ya mchezo kumalizika.

Matokeo hayo yanazifanya timu za Kiluvya na African Sports kufuzu moja kwa moja kucheza Ligi ya Championship ya NBC msimu wa 2024/25 huku fainali ya mashindano hayo ikitarajiwa kupigwa Mei 11, kwenye uwanja wa Mkwakwani ili kupata bingwa wa First League msimu wa 2023/24.

Timu za Mwadui na Malimao zitacheza mchezo wa kutafuta mshindi wa tatu Mei 11 huku pia zikiwa na nafasi ya kupanda daraja msimu ujao ikiwa zitashinda michezo ya mtoano dhidi ya timu za Ligi ya Championship zitakazofungwa michezo ya mtoano.

MZIZIMA ‘DERBY’ KUISIMAMISHA DAR ES SALAAM LEO.

 

MCHEZO wa Ligi Kuu ya NBC ‘Derby’ ya Mzizima unapigwa leo kwenye uwanja wa Benjamin Mkapa saa 12:15 jioni kati ya Azam na Simba.

Mchezo huu unabeba hisia za watu wengi kutokana na nafasi za kila timu kwenye msimamo huku ukiwa ni mchezo wa hatma za timu hizi kwenye nafasi ya kuendelea kupambania ubingwa.

Mchezo wa Mzunguko wa kwanza Simba dhidi ya Azam ulimalizika kwa Sare ya bao 1, bao la Azam likifungwa na Prince Dube huku lile la Simba likifungwa na Clatous Chama.

Kwenye msimamo Azam ipo nafasi ya Pili ikiwa na alama 57 baada ya michezo 25 huku Simba ikiwa nafasi ya Tatu ikiwa na alama 53 kwenye michezo 24 pungufu ya mchezo mmoja nyuma ya Azam.

FIRST LEAGUE NANE BORA KUANZA KUTIMUA VUMBI LEO.

 

MICHUANO ya First League hatua ya Nane Bora inaanza kutimua vumbi leo Mei 2 mkoani Tanga ikishirikisha jumla ya timu nane kutoka mikoa tofauti.

Mchezo wa ufunguzi utazikutanisha African Sports ya Tanga dhidi ya Malimao ya Dar es salaam saa 8:00 mchana katika uwanja wa CCM Mkwakwani ikifuatiwa na mchezo wa saa 10:00 alasiri kati ya Rhino Rangers na Nyumbu.

Timu shiriki ni Nyumbu ya Pwani, African Sports ya Tanga, Kiluvya na Malimao za Dar, Mapinduzi ya Mwanza, Rhino Rangers ya Tabora, Tanesco ya Kilimanjaro na Mwadui ya Shinyanga ambazo zimegawanya kwenye makundi mawili, ya A na B.

Timu mbili za juu kutoka kila kundi zitafuzu moja kwa moja hatua ya nusu fainali huku timu zitakazoingia fainali zitakata tiketi ya kushiriki Ligi ya NBC Championship msimu ujao wa 2024/2025.

Timu mbili zitakazopoteza hatua ya Nusu fainali zinayo nafasi ya kupanda Ligi ya NBC Championship kwa kucheza michezo ya mchujo na timu zilizopoteza mchezo wa mchujo wa Kubaki Ligi ya NBC Championship na mshindi wa jumla kushiriki Ligi ya NBC Championship msimu ujao wa 2024/2025.

KENGOLD BINGWA NBC CHAMPIONSHIP 2023/2024, PAMBA KARIBU LIGI KUU YA NBC.

 

MSIMU wa 2023/2024 Ligi ya NBC Championship umemalizika rasmi kwa KenGold kutawazwa mabingwa wa Ligi hiyo ikifikisha jumla ya alama 70 kwenye michezo 30 ikishinda 21, ikipata sare michezo 7 na kufungwa michezo 2.

Pamba FC imefanikiwa kupanda Ligi Kuu ya NBC moja kwa moja baada ya kushinda mchezo wa leo na kufikisha jumla ya alama 67 ambazo haziwezi fikiwa na timu yeyote inayomfuatia.

Mbeya kwanza na Biashara United watacheza hatua ya mtoano kutafuta timu moja kutoka Ligi ya NBC Championship itakayocheza hatua ya mtoano na timu moja toka Ligi Kuu ya NBC na mshindi wa Jumla kushiriki Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2024/2025.

Timu kutoka Ligi Kuu ya NBC itakayocheza hatua ya mtoano dhidi ya timu ya Ligi ya NBC Championship ni timu itakayopoteza mchezo wa mtoano kati ya timu iliyoshika nafasi ya 13 na 14 ndani ya Ligi Kuu ya NBC.

Timu za Pan African ya Dar es salaam na Ruvu Shooting ya Iringa zimeshuka daraja moja kwa moja na mwakani zitashiriki First League msimu wa 2024/2025.