LIGI Kuu ya NBC inatarajiwa kutimua vumbi leo Mei 5, kwa mchezo mmoja kati ya JKT Tanzania na Simba utakaopigwa kwenye uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, Dar es Salaam huku uwanja huo ukiwa sehemu ngumu kupata matokeo ya ushindi kwa timu kubwa za Ligi Kuu ya NBC.
JKT yenye ‘maskani’ yake Mbweni, Dar es Salaam imecheza uwanja wake wa nyumbani dhidi ya Young Africans na Azam bila kupoteza mchezo kwenye msimu huu wa 2024/25.
Michezo yote miwili dhidi ya timu hizo JKT haijaruhusu bao lolote kwani michezo hiyo ilimalizika kwa suluhu huku golikipa wa timu hiyo Yakoub Suleiman akimaliza michezo hiyo kwa kukusanya (hati safi) mbili.
JKT leo itakuwa mwenyeji wa ‘Kigogo’ mwingine wa Ligi Kuu ya NBC aliyefanikiwa kufuzu fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika timu ya Simba kwenye uwanja huo wa Meja Jenerali Isamuhyo katika mchezo utakaopigwa saa 10:00 alasiri.