Author: Honest Mwanitega

DAR ES SALAAM NI KIJANI NA NJANO LIGI KUU YA NBC.

LIGI Kuu ya NBC imeendelea Aprili 20 kwa mchezo wa ‘Kariakoo Derby’ uliopigwa uwanja wa Benjamin Mkapa na kumalizika kwa Yanga kuibuka washindi kwa mabao 2-1 dhidi ya Simba.

Yanga imeshinda michezo yote ya Ligi Kuu ya NBC iliyokutana na mtani wake Simba msimu huu wa 2023/24 baada ya mzunguko wa kwanza kupata ushindi mnono wa mabao 5-1 ugenini.

Mabao ya Stephane Aziz Ki aliyefunga kwa mkwaju wa penati na Joseph Guede yametosha kuipa Yanga ushindi huo huku bao pekee la Simba likifungwa na Fred Michael Koublan.

Matokeo hayo yanaifanya Yanga kuwa mbele ya Simba kwa tofauti ya alama 12 huku Simba ikiwa na mchezo mmoja mkononi.

Ligi hiyo itaendelea leo kwa michezo mitatu ambapo mchezo wa mapema timu ya Tabora United itakuwa mwenyeji wa Geita Gold saa 8:00 mchana, saa 10:00 alasiri Singida Fountain Gate itaialika Mashujaa kwenye uwanja wa CCM Kirumba na mchezo wa mwisho utakuwa kati ya Azam FC na Ihefu kwenye uwanja wa Azam Complex.

‘STAA’ YUPI WA LIGI KUU YA NBC KUMFUATA INONGA ROBO FAINALI LEO ?

KOMBE la Mataifa ya Afrika linaendelea nchini Ivory Coast huku ‘Mastaa’ watatu wa Ligi Kuu ya NBC wakisalia hadi sasa kwenye mashindano hayo.

Mashindano hayo yanaendelea leo huku wachezaji wawili wa Yanga Djigui Diarra anaekipiga timu ya taifa ya Mali na Stephane Aziz Ki wa Burkina Faso wakikutana leo kila mmoja akitafuta nafasi ya kucheza robo fainali.

Tayari ‘staa’ mmoja wa Ligi Kuu ya NBC Henock Inonga anaecheza timu ya Simba ameshafuzu hatua ya robo fainali kwenye mashindano yake na timu ya Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Congo baada ya kuitoa timu ya Misri.

Mshindi wa mchezo wa leo kati ya Diarra na Ki Aziz ndiye atasalia kwenye mashindano hayo na atakayepoteza atarejea nchini kuitumikia timu yake kwenye michezo ya Ligi Kuu ya NBC inayotarajiwa kurejea Februari 2 kwa mchezo kati ya Kagera Sugar dhidi ya Yanga.

LIGI KUU YA NBC KUREJEA FEBRUARI 2.

BAADA ya kusimama kwa takribani siku 40 kupisha mashindano ya Mataifa ya Afrika yanayoendelea nchini Ivory Coast Ligi Kuu ya NBC inarejea tena Februari 2.

Ligi hiyo itarejea kwa mchezo mmoja utakaopigwa saa 10:00 alasiri kwenye uwanja wa Kaitaba mkoani Kagera kati ya Kagera Sugar na Yanga.

Ligi hiyo namba sita kwa ubora Afrika inarejea baada ya timu ya taifa ya Tanzania kushindwa kufuzu kwenye hatua ya 16 bora na kutolewa kwenye mashindano ya Mataifa ya Afrika.

Ni ‘Mastaa’ watatu pekee waliosalia kwenye mashindano hayo hadi sasa ambao ni Henock Inonga wa timu ya Simba, Stephane Aziz Ki wa Yanga na Djigui Diarra wa Yanga hivyo kuruhusu ligi hiyo kuendelea kwa mujibu wa kanuni.

BIASHARA YAISHUSHA PAMBA, POLISI, TRANSIT HAKUNA MBABE LIGI YA NBC CHAMPIONSHIP.

TIMU ya Bishara United ya Mara imeiduwaza Pamba ya Mwanza baada ya kuifunga bao 1-0 kwenye mchezo uliopigwa uwanja wa Mwadui, Shinyanga.

Pamba iliyokuwa mwenyeji wa mchezo huo imeruhusu bao la dakika ya 87 lililofungwa na Ramadhan Kipalamoto na kuifanya timu hiyo kushuka kutoka nafasi ya pili mpaka ya tatu na kuipisha Biashara iliyokaa nafasi ya pili kwa tofauti ya mabao ya kufunga.

Mkoani Kilimanjaro timu ya Polisi Tanzania imeshindwa kutamba baada ya kulazishwa sare ya bao moja dhidi ya timu ya Transit Camp ya mkoani Dar es Salaam.

Polisi inakwea hadi nafasi ya nane ikiwa na alama 26 huku Transit ikisalia nafasi ya 13 baada ya kufikisha alama 16.

Ken Gold ya Mbeya inaendelea kushika nafasi ya kwanza ikiwa na alama 43 huku Ruvu Shooting ya Pwani ikisalia nafasi ya 16 na alama tatu ikiwa haijashinda mchezo wowote msimu huu.

LIGI KUU YA NBC NAMBA SITA KWA UBORA AFRIKA.

SHIRIKISHO la Kimataifa la Historia na Takwimu za Mpira wa Miguu (IFFHS) limetoa takwimu za Ligi bora duniani huku Ligi Kuu ya NBC Tanzania ikishika namba 6 barani Afrika.

Shirikisho hilo limetoa takwimu za ligi 100 ikijumuisha Bara la Afrika, Ulaya, Amerika ya Kusini, Amerika Kaskazini, Asia, Australia na Antaktiki huku Ligi Kuu ya NBC ikishika nafasi ya 62 Duniani.

Ligi Kuu ya NBC iliyokuwa nafasi ya tano mwaka jana imeshuka kwa nafasi moja mwaka huu barani Afrika ikiwa nyuma ya Misri, Morocco, Algeria, Tunisia na Afrika ya Kusini.