Author: Loveness Bernard

LIGI KUU YA NBC KUREJEA LEO.

LIGI Kuu ya NBC inarejea leo baada ya mapumziko ya michezo ya kalenda ya Fifa ambapo timu ya Singida Black Stars itaikaribisha timu ya Azam katika uwanja wa Airtel mkoani Singida saa 10:00 alasiri.

Mchezo huo ni muhimu kwa timu zote kwani zinatafuta alama tatu muhimu ili kujiweka katika nafasi nzuri ya mbio za ubingwa wa Ligi Kuu ya NBC.

Wachezaji wa timu ya Singida Black Stars.

Singida Black Stars iko nafasi ya sita katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC ikiwa imecheza michezo 15 ikishinda michezo saba sare nne na kufungwa michezo minne ikikusanya alama 25.

 Wachezaji wa Azam

Kwa upande wa Azam ipo nafasi ya tatu katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC ikicheza michezo 15 kushinda michezo saba na sare nane huku ikiwa imekusanya alama 29.

Ratiba ya Ligi Kuu ya NBC 2025/2026

TAARIFA YA KAMATI YA UENDESHAJI NA USIMAMIZI WA LIGI YA BODI YA LIGI KUU TANZANIA.

Kamati ya Uendeshaji na Usimamizi wa Ligi ya Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) katika kikao chake cha Machi 26, 2026 ilipitia mwenendo na matukio mbalimbali ya Ligi na kufanya maamuzi yafuatayo;

Ligi Kuu ya NBC

Mechi Namba 85: Pamba Jiji FC 1-1 Simba SC

Mashabiki wa timu ya Simba.

Klabu ya Simba imetozwa faini ya Sh. 10,000,000 (milioni kumi) kwa kosa la mashabiki wake kuwarushia chupa za maji waamuzi wa mchezo tajwa hapo juu wakati wakitoka kiwanjani baada ya kumalizika kwa mchezo huo.Hii ni mara ya pili ndani ya kipindi cha miezi miwili ambapo Februari 25, 2026 mashabiki wa klabu hiyo walimrushia chupa za maji mchezaji wa klabu ya Dodoma Jiji, William Edgar wakati mchezo huo ukiendelea kwenye uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma. Adhabu hii ni kwa mujibu wa Kanuni ya 47:1 ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti kwa Klabu na mazingatio ya kosa la kujirudia.

Mechi Namba 110: TRA United FC 0-0 Young African SC

Klabu ya TRA United ya mkoani Tabora imetozwa faini ya Sh. 500,000 (laki tano) kwa kosa la wachezaji wake kuonyeshwa kadi zaidi ya tano (5) katika mchezo mmoja, ambapo wachezaji hao walionyeshwa jumla ya kadi sita (6) kwenye mchezo tajwa hapo juu.Adhabu hii ni kwa mujibu wa Kanuni ya 47:10 ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti kwa Klabu.

Mechi Namba 126: Mtibwa Sugar FC 1-1 Young Africans SC

Golikipa wa Young Africans,Djigui Diarra.

Mchezaji Djigui Diarra wa klabu ya Young Africans amefungiwa michezo mitatu (3) na kutozwa faini ya Sh. 2,000,000 (milioni mbili) kwa kosa la kumshambulia mwamuzi wakati wa mchezo tajwa hapo juu, mara baada ya mchezo huo kumalizika kwenye uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma.Adhabu hii ni kwa mujibu wa Kanuni ya 41:5(5.3) ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti kwa Wachezaji.Mchezaji Djigui Diarra wa klabu ya Young Africans ametozwa faini ya Sh. 2,000,000 (milioni mbili) kwa kosa la kuonesha kidole cha kati wakati akitoka uwanjani baada ya kumalizika kwa mchezo tajwa hapo juu.

Diarra ametenda kosa kwa mujibu wa Kanuni ya 41:5(5.4) ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti kwa Wachezaji, kwa sababu kitendo hicho kinaashiria matusi na dharau.Adhabu hii ni kwa mujibu wa Kanuni ya 41:5 ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti kwa Wachezaji.

Mwamuzi wa kati wa mchezo tajwa hapo juu, Gilbert Mrina kutoka Kilimanjaro,ameshushwa Daraja la Uamuzi kwa kosa la kushindwa kuchukua hatua stahili kwa mchezaji Djigui Diarra kwa kitendo chake cha utovu wa nidhamu (kumshambulia mwamuzi) kama ilivyoainishwa kwenye Kanuni ya 42:1(1.6) ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti kwa Waamuzi.Adhabu hii imetolewa kwa kuzingatia kuwa ni kosa la kujirudia ambapo mwamuzi Gilbert Mrina alitenda kosa la aina hiyo katika mchezo namba 65 wa Ligi Kuu ya NBC (Mbeya City vs Namungo) na akaadhibiwa kwa kufungiwa mizunguko mitatu (3).Adhabu hii ni kwa mujibu wa Kanuni ya 42:1 ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti kwa Waamuzi.

Mwamuzi msaidizi namba mbili (2) wa mchezo tajwa hapo juu, Abdulaziz Ally kutokaArusha, amefungiwa mizunguko mitano (5) kwa kosa la kushindwa kutafsiri vema sheriaza mpira wa miguu ambapo katika dakika ya 36 ya mchezo alinyoosha kibendera juu kuashiria kulikuwa na kosa la kuotea kabla ya mchezaji Emmanuel Mwanengo wa Young Africans kupokea pasi kutoka kwa Pacome Zouzoua. Hata hivyo, hakukuwa na kosa la kuotea kwa mujibu wa sheria za mpira wa miguu.Adhabu hii ni kwa mujibu wa Kanuni ya 42:1(1.8) ya Ligi Kuu kuhusu Udhibiti kwaWaamuzi.

Imetolewa na;

Idara ya Habari na Mawasiliano

Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB)

SIMBA YAILIZA PRISONS LIGI KUU YA NBC.

TIMU ya Simba imeipa maumivu timu ya Tanzania Prisons baada ya kuifunga mabao 0-2 kwenye mchezo wa Ligi Kuu ya NBC uliochezwa uwanja wa Jamhuri Dodoma.

Mchezo huo uliokuwa muhimu kwa timu zote ambapo Prisons ikitafuta nafasi ya kujitoka katika eneo la hatari huku Simba ikiwa katika harakati za kujiimarisha na kusogea juu zaidi kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC.

 

Dakika 19 zilimtosha mshambuliaji wa Simba Seleman Mwalimu kufungua ukurasa wa mabao wa mchezo huo huku beki wa timu hiyo Rushine De Reuck akifunga bao la pili dakika ya 45 ya mchezo huo kwa mkwaju wa penati hivyo Simba kwenda mapumziko ikiongoza 0-2.

Kipindi cha pili timu ya Prisons iliamua kucheza kwa kujilinda zaidi ili kutokuruhusu mabao mengine jambo ambalo lilifanikiwa na kwa upande wa Simba wakilinda ushindi wao na kuhakikisha pia wanaondoka na hati safi ambapo pia walifanilisha adhma yao.

Dakika 90 za mchezo huo zilifika tamati na beki wa Simba Rushine De Reuck alichaguliwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo akiisaidia timu yake kubeba alama zote 3.

YOUNG AFRICANS HAIKAMATIKI LIGI KUU YA NBC.

TIMU ya Young Africans imefanikiwa kuifunga timu ya Namungo bao moja kwenye mchezo wa Ligi Kuu ya NBC uliochezwa kwenye uwanja wa Majaliwa mkoani Lindi.

Mchezo ulianza kwa timu zote kushambuliana kwa kasi kubwa kuhakikisha wanachukua alama tatu za Ligi Kuu ya NBC ili kujiweka katika nafasi nzuri kwenye mbio za ubingwa wa Ligi Kuu.

Dakika 26 zilimtosha mshambuliaji wa Young Africans Laurindo Dilson kufungua ukurasa wa mabao kupitia mkwaju wa penati baada ya mchezaji wao Max Nzengeli kufanyiwa madhambi na mchezaji wa Namungo bao lililodumu hadi mwisho wa kipindi cha kwanza.

Kipindi cha pili timu zote zilirejea kwa kasi kubwa Namungo ikijaribu kufanya mashambulizi ya mbali ambayo hata hivyo hayakuweza kuzaa matunda hadi dakika 90 za mchezo huo zinatamatika wageni Young Africans walifanikiwa kubeba alama zote tatu kutoka kwa Namungo. Mchezaji Max Nzengeli wa Young Africans alichaguliwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo.

Max Nzemgeli akiwa na tuzo yake

AZAM YATAKATA KMC COMPLEX.

TIMU ya Azam imeendeleza ubabe wake dhidi ya timu ya KMC baada ya kuifunga 0-2 katika mchezo uliopigwa leo kwenye uwanja wa KMC Complex, Dar es Salaam.

Katika mchezo huo timu zote zilikuwa zikiutaka mchezo na zilishambuliana kwa kasi licha ya Azam kuutawala mchezo huo lakini hadi dakika 45 zinatamatika hakuna aliyefanikiwa kuguza nyavu za mwenzake kwa bao.

Akaminko (kushoto) akipambana namchezaji wa KMC

Kipindi cha pili dakika ya 55 ya mchezo mchezaji wa Azam Iddy Seleiman alifungua ukurasa wa mabao wa timu hiyo na kurejea tena kambani dakika ya 64 ya mchezo huo na kufanya Azam kuongoza kwa mabao mawili.

Hadi mwamuzi wa mchezo huo Ramadhani Kayoko anapuliza kipenga cha mwisho matokeo yalisalia 0-2 na kuifanya KMC kuendelea kuburuza ‘mkia’ wa Ligi Kuu ya NBC huku Iddy Selemani akichaguliwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo.