Author: Yahaya Abushehe

NBC CHAMPIONSHIP HAKUNA KULALA, MECHI TATU KUPIGWA LEO.

 

LIGI ya NBC Championship inaendelea leo januari 7, kwa michezo mitatu kupigwa kwenye mikoa mitatu tofauti.

Mkoani Mara Biashara United watakuwa wenyeji wa Mbuni saa 8:00 mchana kwenye uwanja wa Karume.

Mchezo huo unabeba hisia za mashabiki wengi kutokana na nafasi za kila timu, Biashara wapo nafasi ya tano kwenye msimamo wakiwa na alama 30 huku Mbuni ikiwa nafasi ya sita kwenye msimamo na alama 27 hivyo kila timu kupambana kutafuta alama tatu ili kusogea juu zaidi kwenye msimamo.

Ruvu Shooting watawaalika FGA Talents kwenye uwanja wa Jamhuri mkoani Dodoma saa 10:00 alasiri, Ruvu Shooting wapo nafasi ya mwisho kwenye msimamo wakiwa na alama mbili pekee baada ya kucheza michezo 15.

Mchezo wa mwisho hii leo utazikutanisha Cosmopolitan na Pamba kwenye uwanja wa Mabatini mkoani Pwani saa 10:00 alasiri.

Michezo hii inakwenda kukamilisha mzunguko wa 16 wa Ligi ya NBC Championship.

YANGA KUWAVAA APR ROBO FAINALI KOMBE LA MAPINDUZI LEO.

 

KOMBE la Mapinduzi linaendelea leo Januari 7 katika hatua ya Robo fainali ambapo mwakilishi wa Ligi Kuu ya NBC Yanga atakuwa kibaruani saa 2:15 usiku kwenye uwanja wa New Amaan Complex kuwakabili APR ya Rwanda.

Yanga wamefika hatua hii baada ya kuongoza kundi C kwa kujikusanyia alama saba kwenye michezo mitatu huku APR wakipita kama best looser kutoka kundi B.

Wawakilishi wengine wa Ligi Kuu ya NBC Azam, Singida na Simba wao watacheza michezo yao ya robo fainali kesho januari 8.

TMA, POLISI ZATAKATA NBC CHAMPIONSHIP LEO.

 

LIGI ya NBC Championship imeendelea leo Januari 6, kwa michezo minne kupigwa kwenye mikoa mitatu tofauti.

Mkoani Pwani michezo miwili ilipigwa kwenye uwanja wa Mabatini huku mapema saa 8:00 mchana Pan African waliwaalika Copco na mchezo huo kumalizika kwa sare ya bao moja, saa 10:00 alasiri Green Warriors wakawaalika Mbeya City na kumalizika kwa suluhu.

Polisi Tanzania wakiwa kwenye uwanja wao wa nyumbani ushirika mkoani Kilimanjaro saa 8:00 mchana wakawakaribisha Mbeya Kwanza na kuibuka na ushindi wa bao moja.

Mkoani Shinyanga saa 10:00 alasiri Stand United ikawakaribisha TMA kwenye uwanja wa Mwadui Complex na Stand United kukubali kichapo cha mabao 1-6.

Kwa matokeo hayo TMA wanapanda hadi nafasi ya pili kwenye msimamo wakiwa na jumla ya alama 33 baada ya michezo 16.

NBC CHAMPIONSHIP KUPIGWA MIKOA MITATU TOFAUTI LEO.

 

LIGI ya NBC Championship inaendelea leo Januari 6, 2024 kwa michezo minne kuchezwa kwenye mikoa mitatu tofauti.

Michezo ya mapema saa 8:00 mchana itazikutanisha Pan African na Copco katika uwanja wa Mabatini mkoani Pwani, na mchezo mwingine Polisi Tanzania watawaalika Mbeya Kwanza katika uwanja wa Ushirika, Kilimanjaro.

Green Warriors watakuwa wenyeji wa Mbeya City saa 10:00 alasiri katika uwanja wa Mabatini mkoani Pwani, huku Stand United wakicheza na TMA katika uwanja wa Mwadui Complex, Shinyanga.

Ken Gold wapo kileleni mwa msimamo wa Ligi hiyo wakiwa na jumla ya alama 36 baada ya michezo 16, Mbeya kwanza wanashika nafasi ya pili wakiwa na alama 32 baada ya michezo 15 huku nafasi ya tatu ikishikwa na Pamba akiwa na alama 31 baada ya michezo 15.

NBC CHAMPIONSHIP KUREJEA LEO, TRANSIT CAMP KUWAVAA KEN GOLD.

 

Ligi ya NBC Championship inaendelea leo kwa Mchezo mmoja kati ya Transit Camp na Ken Gold saa 10:00 alasiri kwenye uwanja wa Jamhuri mkoani Morogoro.

Transit Camp wapo nafasi ya 13 wakiwa na alama 13 baada ya michezo 15 huku Ken Gold wakiwa kileleni mwa msimamo wakiwa na alama 35 baada ya michezo 15.

Ligi hiyo itaendelea tena kesho kwa michezo minne katika mikoa mitatu tofauti.