Category: STORY

PAMBA YAANZA KIBABE NBC CHAMPIONSHIP

LIGI ya NBC Championship imeendelea leo Septemba 11 kwa mchezo mmoja kuchezwa kati ya Pamba Jiji ya Mwanza na Cosmopoilitan ya Dar uliomalizika kwa Cosmo kupoteza kwa mabao 4-0.

Mchezo huo uliopigwa katika uwanja wa Nyamagana mkoani Mwanza umeshuhudiwa Cosmo waliokuwa mabingwa wa First League msimu wa 2022-2023 wakienda mapumziko wakiwa wameruhusu mabao matatu.

“Hii timu ina malengo yake, niliwaambia wachezaji tunahitaji sana kupanda Ligi Kuu ya NBC na endapo tukifungwa sana isiwe zaidi ya mechi mbili na wametekeleza majukumu tumeweza kupata ushindi” amesema kocha mkuu wa Pamba Mbwana Makata.

Kwa ushindi huo Pamba imepanda moja kwa moja kileleni mwa msimamo wa Ligi ya NBC Championship kwa tofauti ya idadi ya mabao juu ya timu za Mbeya City, Pan Africans na FGA Talents walioshinda michezo yao kwanza kama ilivyo kwa Pamba.

NBC CHAMPIONSHIP YAPAMBA MOTO

LIGI ya NBC Championship imeendelea Leo Septemba 10 kwa michezo minne kuchezwa kwenye mikoa mitatu tofauti.

Mchezo wa mapema saa 8:00 mchana ulizikutanisha TMA na Stand United katika uwanja wa Sheikh Amri Abeid, Arusha na kumalizika kwa suluhu.

Mchezo mwengine ulizikutanisha Mbuni na Biashara United saa 10:00 alasiri kwenye uwanja wa Sheikh Amri Abeid, Arusha na kumalizika kwa sare ya bao moja.

KenGold wakiwa katika uwanja wao wa nyumbani Sokoine mkoani mbeya wakagawana alama na Transit Camp kwa sare ya bao moja.

FGA Talents imekuwa timu pekee kwa siku ya leo kuondoka na alama tatu baada ya kuwafunga Ruvu shooting mabao 2-1 kwenye uwanja wa Jamnhuri mkoani Morogoro.

Ligi hiyo itaendelea tena kesho Septemba 11 kwa mchezo mmoja kuchezwa Pamba wakiwaalika Cosmopolitan kwenye uwanja wa Nyamagana mkoani Mwanza.

NBC CHAMPIONSHIP KUENDELEA TENA LEO.

PAZIA la Ligi ya NBC Championship lilifunguliwa rasmi jana septemba, 9 kwa michezo mitatu kuchezwa.

Ligi hiyo itaendelea tena leo kwa michezo minne kati ya TMA na Stand United kwenye uwanja Sheikh Amri Abeid,Arusha saa 8:00 mchana.

Mchezo wa pili utazikutanisha Ken Gold dhidi ya Transit Camp uwanja wa Sokoine, Mbeya saa 10:00 alasiri.

Mchezo wa tatu ni Kati ya FGA Talents na Ruvu Shooting uwanja wa Jamhuri Mkoani Morogoro saa 10:00 alasiri na Mchezo wa mwisho Mbuni atakuwa mwenyeji wa Biashara United kwenye uwanja wa Sheikh Amri Abeid, Arusha saa 10:00 alasiri.

WARATIBU ‘WANOLEWA’ DAR.

SHIRIKISHO la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kwa kushirikiana na Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) leo Septemba 9, imeendesha semina ya waratibu wa michezo iliyofanyika kwenye ukumbi wa mikutano Benjamin Mkapa Dar es saalam.

Semina hiyo ilikuwa na lengo la kuwaongezea ufanisi katika kusimamia michezo mbalimbali ya kimashindano iliyo chini ya TFF na TPLB.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa semina hiyo Afisa Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Ligi Kuu Almasi Kasongo amesema lengo la semina hiyo ni kuongeza ufanisi na uwezo wa waratibu katika usimamizi wa michezo inayoendeshwa chini ya TFF na Bodi ya ligi.

Kasongo amewataka waratibu wa michezo kuwa mabalozi Wazuri wa Bodi ya Ligi na TFF katika usimamizi wa michezo.

“Ligi yetu ni ya 5 kwa ubora na hili limefanikiwa kwa mchango wenu katika kusimamia michezo hii vizuri hivyo niwaombe muendelee kuwa bora zaidi kupitia mafunzo haya” alisema Kasongo.

Miongoni mwa mada zilizowasilishwa ni pamoja na udhamini wa ligi na mipangilio (League sponsorship and branding), taratibu za mchezo (Match Coordination), taratibu za habari siku ya mchezo (Match day media operations) na Kanuni (Regulations).

Semina hiyo imehudhuriwa na waratibu Zaidi ya 30 kutoka mikoa zaidi ya 22 Tanzania Pamoja na watumishi wa Bodi ya Ligi na TFF.

NBC CHAMPIONSHIP KUANZA RASMI LEO

PAZIA la Ligi ya NBC Championship msimu wa 2023/2024 linafunguliwa rasmi leo Septemba 9 kwa michezo mitatu kuchezwa katika viwanja mbalimbali.

Mchezo wa kwanza wa ufunguzi utazikutanisha Mbeya City dhidi ya Green Warriors saa 10:00 alasiri katika uwanja wa Sokoine, Mbeya mchezo wa pili utazikutanisha Mbeya Kwanza dhidi Polisi Tanzania saa 10:00 alasiri katika Uwanja wa Nangwanda Sijaona, Mkoani Mtwara na mchezo wa mwisho ni kati ya Copco na Pan Africans saa 10:00 alasiri uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza.

Hii ni kwa mara ya kwanza Ligi ya Championship kupata udhamini ambapo Benki ya Taifa ya Biashara, NBC imeandika historia ya kuwa mdhamini wa kwanza na kuifanya Ligi hiyo sasa kutambulika kama Ligi ya NBC Championship.