Category: STORY

MTIBWA SUGAR YASOGEA NAFASI YA NNE LIGI KUU YA NBC

 

LIGI Kuu ya NBC imeendelea kwa mchezo mmoja uliochezwa katika uwanja wa Jamhuri mkoani Dodoma na kushuhudia Mtibwa sugar ikifanikiwa kuondoka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Mbeya City.

Mtibwa Sugar ilianza mchezo kwa kasi na dhamira ya kutafuta ushindi mapema na juhudi zao zilizaa matunda dakika ya 27 baada ya George Chota kufunga bao la kwanza kwa shuti lililomshinda kipa wa Mbeya City Beno Kakolanya na kuwapa wenyeji uongozi wa 1-0.

Mbeya City haikukata tamaa na dakika ya 45+2 Eliud Ambokile aliisawazishia Mbeya City bao baada ya kutumia vyema krosi ya beki wa kulia Maranyingi na kufanya matokeo kuwa 1-1 hadi mapumziko.

Kipindi cha pili kilianza kwa kasi kubwa kutoka Mtibwa Sugar wakitafuta bao la ushindi na dakika ya 63 Said Mkopi aliibuka shujaa baada ya kufunga bao la pili kwa ustadi mkubwa lililowarejesha Mtibwa Sugar mbele na matokeo kuwa 2-1.

Mbeya City ilijaribu kurejea mchezoni kwa kuongeza kasi ya mashambulizi lakini safu ya ulinzi ya Mtibwa Sugar ilisimama imara hadi filimbi ya mwisho na kuhakikisha wanachukua alama tatu muhimu huku timu hiyo ikipanda hadi nafasi ya 4 kwenye msimamo wa Ligi Kuu wakifikisha na alama 14.

 

YOUNG AFRICANS ‘YAICHAPA’ MASHUJAA LIGI KUU YA NBC.

Young Africans imeendelea kuonyesha ubora wao katika Ligi Kuu ya NBC ilipokutana na Mashujaa katika wa uwanja KMC Complex baada ya kuichapa Mashujaa mabao 6-0.

Kikosi cha Young Africans kilitawala mchezo kuanzia dakika ya kwanza hadi mwisho huku wachezaji sita wakiandika majina yao kwenye orodha ya wafungaji.

Bao la kwanza lilifungwa mapema dakika ya 8 na Mohamed Damaro na dakika ya 28 Duke Abuya aliongeza bao la pili baada ya kumalizia pasi safi kutoka kwa Maxi Nzengeli.

Dakika saba baadae Pacome Zouzoua aliweka bao la tatu kwenye dakika ya 35 na Young Africans kwenda mapumziko ikiwa mbele kwa mabao matatu.

Kipindi cha pili Young Africans waliendelea kushambulia bila kuchoka na alikuwa Prince dube alifunga bao la nne dakika ya 79 kabla ya Mudathir Yahya kuongeza bao la tano dakika moja baadae na msumari wa sita wa ‘Wananchi’ ulipigiliwa na mshambuliaji wao mpya Laurindo Dilson ‘Depu’.

Ushindi huu unaipeleka Young Africans ‘kileleni’ mwa msimamo wa Ligi Kuu ya NBC Katika mchezo huu Mudathir Yahya alikuwa mchezaji bora wa mchezo huu

SIMBA YABANWA NYUMBANI LIGI KUU YA NBC.

TIMU ya Simba imeshindwa kupata ushindi kwenye mchezo wa pili mfululizo baada ya kulazimishwa sare ya bao moja na timu ya Mtibwa Sugar kwenye uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, Dar es Salaam.

‘Mnyama’ alikuwa wa kwanza kupata bao kupitia kwa Ellie Mpanzu mapema kipindi cha kwanza kabla ya Mtibwa kusawazisha kupitia kwa Magata Fredrick bao lililowapa Mtibwa alama moja muhimu ugenini dhidi ya timu inayowakilisha nchi kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika.

Simba imeshindwa kupata ushindi nyumbani kwa mara pili mfululizo baada ya kupoteza mchezo uliopita dhidi ya Azam kwa mabao 2-0.

Sare hiyo inaifanya Simba kukaa nafasi ya nne ikifikisha alama 13 huku Mtibwa ikifikisha alama 11 na kusalia nafasi ya nane kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC.

Ligi Kuu ya NBC itaendelea leo Januari 19 kwa mchezo mmoja kati ya Young Africans itakayokuwa mwenyeji wa Mashujaa kwenye uwanja wa KMC, Dar es Salaam.

Endapo Young Africans itafanikiwa kupata ushindi leo itaishusha timu ya JKT Tanzania na kukwea kileleni mwa Ligi Kuu ya NBC.

AZAM YA IBENGE NI MOTO WA KUOTEA MBALI LIGI KUU YA NBC.

TIMU ya Azam yenye maskani yake kwenye uwanja wa Azam Complex imekuwa moto wa kuotea mbali msimu huu ikiwa haijapoteza mchezo wowote wa Ligi Kuu ya NBC hadi sasa.

Mchezo uliopita Azam ilishinda dhidi ya Coastal Union kwenye uwanja wa nyumbani kwa mabao 3-0 yaliyofungwa na Yahya Zayd, Feisal Salum na Jephte Kitambala huku mabao yote yakifungwa kipindi cha kwanza na kudumu kwa dakika zote 90.

Azam imefunga mabao 9 na kuruhusu mabao mawili pekee huku ikiwa imetoka sare michezo mitatu hadi sasa kwenye Ligi Kuu ya NBC.

Timu hiyo inaingia mawindoni kulisaka taji la Ligi Kuu ya NBC baada ya kulikosa kwa miaka 13 wakiwa na matumaini ya kufanya hivyo msimu huu chini ya kocha Florent Ibenge ambaye hadi sasa amewasaidia kufuzu hatua ya makundi ya mashindano ya Afrika kwa mara ya kwanza kuanzia timu hiyo ianzishwe.

Mara ya mwisho timu ya Azam kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu ilikuwa mwaka 2013 na walitwaa bila kupoteza mchezo wowote.

NBC CHAMPIONSHIP YAFIKA PATAMU.

IKIKAMILISHA mizunguko 15 Ligi ya NBC Championship imepamba moto timu zote zikiwa zimecheza michezo 15 huku zikisaliwa na michezo 15 kufunga msimu.

Geita Gold inaongoza mbio za ubingwa ikiwa na alama 37 baada ya kushinda michezo 11 huku ikiwa timu pekee ambayo haijapoteza mchezo wowote hadi sasa.

Kagera Sugar inashika nafasi ya pili ikiwa na alama 36 ikipoteza mchezo mmoja pekee kwenye mzunguko wa 15 dhidi ya ‘wababe’ wa mkoa wa Tabora timu ya Mbeya Kwanza inayokamata nafasi ya tatu ikiwa na alama 34.

Transit Camp inashika nafasi ya nne ikiwa na alama 33 ikizidiwa alama nne pekee na vinara wa ligi hiyo timu ya Geita Gold, Transit ikiwa imeshinda michezo 10 hadi sasa, ikipoteza miwili na kutoa sare mitatu.

Bingwa wa ligi ya Championship ya NBC atapata Kikombe na kupanda daraja moja kwa moja hadi Ligi Kuu ya NBC, mshindi wa pili akipanda daraja huku mshindi wa tatu na wa nne wakicheza mchezo wa mtoano na timu itakayoshinda kwenye matokeo ya jumla itacheza na timu ya Ligi Kuu ya NBC ili kupata timu moja itakayoshiriki ligi hiyo ya nne kwa ubora Afrika msimu wa 2026/27.