Category: STORY

WAKALI WA MGUU WA KUSHOTO LIGI KUU YA NBC

LIGI Kuu ya NBC inazidi kushika kasi ikiwa ni takribani michezo 183 imeshachezwa huku mabao 406 yakiwa yamefungwa ikiwemo yaliyofungwa kwa mguu wa kushoto na wakali wafuatao.

Ki Azizi ni kiungo mshambuliaji wa Young African katika msimu huu wa 2024/2025 ameshatia wavuni mabao sita kwa mguu wake wa kushoto kati ya mabao saba aliyofunga mpaka sasa.

Winga wa  timu ya Azam, Gibril Sillah, ameshatia wavuni mabao matano  kwa mguu wake wa kushoto kati ya saba ambayo ameshafunga mpaka sasa.

Offen Chikola wa Tabora United ameshatikisa nyavu mara tano kwa mguu wa kushoto kati ya mabao saba aliyofunga msimu huu.

Nassor Saaduni ni mshambuliaji wa Azam akiwa amefanikiwa kuingia langoni mwa wapinzani wao mara tano akitumia mguu wake wa kushoto.

Mchezaji Selemani Bwenzi aliyeingia dirisha dogo kwa timu ya KenGold mkali huyo mpaka sasa amefanikiwa kutikisa nyavu za wapinzani akitumia mguu wake wa kushoto.

Naye mchezaji wa Namungo Joshua Ibrahimu kafanikiwa kuweka mpira wavuni mara nne akitumia mguu wake wa kushoto.

HAWA HAPA WABABE WA MABAO NBC CHAMPIONSHIP

LIGI ya championship ya NBC inazidi kushika kasi ikielekea ukingoni huku Mbeya City ikiwa kinara wa ‘kupachika’ mabao baada ya kufunga mabao 45 hadi sasa ikiwa ni idadi kubwa kwa timu ya Ligi hiyo hadi sasa.

Mbeya city ipo nafasi ya pili kwenye msimamo ikiwa na alama 49 huku Mtibwa sugar ikiwa kinara kwenye msimamo na alama 54 na ikishika nafasi ya pili kwa mabao baada ya kufunga 44 na kuruhusu mabao 11 hadi sasa.

Geita gold inashika nafasi ya nne kwenye msimamo ikiwa na alama 48 huku ikiwa timu ya tatu kwa idadi kubwa ya mabao baada ya kufunga 41 huku ikifungwa mabao 17.

Stand united ni timu ya nne kwa kupachika mabao ikiwa nayo 37 na kufungwa 19 huku ikishika nafasi ya tatu kwenye msimamo wa ligi na alama 49.

‘TSHABALALA’ MKALI WA PASI ZA MWISHO LIGI KUU NBC.

BEKI wa timu ya Simba,Mohammed Hussein ‘Tshabalala’ ndiye kinara wa  kutoa pasi za mwisho kwenye Ligi Kuu ya NBC msimu huu wa 2024/2025 akiwa nazo nne.

Tshabalala alitoa pasi za mwisho na kuisaidia timu yake kupata alama katika michezo ya Simba dhidi ya timu za Fountain Gate (1),Dodoma Jiji (1),Tabora (1) na Kagera Sugar.

Nafasi ya pili inashikiliwa na beki wa Singida Black Stars, Ande Koffi akiwa ametoa pasi tatu katika mechi za Singida dhidi ya Fountain Gate (1),Pamba Jiji (1) na KenGold (1).

Datius Peter wa Kagera Sugar anafuata akiwa na pasi za mwisho tatu alizotoa katika michezo ya Kagera Sugar dhidi ya timu za Pamba Jiji (1),KenGold (1) na mchezo wa Mashujaa (1).

Beki wa Simba, Shomari Kapombe, amepiga pasi za mwisho tatu alizoweza kutoka katika michezo ya timu yake dhidi ya Prisons (2) na Fountain Gate (1).

Beki na nahodha wa Fountain Gate,Amos Kadikilo anashika nafasi ya tano akiwa na pasi za mwisho tatu alizopata katika michezo ya Fountain Gate dhidi ya Namungo (1) na Tanzania Prisons (2).

Wachezaji wa Biashara United wakishangilia bao pekee walilofunga dhidi ya African Sports kwenye mchezo uliopigwa uwanja wa Karume, Mara.

BIASHARA YAFUFUA MATUMAINI MZUNGUKO UKIKAMILIKA NBC CHAMPIONSHIP.

MZUNGUKO wa 23 wa Ligi ya Championship ya NBC umehitimishwa jana kwa mchezo mmoja kuchezwa katika uwanja wa Karume Mkoani Mara na kushuhudia Biashara United ikiibuka na Ushindi wa Bao 1-0 dhidi ya African Sports.

Licha ya Ushindi huo Biashara United inaendelea kusalia nafasi ya mwisho kwenye msimamo ikifikisha alama saba baada ya michezo 23.

Ikumbukwe Biashara United ilipokwa alama 15 baada ya kushindwa kutokea kwenye mchezo dhidi ya Mbeya City.

Mtibwa Sugar inaendelea kusalia kileleni licha ya kupoteza kwenye mchezo wake dhidi ya Stand United ikiwa na alama 54 baada ya michezo 23 ikifuatiwa na Mbeya City na Stand United kwa pamoja zikiwa na alama 49 zikipishana kwa mabao ya kufunga na kufungwa.

STAND, GEITA, MBEYA CITY MOTO HAUZIMI LIGI YA CHAMPIONSHIP YA NBC.

LIGI ya Championship ya NBC imeendelea jana kwa michezo mitatu iliyoshuhudia mabao nane yakifungwa na magolikipa watatu wakimaliza michezo bila kuruhusu bao.

Stand United ilikuwa mwenyeji wa Mtibwa Sugar ya Morogoro kwenye uwanja wa Kambarage, Shinyanga na kushuhudia Stand ikikusanya alama zote tatu baada ya ushindi wa bao moja lililofungwa na Omar Issa mapema dakika ya sita kwa mkwaju wa penati.

Matokeo hayo yanaifanya Stand kufikisha alama 49 na kukaa nafasi ya tatu huku ikiwa timu ya pili kwa kushinda michezo mingi msimu huu ikishinda 15 sawa na timu ya Geita Gold.

Geita Gold ilikuwa nyumbani kwenye uwanja wa Nyankumbu, Geita na kufanikiwa kuichapa Mbeya Kwanza mabao 3-0 yaliwekwa kambani na Andrew Simchimba (2) na Jackson Suluja aliyefunga moja.

Geita inafikisha alama 48 na kusalia nafasi ya nne nyuma ya Stand United inayoshika nafasi ya tatu na Mbeya City inayoshika nafasi ya pili na kufanya upinzani wa kucheza Ligi Kuu ya NBC msimu ujao kuzidi kushika kasi.

Mchezo wa mwisho ulikuwa kati Mbeya City iliyoshusha mvua ya mabao 4-0 dhidi ya timu ya Kiluvya kwenye uwanja wa Sokoine, Mbeya huku mchezaji wa Mbeya City Mwami Thobias akifunga mabao matatu na Adil Buha kufunga moja.

Ushindi huo umeifanya Mbeya City kusalia nafasi ya pili ikifikisha alama 49 huku ikiwa kinara wa mabao hadi sasa baada ya kufunga (45) huku Cosmopolitan ikiwa timu iliyofunga mabao machache (15).