Category: STORY

CAMARA KINARA WA KUTORUHUSU MABAO LIGI KUU YA NBC.

Kipa wa Simba Moussa Camara amezidi kujiweka katika nafasi nzuri baada ya kucheza michezo 12 bila kuruhusu bao katika michezo 15 ya Ligi Kuu ya NBC aliyocheza.

Golikipa huyo aliyesajiliwa na Simba msimu huu ameonekana kama ‘lulu’ baada ya kuruhusu mabao Matano tu katika michezo yote aliyocheza huku timu yake ikiwa imefunga mabao 31 na kufanikiwa kuwa kileleni mwa msimamo wa ‘Cleansheet’ ndani ya Ligi Kuu ya NBC.

Camara alifungwa na Yanga oktoba 19 katika dabi ya kariakoo goli walilojifunga Simba kupitia mchezaji wao Kelvin Kijili hivyo mchezo kumalizika kwa Yanga kushinda mchezo huo mhimu.

Katika mchezo wa Simba dhidi ya Coastal Union uliochezwa uwanja wa KMC, Camara aliruhusu mabao mawili kipindi cha pili cha mchezo huo na pia mchezo wa Kagera Sugar dhidi ya Simba uliochezwa uwanja wa Kaitaba Simba walishinda mabao matano huku wakiruhusu mabao mawili.

Patrick Munthali wa Mashujaa anashika nafasi ya pili kwenye msimamo huo baada ya kufanikiwa kukusanya nane katika michezo 16 ambayo timu yake imecheza.

Nafasi ya tatu inashikiliwa na Djigui Diarra akiwa amekusanya saba sawa na Metacha Mnata wa Singida Big Stars.

Kipa wa Azam Mohamed Mustapha naye yupo katika orodha hii baada ya kufanikiwa kukusanya sita huku timu yake ikiwa na alama 36 kwenye nafasi ya tatu katika msimamo wakiwa wameruhusu mabao nane na wakifunga mabao 25.

LIGI KUU NBC KUSIMAMA KWA MIEZI MIWILI

BODI ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) imetangaza rasmi kuwa baada ya michezo ya Ligi Kuu ya NBC iliyofanyika Desemba 29, 2024, Ligi hiyo itasimama hadi Machi 1, 2025 itakaporejea kwa michezo ya mzunguko wa 17.

Kusimama kwa Ligi hiyo ni kutokana na kupisha michuano ya kuwania Kombe la Mapinduzi itakayofanyika kisiwani Pemba na Fainali za Mataifa ya Afrika kwa 6wachezaji wa ndani (CHAN), ambazo Tanzania ni moja ya nchi zitakazoandaa shindano hilo.

Bodi imejipanga kuhakikisha msimu wa 2024/2025 unafika tamati kwa wakati kwa mujibu wa kanuni za Ligi, hivyo kutoathiri kipindi cha mapumziko na maandalizi ya msimu wa 2025/2026 kwa klabu zetu.

Aidha, Bodi ya Ligi Kuu Tanzania inaamini klabu zake zitatumia kipindi hiki kufanya marekebisho na maboresho katika vikosi vyake ili kuendana na ushindani mkubwa uliopo kwenye Ligi Kuu ya NBC msimu huu.

Bodi inaitakia kila la kheri timu ya taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ katika michuano tajwa hapo juu huku pia ikiwatakia kheri ya mwaka mpya 2025 wadau wote wa mpira wa miguu zikiwemo klabu, mashabiki, wadhamini, vyama vya soka vya mikoa, vyama shiriki na watanzania wote kwa ujumla.

RUPIA HASHIKIKI LIGI KUU YA NBC

MSHAMBULIAJI wa Singida Black Stars Elvis Rupia amekuwa kinara wa kuchana nyavu za timu mbalimbali za Ligi Kuu ya NBC kwa kufunga mabao baada ya kufanikiwa kuifungia mabao nane timu yake hadi sasa.

Rupia ameweza kufunga katika michezo ya Singida dhidi ya KenGold, Dodoma, Azam, Tabora na JKT Tanzania ndani ya michezo 16 ambayo timu yake imecheza na kufanikiwa kuipatia alama 33 ikiwa nafasi ya nne katika msimamo wa Ligi Kuu.

Kiungo wa Simba Jean Ahoua anashikilia nafasi ya pili akiwa ameshafunga mabao saba na kuweza kusaidia timu yake kupata alama 40 huku ikiwa kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu.

Selemani Mwalimu wa Fountain Gate anashikilia nafasi ya tatu akiwa amefunga mabao sita na kuiwezesha timu yake kupata alama 20 huku wakiwa nafasi ya sita katika msimamo wa Ligi Kuu.

Clement Mzize wa Yanga anafuata licha ya kuanza msimu vibaya baada ya kuwa majeruhi mpaka sasa amefanikiwa kufunga mabao sita huku timu yake ikiwa imekusanya alama 39.

Leonel Ateba wa Simba amefunga mabao matano akiwa katika mbio za ufungaji bora kwa kuiwezesha timu yake kupata alama 40 huku wakiwa ndio vinara wa kukusanya alama nyingi kuliko timu yoyote.

HII HAPA TAARIFA YA KAMATI YA UENDESHAJI NA USIMAMIZI WA LIGI.

KAMATI ya Uendeshaji na Usimamizi wa Ligi ya Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) katika kikao chake imepitia mwenendo na matukio mbalimbali na kufanya maamuzi yafuatayo

Meneja wa Klabu ya KenGold, Nuhu Nkaekwa amefungiwa michezo mitatu na kutozwa fani ya shilingi laki tano kwa kosa la kumshambulia kwa maneno makali mwamuzi msaidizi namba moja katika mchezo wa KenGold na Pamba kulingana na kanuni ya 45:4(2.11) ya Ligi Kuu pia meneja huyo amefungiwa michezo miwili na kutozwa faini ya shilingi milioni moja kwa kosa la kutoboa mpira mmoja uliokuwa ukitumika katika mchezo huo na atapaswa kulipa mpira mpya kwa mujibu wa kanuni ya 45:2(2.5)ya Ligi Kuu.

Klabu ya Kagera Sugar ya mkoani Kagera imepewa onyo kali kwa kosa la kuchelewa kuwasili kwenye kikao cha kitaalamu cha maandalizi ya mchezo wao dhidi ya Namungo disemba 10 mjini Bukoba ambapo Kagera waliwasili saa nne na dakika 10 badala ya saa nne kamili huku adhabu hii ikiwa kwa mujibu wa kanuni ya 1:2(2.2) ya Ligi Kuu kuhusu taratibu za michezo.

Kocha msaidizi wa Azam Bard Eddine ametozwa faini ya shilingi milioni moja kwa kosa la kuvunja paa la benchi la ufundi kwa hasira baada ya mchezo kumalizika katika uwanja wa Ali Hassan Mwinyi mjini Tabora wakati wa mchezo wa Tabora United dhidi ya Azam aidha kocha huyo atalazimika kulipa gharama za matengenezo ya paa hilo kwa mujibu wa kanuni ya 45:2(2.5) kuhusu udhibiti wa Makocha.

Ofisa Mtendaji Mkuu wa Klabu ya JKT Tanzania Jemedari Said amepewa onyo kali kwa kosa la kuingia katika eneo la kimashindano la uwanja wa KMC Complex wakati wa mchezo wa Simba dhidi ya JKT ukiendelea.

Kiongozi huyo alishuka kutoka jukwaani na kwenda hadi eneo la benchi la ufundi la klabu yake kwa lengo la kuzungumza na viongozi kinyume na matakwa ya kanuni ya 17:17 ya Ligi Kuu kuhusu taratibu za michezo

Klabu ya JKT Tanzania imetozwa faini ya shilingi milioni 5 kwa kosa la wachezaji wake kuonywa kwa kadi zaidi ya mara tano katika mchezo wa Simba dhidi yaoambapo JKT walionywa kwa kadi mara saba na adhabu hii ikiwa ni kwa mujibu wa kanuni ya 47:10 ya Ligi Kuu.

Kamati ya Uendeshaji na Usimamizi wa Ligi ya Bodi ya Ligi Kuu imempa onyo kali Mkurugenzi wa Ufundi wa Yanga Abdihimid Moallin kwa kosa la kuketi kwenye benchi la ufundi katika michezo mitatu ya Ligi Kuu ya NBC kinyume na matakwa ya Kanuni ya 17:17 ya Ligi Kuu kuhusu taratibu za michezo adhabu imetolewa kwa mujibu wa kanuni ya 17:62 kuhusu taratibu za michezo.

Aidha Bodi ya Ligi Kuu imepokea taarifa kutoka Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kuwa klabu ya Yanga imekamilisha taratibu zote za kumtumia Abdihamid Moallin kama kocha msaidizi.

Kwa upande wa Ligi ya Championship Mchezaji Pascal Mwakapusya wa klabu ya Mbuni, amefungiwa michezo mitano na kutozwa faini ya Shilingi milioni moja kwa kosa la kumpiga mwamuzi msaidizi namba mbili, Leah Petro wa mchezo kati ya Mbuni FC na Mtibwa Sugar FC kabla hajaokolewa na walinzi wa uwanjani (stewards) 1adhabu hii imetolewa kwa kuzingatia kanuni ya 41:5(5.3) ya Ligi ya Championship kuhusu Udhibiti kwa Wachezaji.

Klabu ya Mbuni ya mkoani Arusha imetozwa faini ya shilingi milioni moja kwa kosa la mashabiki wake kumshambulia kwa matusi na kumpiga mwamuzi msaidizi namba mbili (2), Leah Petro wa mchezo tajwa hapo juu, kabla hajaokolewa na walinzi wa uwanjani (stewards) adhabu hii ni kwa kuzingatia Kanuni ya 47:1 ya Ligi ya Championship kuhusu Udhibiti kwa Klabu.

Klabu ya Biashara United ya mkoani Mara imeadhibiwa kwa kutozwa faini ya Shilingi milioni tatu na kupoteza mchezo wa Mbeya City FC dhidi ya Biashara United FC na kupokwa alama 15 (kumi na tano) katika msimamo wa Ligi ya Championship ya NBC 2024/2025, kwa kosa la kushindwa kufika kwenye uwanja wa Sokoine mkoani Mbeya bila sababu za msingi, jambo lililosababisha mchezo huo usifanyike.

Biashara iliiandikia barua Bodi ya Ligi Kuu Tanzania kuomba mchezo huo ambao awali ulipangwa kufanyika Desemba 1, 2024 usogezwe mbele na ombi lao likakubaliwa ambapo mchezo huo ulipangwa kufanyika Desemba 3, 2024 hata hivyo klabu ya Biashara United haikufika uwanjani katika tarehe hiyo mpya, hivyo maofisa wa mchezo huo kuahirisha mchezo kwa mujibu wa Kanuni.

Kufuatia maamuzi hayo ya kamati, klabu ya Mbeya City imepewa alama tatu na mabao matatu adhabu hii imetolewa kwa kuzingatia kanuni ya 31:1 ya Ligi ya Championship kuhusu Kutofika Uwanjani.

Kocha wa magolikipa wa klabu ya Geita Gold, Augustino Malindi amefungiwa michezo 16 (kumi na sita) na kutozwa faini ya Shilingi milioni moja kwa kosa la kumshika sehemu za siri mwamuzi wa akiba wa mchezo wa Mbeya City FC 1-0 Geita Gold FC, baada ya kuonywa kwa kadi nyekundu kwa kosa la kumtukana mwamuzi msaidizi namba moja wa mchezo huo.

Kocha huyo alitenda kosa lingine akiwa anakwenda vyumbani baada ya kuonywa kwa kadi, kwa kumshika kifuani mratibu wa mchezo huo (GC) ambaye ni mwanamke jambo ambalo ni kinyume na maadili ya ukocha na mpira wa miguu kwa ujumla adhabu hii imetolewa kwa kuzingatia kanuni ya 45:2(2.1) ya Ligi ya Championship kuhusu Udhibiti kwa Makocha.

Pia kocha Augustino Malindi amefungiwa michezo mitatu na kutozwa faini ya Shilingi laki tano kwa kosa la kumtukana mwamuzi msaidizi namba moja wa mchezo huo jambo lililosababisha aonywe kwa kadi nyekundu adhabu hii imetolewa kwa kuzingatia kanuni ya 45:2(2.11) ya Ligi ya Championship kuhusu Udhibiti kwa Makocha.

Kwa upande wa First League Kocha wa klabu ya African Lyon, Elia James amefungiwa michezo mitatu na kutozwa faini ya Shilingi laki tano kwa kosa la kuwatukana waamuzi wa mchezo wa Hausang FC 1-0 African Lyon FC jambo lililosababisha aonywe kwa kadi nyekundu adhabu hii imetolewa kwa kuzingatia kanuni ya 45:2(2.11) ya First League kuhusu Udhibiti kwa Makocha.

Golikipa wa akiba wa African Lyon, Ibrahim Bigambo amefungiwa michezo mitano na kutozwa faini ya Shilingi laki tano kwa kosa la kumpiga ngumi mchezaji wa klabu ya Hausang, kisha kwenda kujificha ndani ya chumba cha kuvalia cha klabu yake adhabu hii imetolewa kwa kuzingatia kanuni ya 46:3 ya Ligi ya Championship kuhusu Udhibiti kwa Viongozi.

LIGI KUU YA NBC KUENDELEA LEO.

LIGI Kuu ya NBC inaendelea kushika kasi ambapo michezo ya mizunguko ya 14,15 na 16 imepigwa katika mikoa mbalimbali.

Singida Black Stars waliwakaribisha KenGold katika uwanja wa CCM Liti mkoani Singida katika mchezo uliochezwa disemba 24, saa 8:00 mchana.

Mchezo huo uliozikutanisha timu hizo kwa mara ya pili kwenye Ligi Kuu ya NBC ulianza kwa kasi ambapo KenGold walifanikiwa kuanza kutikisa nyavu dakika ya 25 kupitia mchezaji wao Herbet Lukindo hivyo kwenda mapumziko wakiwa wanaongoza kwa bao 1.

Kipindi cha pili Singida walirudi kwa kasi na kufanikiwa kufunga mabao mawili kupitia wachezaji wake Josephat Arthur ambaye pia alichaguliwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo na Elvis Rupia hivyo kufanikiwa kuweka kabatini alama 3 muhimu za mchezo huo.

Mchezo wa pili ulichezwa majira ya saa kumi na robo alasiri mkoani Dar es Salaam Simba wakiwakaribisha JKT Tanzania katika uwanja wa KMC Complex uliopo Mwenge.

Katika mchezo huo timu zote zilishambuliana kwa kasi dakika zote huku timu ya JKT Tanzania wakiwa wanalinda lango lao kwa ustadi mkubwa kuzuia mashambulizi yaliyokuwa yakifanywa na Simba.

Simba walifanikiwa kupata bao dakika za nyongeza za mchezo huo kupitia mkwaju wa penati uliopigwa na mchezaji wao Jean Ahoua baada ya beki wao Shomari Kapombe kufanyiwa madhambi akiwa ndani ya boksi hivyo mchezo huo kuisha kwa 1-0.

Golikipa wa JKT Yakoub Suleiman alichaguliwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo baada ya kuonyesha kiwango kikubwa ndani ya dakika 90.

Disemba 25 Ligi Kuu ya NBC iliendelea mkoani Manyara na Dodoma katika mchezo wa kwanza uliopigwa saa nane mchana Fountain Gate ikiwakaribisha Namungo katika uwanja wa Tanzanite Kwaraa.

Namungo walianza kwa kasi kwa kulisaka lango la mwenyeji wao ambapo dakika ya 10 ya mchezo huo mchezaji Pius Buswita alifanikiwa kuwaweka mbele Namungo na dakika ya 30 mchezaji wa Fountain Gate Salum Kihimbwa aliwafanikiwa kusawazisha hivyo kwenda mapumziko wakiwa 1-1.

Kipindi cha pili Namungo walifanikiwa kufunga bao la pili kupitia mchezaji wao Geofrey Julius hivyo kufanikiwa kuondoka na alama tatu za mchezo huo na pia alichaguliwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo.

Mchezo mwingine ulichezwa jijini Dodoma ambapo Dodoma Jiji waliwakaribisha timu ya Yanga majira ya saa 10 alasiri katika uwanja wa CCM Jamhuri .

Yanga walianza kwa kasi na kufanikiwa kuutawala mchezo huo kwa kiasi kikubwa ambapo dakika ya 19 mshambuliaji Clement Mzize alianza kutikisa nyavu za wenyeji wao, dakika ya 29 Aziz Ki aliongezea bao na dakika chache baadae Mzize aliongezea bao la 3 hivyo Yanga kwenda mapumziko wakiwa mbele kwa mabao matatu.

Kipindi cha pili kilianza kwa Yanga kuendelea kutawala mchezo huo ambapo dakika ya 63 Prince Dube alifunga bao la 4 kwa Yanga na mshambuliaji wa Yanga Clement Mzize alichaguliwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo baada ya kufunga mabao mawili na kiwango kikubwa alichoonyesha katika mchezo huo.

Ligi Kuu itaendelea leo siku ya kufungua zawadi za Krismasi mkoani Mbeya ambapo timu ya Prisons watawakaribisha Pamba kutoka Mwanza saa 10:00 alasiri.