Author: Honest Mwanitega

AZAM YAFANYA ‘MAUAJI’ LIGI KUU YA NBC.

TIMU ya Azam kutoka Dar es Salaam imeishushia kipigo kizito Dodoma Jiji cha mabao 5-0 kwenye mchezo wa Ligi Kuu ya NBC uliochezwa uwanja wa Azam Complex, Dar.

Hiki ni kipigo kikubwa zaidi hadi sasa kwenye mzunguko wa 28 ukisalia mchezo mmoja pekee utakaopigwa leo kukamilisha mzunguko huo.

Nahodha wa Azam Lusajo Mwaikenda alikuwa mfano wa kuigwa na wenzake baada ya kufungua ukurasa wa mabao kwa timu yake dakika ya sita ya mchezo huku Abdul Sopo, Gibril Sillah, Nassor Saadun na Frank Tiesse wakifunga bao moja kila mmoja na kukamilisha karama hiyo ya mabao.

Dodoma Jiji imepoteza mchezo wa 12 ikisalia nafasi ya saba baada ya kukusanya alama 34 ikiwa imeshinda michezo tisa hadi sasa huku ikihitaji alama tatu pekee kujihakikishia nafasi ya kushiriki Ligi Kuu ya NBC msimu ujao.

Baada ya kufunga mabao matano Azam imefikisha jumla ya mabao 48 na kushika nafasi ya tatu kwa idadi kubwa ya mabao nyuma ya Simba yenye mabao 62 na Young Africans inayoongoza ikiwa na mabao 71.

STAND, GEITA KUISAKA LIGI KUU YA NBC.

IKITAMATIKA kwa mzunguko wa 30 ligi ya Championship ya NBC na kushuhudia Mtibwa Sugar ikiibuka mabingwa wa ligi hiyo na Mbeya City kupanda daraja timu za Stand United ya Shinyanga na Geita Gold ya Geita bado zina nafasi ya kushiriki Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2025/26.

Stand iliyomaliza nafasi ya tatu kwenye msimamo wa ligi hiyo itacheza michezo ya mtoano kwenye uwanja wa nyumbani na ugenini dhidi ya Geita Gold na mshindi wa mchezo huo atacheza na timu ya Ligi Kuu ya NBC itakayopoteza mchezo wake wa mtoano.

Mchezo wa mwisho timu hizo kukutana ulikuwa mchezo wa kufunga pazia la ligi ya Championship ya NBC mzunguko wa 30 na kumalizika kwa sare ya 1-1 timu ya Stand ikiwa nyumbani kwenye uwanja wa Kambarage, Shinyanga.

Mshindi wa jumla wa michezo yote miwili atacheza na timu itakayopoteza mchezo wake wa mtoano kutoka Ligi Kuu ya NBC na endapo timu ya Championship itashinda itapanda Ligi Kuu na endapo timu ya Ligi Kuu itashinda basi itasalia kwenye ligi hiyo kwa msimu wa 2025/26.

NYASI ‘KUWAKA’ MOTO LIGI KUU YA NBC

LIGI Kuu ya NBC leo inatimua vumbi kwa michezo miwili itakayopigwa kwenye viwanja vya Sokoine, Mbeya na Kaitaba, Kagera.

Mchezo wa saa 10:00 alasiri utakuwa kati ya Tanzania Prisons dhidi ya Coastal Union ambapo Prisons inahitaji kushinda mchezo wa leo ili kujiondoa kwenye nafasi ya kucheza michezo ya mtoano.

Endapo Prisons inayoshika nafasi ya 14 itashinda itafikisha alama 30 na itakuwa nyuma ya Coastal Union inayoshika nafasi ya nane kwa tofauti ya alama moja pekee.

Mchezo wa mwisho utapigwa mkoani Kagera kwenye uwanja wa Kaitaba saa 12:30 jioni kati ya Kagera Sugar dhidi ya Mashujaa.

Kagera inayoshika nafasi ya 14 inahitaji kushinda mchezo wa leo ili kufufua matumaini ya kusalia Ligi Kuu ya NBC msimu 2025/26 huku Mashujaa ikihitaji alama tatu muhimu kujihakikishia nafasi ya kusalia kwenye ligi hiyo.

COSMOPOLITAN YAAGA NBC CHAMPIONSHIP

TIMU ya Cosmopolitan kutoka Dar es Salaam imeshuka daraja kutoka Ligi ya Championship ya NBC na kuungana na Biashara United ya Mara hivyo rasmi timu hizo zitashiriki ligi ya First League msimu wa 2025/26.

Cosmopolitan imeshuka daraja baada ya kukubali kichapo cha mabao 2-1 kutoka kwa Songea United kwenye mchezo wa mwisho wa ligi hiyo.

Timu hiyo imeshuka daraja huku ikiwa imefunga mabao machache (19) sawa na timu ya Kiluvya kutoka Dar es Salaam itakayocheza hatua ya mtoano kutafuta nafasi ya kusalia ligi ya Championship ya NBC.

Cosmopolitan imeaga ligi ya Championship ya NBC ikiwa imeshinda michezo michache (5) sawa na timu ya Transit Camp inayotafuta nafasi ya kusalia kwenye ligi hiyo endapo itashinda mchezo wake wa hatua ya mtoano dhidi ya Kiluvya.

KIVUMBI CHA LIGI KUU YA NBC KUENDELEA LEO.

IKIELEKEA siku za mwisho za msimu wa 2024/25 Ligi Kuu ya NBC inatarajiwa kuendelea leo kwa mchezo mmoja utakaokutanisha timu ya Simba itakayokuwa uwanja wa nyumbani wa KMC Complex dhidi ya Pamba Jiji kutoka Mwanza.

Simba iliyoshinda mchezo wake uliopita kwa bao moja ugenini dhidi ya JKT Tanzania inarudi uwanjani leo kucheza na Pamba Jiji iliyolazimishwa sare ya 1-1 nyumbani dhidi ya Fountain Gate.

Pamba inaingia kwenye mchezo wa leo ikiwa timu namba tatu kwa kushinda michezo michache ikishinda sita, nyuma ya Kagera iliyoshinda mitano na KenGold iliyoshinda mitatu.

Simba inaingia kwenye mchezo wa leo akiwa imepoteza mchezo mmoja pekee huku ikiwa timu iliyoruhusu mabao machache hadi sasa kwenye Ligi Kuu ya NBC ikifungwa tisa.