Author: Loveness Bernard

KAGERA SUGAR ‘HATIHATI’ KUSHIRIKI LIGI KUU YA NBC MSIMU UJAO.

MATUMAINI ya wapenzi na mashabiki wa timu ya Kagera Sugar kusalia Ligi Kuu ya NBC yamezidi kufifia baada ya kufungwa na timu ya Mashujaa katika uwanja wa Kaitaba mkoani Kagera jana kwa bao 1-0.

Timu hiyo imeshacheza michezo 28 ya Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2024/25 na kufanikiwa kuvuna alama 22 ikifunga mabao 22 na kuruhusu mabao 40 huku ikiwa imebakisha michezo miwili kumaliza msimu.

Aidha timu hiyo endapo ikishinda michezo yote iliyobakia itaweza kufikisha alama 28 ikiwa ni tofauti ya alama moja na Pamba Jiji ambayo ina alama 27 ikifunga mabao 18 na kufungwa mabao 32 huku ikiwa imebaki michezo mitatu mkononi.

Endapo Pamba Jiji itashinda mchezo wa leo dhidi ya KenGold rasmi Kagera Sugar itashuka daraja na kushiriki Ligi ya Championship ya NBC.

PRISONS YATAKATA SOKOINE LIGI KUU YA NBC

LIGI Kuu ya NBC imeendelea mkoani Mbeya ambapo timu ya Tanzania Prisons iliikaribisha timu ya Coastal Union katika uwanja wa Sokoine na kukusanya alama zote tatu baada ya ushindi wa 2-1.

Mchezo huo ulianza saa 10:00 alasiri timu zote zilionyesha ari ya kupambania alama tatu muhimu ili kuweza kujiweka katika mazingira ya kusalia Ligi Kuu ya NBC msimu ujao.

Iliwachukua dakika 27 timu ya Tanzania Prisons kufungua ukurasa wa mabao kupitia mchezaji wao Ezekia Mwashilindi hivyo kuifanya timu hiyo kwenda mapumziko ikiwa inaongoza kwa 1-0.

Kipindi cha pili kilianza ambapo Coastal Union walionekana kuliandama zaidi lango la Prisons hata hivyo juhudi zao zilizimwa na mchezaji Beno Ngasa aliyeongeza bao la pili kwa timu yake dakika ya 74.

Dakika ya 89 Coastal Union ilipata bao la kufutia machozi kupitia mchezaji wao Bakari Msimu hivyo mchezo kutamatika kwa matokeo ya 2-1.

Tanzania Prisons ipo nafasi ya 11 kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC ikiwa imevuna alama 30 katika michezo 28 huku Coastal Union ikiwa nafasi ya 9 na alama 31 katika michezo 28 ya Ligi Kuu msimu wa 2024/2025.

CAMARA MKALI WA ‘HATI SAFI’ LIGI KUU YA NBC.

GOLIKIPA wa timu ya Simba, Moussa Camara ameendeleza moto wake wa kuongoza kwa kuwa na hati safi nyingi kuliko magolikipa wengine wa timu za Ligi Kuu ya NBC akiwa hajaruhusu bao kwenye michezo 16 akiwa kwenye msimu wa kwanza ndani ya Simba.

Camara mpaka sasa amecheza michezo 24 sawa na dakika 2160 huku timu yake ya Simba ikiwa nafasi ya pili kwenye msimamo nyuma ya Young Africans inayoshikilia usukani.

Golikipa wa Young Africans,Djigui Diarra anafuatia akiwa amecheza dakika 1819 katika michezo 20 ya Ligi Kuu ya NBC amefanikiwa kukusanya hati safi 14.

Patrick Munthali wa timu ya Mashujaa kutoka Kigoma anashika nafasi ya tatu akiwa amefanikiwa kukusanya hati safi 12 huku Mohamed Mustapha wa timu ya Azam akishika nafasi ya nne na hati safi 10.

Nafasi ya tano inashikiliwa na Yona Amos wa Pamba Jiji aliyefanikiwa kukusanya hati safi tisa huku Yakoub Suleiman wa JKT Tanzania amekusanya hati nane akishika nafasi ya sita.

Metacha Mnata wa Singida Black Stars na Ngaleka Katembua wa Dodoma Jiji wanafunga orodha wakifanikiwa kukusanya hati safi saba kila mmoja.

AHOUA MKALI WA ‘KUCHEKA NA NYAVU’ LIGI KUU YA NBC.

KIUNGO wa timu ya Simba Jean Ahoua ameendelea kujiimarisha kwenye mbio za ufungaji bora baada ya kufikisha mabao 15 ikiwa ni msimu wake wa kwanza tangu ajiunge na timu hiyo kwenye Ligi Kuu ya NBC.

Ahoua amefanikiwa kufunga mabao hayo akiwa amecheza mechi 24 kwa jumla ya dakika 1773 katika Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2024/2025.

Clement Mzize wa Young Africans anafuata akiwa amefanikiwa kufunga mabao 13 huku mchezaji mwenzake Prince Dube wa timu hiyo akifanikiwa kucheka na nyavu za wapinzani wao mara 12 sawa na Leonel Ateba wa Simba.

Steven Mukwala wa Simba na Jonathan Sowah wa Singida Black Stars wamefanikiwa kufunga mabao 11 kila mmoja huku Elvis Rupia wa Singida Black Stars akitupia nyavuni mabao 10.

SIMBA ‘YAIBAMIZA’ KMC LIGI KUU NBC

LIGI Kuu ya NBC imeendelea leo kwa mchezo mmoja uliochezwa uwanja wa KMC Complex, mkoani Dar es Salaam kati ya KMC ikiikaribisha timu ya Simba na kushuhudia ‘Mnyama’ akishinda 1-2 ugenini.

Mchezo huo ulianza majira ya saa kumi alasiri kwa timu zote kuwa na ari ya kuzitaka alama tatu muhimu KMC ikitaka kujihakikishia nafasi ya kusalia Ligi Kuu ya NBC msimu ujao huku Simba ikijiimarisha kwenye mbio za ubingwa.

Dakika nane ziliitosha timu ya KMC kufungua ukurasa wa mabao kupitia kwa Rashid Chambo kabla ya timu ya Simba kusawazika kupitia mshambuliaji wake Steven Mukwala dakika ya 15 ya mchezo na dakika 46 aliongeza bao la pili hivyo mchezo kumalizika kwa 1-2.

Simba imefikisha alama 69 ikiwa nafasi ya pili kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC ikifunga mabao 62 na kuruhusu mabao 11 katika michezo 26 ambayo timu hiyo imecheza huku KMC ikiwa nafasi ya 11 na alama 30 ikifunga mabao 23 na kuruhusu mabao 41 katika michezo 27 ambayo timu hiyo imeshacheza.