Author: Loveness Bernard

AHOUA HAKAMATIKI LIGI KUU NBC

Kiungo wa Simba Jean Ahoua amekuwa tishio katika Ligi Kuu ya NBC baada ya kuchangia mabao 9 kati ya 21 ambayo timu yake ya Simba imefunga katika mizunguko 10 iliyocheza.

Ahoua ambaye amesajiliwa na Simba mwanzoni mwa msimu huu amefanikiwa kufunga mabao matano katika Ligi Kuu na kuhusika katika pasi nne zilizozaa mabao.

Mchezaji huyo pia amefanikiwa kuchukua tuzo ya mchezaji bora wa mwezi Agosti na pia amechukua tuzo mbili za mchezaji bora wa mechi kati ya Simba na Fountain Gate baada ya kufunga bao moja na kutoa pasi ya mwisho moja na mchezo kati ya Simba na KMC alipofunga mabao mawili hivyo kuchangia ushindi wa mabao manne ilioupata timu yake.

Ligi Kuu ya NBC inazidi kushika kasi ambapo mpaka sasa timu nyingi zimekuwa zikileta ushindani na upinzani mgumu jambo linalodhihirisha ubora wa Ligi hii

SIMBA YAITOLEA UVIVU KMC.

LIGI Kuu ya NBC iliendelea jana kwa mchezo mmoja uliochezwa katika Uwanja wa KMC, Dar es Salaam Simba waliwakaribisha KMC majira ya saa 10 alasiri na kufanikiwa kushinda 4-0.

Awesu Awesu alifungua ukurasa wa mabao dakika 25 ya mchezo huo baada ya kupokea mpira kutoka kwa mshambuliaji wa timu hiyo Steven Mukwala hivyo kuiweka mbele timu yake ya Simba.

Dakika ya 38 ya mchezo Jean Ahoua alifanikiwa kuipatia timu yake bao la pili kwa mkwaju wa penati baada ya mchezaji wa KMC, Raheem Shomari kufanya faulo kwa Shomari Kapombe hivyo Simba kwenda mapumziko wakiwa mbele kwa mabao 2-0.

Baada ya mapumziko mchezo uliendelea kwa timu zote mbili kushambuliana kwa kasi na dakika ya 66 Edwin Balua alifanikiwa kuiongezea timu yake bao la tatu akipokea pasi kutoka kwa Valentin Nouma huku bao la mwisho likifungwa na Jean Ahoua dakika ya 69 ya mchezo huo na kuchaguliwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo.

Ligi Kuu ya NBC itaendelea katika Uwanja wa Azam Complex ambapo Yanga watawakaribisha timu ya Tabora United mchezo utakaochezwa saa 12 jioni.

PAMBA JIJI YAONJA RAHA YA USHINDI, SIMBA, KMC HAPATOSHI LEO.

Ligi Kuu ya NBC jana iliendelea kwa mchezo mmoja uliochezwa katika Uwanja wa Tanzanite Kwaraa mkoani Manyara ambapo Fountain Gate waliwakaribisha timu ya Pamba Jiji kutoka Mwanza.

Iliwachukua dakika 28 Fountain Gate kufungua ukurasa wa mabao kupitia mchezaji wake Ellie Makono ambapo dakika ya 34 Pamba Jiji waliweka mzani sawa kwa kupata bao kupitia mchezaji wake James Mwashinga kabla ya kuongeza bao la pili katika dakika ya 45 ya mchezo huo kupitia mchezaji Salehe Masoud hivyo kwenda mapumziko wakiwa wanaongoza.

Kipindi cha pili kilianza kwa timu zote kushambuliana na dakika ya 85 ya mchezo huo mchezaji Ally Ramadhan aliiongezea Pamba Jiji bao la 3 hivyo kuifanya timu hiyo kupata ushindi wao wa kwanza tangu kupanda Ligi kuu ya NBC huku wakiwa wamecheza michezo 11.

Ligi Kuu ya NBC itaendelea leo mkoani Dar es Salaam ambapo timu ya Simba itakuwa mwenyeji wa KMC katika Uwanja wa KMC Complex, uliopo Mwenge majira ya alasiri.

KARIA AZITAKA KLABU LIGI KUU KUTOKA NA AZIMIO MOJA

Rais wa Shirikisho la Soka nchini (TFF), Wallace Karia amezitaka klabu za Ligi Kuu ya NBC kutoka na azimio moja mara baada ya mafunzo ya Weledi katika Uendeshaji wa klabu nchini kwa Watendaji Wakuu na Wenyeviti wa Klabu.

Akizungumza wakati wa kufunga mafunzo hayo Karia amesema kuwa Klabu zinapaswa kuwa na azimio moja kwa ajili ya ustawi wa soka letu hususani kwa upande wa matangazo wanayopata klabu.

“Ligi yetu imekua sana tunapaswa tuwe na azimio moja mfano kuhusu matangazo yanayoonekana wakati wa mechi zetu yanapaswa kuzinufaisha klabu zetu na sio wale wanaoandaa mabango hayo”alisema Karia na kuongeza,

“FIFA wameleta mafunzo haya kwa wakati muafaka nawashukuru sana natazamia kukaa na Bodi ya Ligi Kuu ili kuona namna ya kuongeza uwepo wa mafunzo kama haya kwa manufaa ya taifa letu na vizazi vijavyo vya soka hususani katika masuala ya utawala bora katika klabu za soka” alisema Karia.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Ligi, Steven Mnguto amewashukuru FIFA kwa mafunzo waliyopata kwani klabu nyingi zitanufaika na ujuzi waliopata.

“Nawashukuru sana FIFA sisi kama Klabu za Tanzania tumenufaika kwa hizi siku mbili na tunatamani tupate muda mwingi zaidi kuwa nanyi” alisema Mnguto.

Mafunzo hayo ya siku mbili yaliyoandaliwa na FIFA wakishirikiana na TFF na Bodi ya Ligi yamefanyika Dar es Salaam katika hoteli ya Johari Rotana.

MTINE, POPAT WAFUNGUKA SEMINA YA FIFA UENDESHAJI KLABU NCHINI.

Watendaji Wakuu wa Klabu za Yanga na Azam wameshukuru Shirikisho la Soka Duniani (FIFA) wakishirikiana na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) Pamoja na Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) kwa kuandaa semina ya siku mbili jijini Dar es salaam kuhusu Weledi katika Uendeshaji wa klabu nchini kwa Watendaji Wakuu na Wenyeviti wa Klabu zinazoshiriki Ligi Kuu ya NBC.

Akizungumza katika semina hiyo Mtendaji Mkuu wa Yanga Andre Mtine amesema kuwa semina hii ni muhimu kwani elimu haina mwisho na itawezesha viongozi wa klabu kutambua namna nzuri ya kuendesha klabu.

“Elimu ni jambo la muhimu kwa kila mtu na haina mwisho iwe kijana ama mzee bado anapaswa kujifunza hii ni nzuri kwetu kwani tunajifunza namna ya kuendesha klabu zetu kwa manufaa ya Ligi yetu ya NBC” Alisema Mtine.

Kwa upande waka Mtendaji Mkuu wa Azam Abdulkarim Amin ‘Popat’ amesema kuwa anashukuru kwa kupata fursa hii adimu kutoka FIFA wakishirikiana na TFF Pamoja na Bodi ya Ligi kwani itawajengea ujuzi na uzoefu mpya kwenye tasnia ya mpira.

“Nashukuru FIFA, TFF na Bodi ya Ligi kwa kuja na semina hii kwani ni fursa adimu naamini itatujengea uwezo na kutupa ujuzi mpya sisi kama watendaji wakuu wa klabu za Ligi Kuu ya NBC na kama Azam tunaahidi kwenda kufanyia kazi tulichojifunza na tutaenda kuwafundisha waliopo chini yetu ili nao wanufaike na haya”alisema Popat.