Category: STORY

PRISONS WABABE WA MBEYA DABI LIGI KUU YA NBC

Mchezaji wa Mbeya City (kushoto) akichuana na mchezaji wa Tanzania Prisons

TIMU ya Tanzania Prisons imeendeleza ubabe wake katika mchezo wa dabi ya Jiji la Mbeya baada ya kuifunga timu ya Mbeya City mabao 2-1 katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC uliochezwa Uwanja wa KMC mkoani Dar es Salaam jana Oktoba 21.

Mchezo huo ulianza majira ya saa 10:00 alasiri ambapo timu zote zilikuwa zikipambana kupata alama tatu huku mashabiki wa timu zote mbili wakionekana kushangilia kwa bendi na ngoma zilizonogesha mchezo huo.

Mbeya City kinara wa Ligi Kuu ya NBC alianza mchezo kwa kushambulia sana lango la ‘hasimu’ wake huku Tanzania Prisons ikifanya mashambulizi ya kushtukiza na hadi timu zinaenda mapumzikoni hakuna aliyekuwa ametikisa ‘nyavu’ za mwenzake hivyo kuwapa kazi ya ziada makocha wakati wa mapumziko namna bora ya kujipanga kwa ajili ya kipindi cha pili.

Dakika ya 73 kipindi cha pili Tanzania Prisons ilipata bao la kwanza kupitia kwa Jeremiah Juma na dakika moja baadae Haruni Chanongo aliiongezea bao la pili na kufifisha matumaini ya Mbeya City kubakiza alama zote tatu nyumbani.

Tanzania Prisons wakishangilia

Dakika ya 87 Mbeya City ilipata bao la kufutia machozi kupitia kwa Daniel Lukandamila hivyo mchezo kutamatika kwa Mbeya City kupoteza 1-2 na kuifanya ‘Purple Nation’ kupoteza mchezo wa kwanza wa Ligi Kuu ya NBC msimu huu.

Mchezaji wa Tanzania Prisons, Jeremiah Juma alitangazwa kuwa mchezaji bora wa mchezo kutokana na kiwango kizuri alichokionyesha ikiwa ni pamoja na kuwafungia ‘Wajelajela’ bao na kuonyesha kiwango kizuri akiisaidia timu yake kushinda.

Jeremiah Juma

Matokeo hayo yanaifanya Tanzania Prisons kupanda hadi nafasi ya tano ikiwa na alama sita huku Mbeya City ikiendelea kushikilia ‘usukani’ wa Ligi Kuu ya NBC ikiwa na alama saba.

MBEYA DERBY NDANI YA DAR LIGI KUU YA NBC.

LIGI Kuu ya NBC inatarajiwa kushuhudia mchezo kati ya Mbeya City na Prisons (Mbeya Derby) kwenye uwanja wa KMC Complex kwa mara ya kwanza ukipigwa mkoani Dar es Salaam huku timu zote asili yake ikiwa ni mkoani Mbeya.

Hii inatokea baada ya timu ya Mbeya City kuuchagua uwanja wa KMC kama uwanja wake wa nyumbani badala ya uwanja Sokoine uliofungiwa na kamati ya ukaguzi kupisha marekebisho.

Mara ya mwisho timu hizo kukutana ilikuwa Disemba 25, 2022 na Tanzania Prisons kuibuka na ushindi wa mabao 2-1 huku mchezo wa mzunguko wa kwanza msimu huo ukimalizika kwa sare ya bao moja.

Mbeya City inayoongoza msimamo wa Ligi Kuu ya NBC hadi sasa ikiwa na alama saba baada ya kushinda michezo miwili, sare mmoja na kupoteza mmoja inakutana na ‘Wajelajela’ Prisons walioshinda mchezo mmoja pekee na kupoteza miwili huku wakikamata nafasi ya 13 kwenye msimamo.

Mchezaji wa Mbeya City Soudy Dondola amesema kuwa mchezo wao dhidi ya Prisons utakuwa mgumu lakini wamejipanga vizuri kuhakikisha wanapata matokeo mazuri na kuwapa furaha mashabiki wa Mbeya City.

“Morali ni ya kutosha kuelekea mchezo wetu, tunatambua ni mchezo muhimu sana kwetu kupata ushindi ili tuwe na muendelezo mzuri wa msimu. Alisema Soudy.

Nae Dotto Shabani wa Tanzania Prisons amesema wamejipanga vizuri kuendeleza ubabe dhidi ya Mbeya City ingawa haiwezi kuwa kazi nyepesi wao kufanya hivyo.

” Kiu yetu kubwa ni kuifunga Mbeya City na kuendeleza ubabe dhidi yao ingawa mchezo lazima utakuwa mgumu kutokana na wapinzani wetu kuanza msimu vizuri na wakiwa vinara hadi sasa.” alisema Dotto.

Mchezo huo utaanza saa 10:00 alasiri na kuonyeshwa mbashara kwenye chaneli ya  Azam Sports huku matangazo ya redio yakirushwa moja kwa moja na kituo cha TBC.

NBC CHAMPIONSHIP KUANZA KUTIMUA VUMBI LEO

LIGI ya NBC Championship inatarajiwa kuanza kutimua vumbi leo kwa michezo miwili kupigwa kwenye mikoa ya Kagera na Arusha.

Majira ya saa 10:00 alasiri Kagera Sugar iliyoshuka daraja kutoka Ligi Kuu ya NBC inatarajiwa kucheza karata yake ya kwanza leo kwenye uwanja wa Kaitaba, Kagera dhidi ya Transit Camp ili kutafuta nafasi ya kurejea kwa mara nyingine ligi hiyo.

Timu hiyo ‘inayonolewa’ na mchezaji wa zamani wa Taifa Stars (Tanzania) Juma Kaseja imedhamiria kufanya vizuri msimu huu ikiwa imesajili wachezaji wenye uzoefu na waliocheza Ligi Kuu ya NBC wakiwemo Andrew Vicent (Chikupe), Joseph Mahundi, Fredy Tangalo na Hassan Mwaterema.

Kwenye uwanja wa Sheikh Amri Abeid, Arusha timu ya Mbuni itakuwa mwenyeji wa Mbeya kwanza ya Mtwara saa 10:00 alasiri.

Mbuni iliyomaliza nafasi ya tisa kwenye msimamo wa ligi ya NBC ya Championship inatarajia kuivaa Mbeya Kwanza iliyomaliza nafasi ya saba ikishindwa kucheza hatua ya mtoano msimu uliopita kwa tofauti ya alama sita pekee.

Ligi ya NBC Championship inatarajiwa kupata bingwa mpya msimu huu baada ya bingwa mtetezi timu ya Mtibwa Sugar kupanda Ligi Kuu ya NBC na hivyo kushindwa kutetea ubingwa wake.

Chaneli ya Fifa Plus itaonyesha mchezo kati ya Mbuni na Mbeya Kwanza moja kwa moja na itaendelea kufanya hivyo kwenye michezo mingine ya Ligi ya Championship ya NBC msimu wa 2025/26.

Simba Kileleni

SIMBA YAPAA KILELENI, JKT, AZAM ZATOSHANA NGUVU LIGI KUU YA NBC

TIMU ya Simba imepaa kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu ya NBC baada ya kuichapa timu ya Namungo mabao 3-0 kwenye mchezo uliochezwa uwanja wa Mkapa, Dar es Salaam.

Simba ilifanikiwa kupata bao la kuongoza dakika mbili kabla ya kipindi cha kwanza kutamatika kupitia kwa Karaboue Chamou kwa kichwa baada ya mpira wa kona uliopigwa na Joshua Mutale.

SIMBA VS NAMUNGO
SIMBA VS NAMUNGO

Dakika ya 61 Rushine De Reuck aliiandikia Simba bao la pili kwa pasi ya mpira uliokufa iliyopigwa na raia mwenzake wa Afrika Kusini Neo Maema.

Dakika ya 83 Mtanzania Selemani Mwalimu alifungua akaunti yake ya mabao kwenye Ligi Kuu ya NBC baada ya mabeki wa Namungo kushindwa kuokoa mpira kwenye eneo lao.

Kocha wa Namungo Juma Mgunda alisema timu yake ilizidiwa kimbinu na ukomavu hivyo watajifunza ili kujiimarisha na michezo ijayo.

” Tumejifunza, kuna wachezaji wadogo ambao wapo kwenye timu yangu wameona namna ya kucheza na timu kubwa hivyo hili ni funzo kwetu wakati mwingine tutafanya vizuri” Alisema Mgunda.

Rushine De Reuck mlinzi wa timu ya Simba alichaguliwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo akifunga bao na kumaliza mchezo huo bila kuruhusu bao huku ikiwa mchezo wa pili mfululizo kwa Simba kucheza bila kuhurusu bao. 

JKT TANZANIA VS AZAM FC

Mchezo wa mapema uliopigwa saa 12:00 jioni uliozikutanisha timu za JKT Tanzania na Azam kwenye uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo uliopo mkoani Dar es Salaam na kushuhudia zikitoka sare ya bao moja.

Azam ilikuwa ya kwanza kuandika bao kupitia kwa kinara wa pasi za mabao msimu wa 2024/25 Feisal Salum dakika ya 42 lililosimama hadi mapumziko na kuwafanya ‘Maafande’ wa JKT Kwenda mapumziko vichwa chini.

JKT TANZANIA VS AZAM FC
JKT TANZANIA VS AZAM FC

Kipindi cha pili JKT ilirudi imara na dakika ya 90 Paul Peter aliisawazishia kwa mpira wa kichwa uliomshinda golikipa wa Azam Issa Fofana.

Paul Peter wa JKT Tanzania alichaguliwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo kutokana na kiwango kizuri alichokionyesha ikiwa ni Pamoja na kuisaidia timu yake kupata bao la kusawazisha na kuendeleza rekodi ya mchezo wa tatu bila kupoteza.

AZAM,JKT

AZAM, JKT HAPATOSHI ISAMUHYO, SIMBA IKIIKARIBISHA NAMUNGO LIGI KUU YA NBC.

MZUNGUKO wa tatu wa Ligi Kuu ya NBC unaendelea leo mkoani Dar es salaam katika viwanja viwili vya Meja Jenerali Isamuhyo na uwanja wa Benjamin Mkapa.

Katika mchezo wa kwanza utakaochezwa Isamuhyo majira ya saa kumi na mbili jioni timu ya JKT Tanzania inayonolewa na kocha Ahmad Ally itakuwa mwenyeji wa Azam iliyo chini ya Florent Ibenge.

JKT Tanzania

JKT inashika nafasi ya nne katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC ikiwa imekusanya alama nne baada ya kushinda mchezo mmoja dhidi ya Coastal Union na kutoka sare na Mashujaa huku timu ya Azam ikishika nafasi ya tisa baada ya kukusanya alama tatu kwenye mchezo mmoja iliyocheza dhidi ya Mbeya City.

Mchezo wa pili ni kati ya Simba na Namungo utakaopigwa majira ya saa 2:15 usiku ukiwa ni mchezo wa mwisho wa kukamilisha mzunguko wa tatu.

 

Simba SC

 

Simba iliyo chini ya kocha Selemani Matola inashika nafasi ya nane katika msimamo ikikusanya alama tatu katika mchezo wao pekee waliocheza dhidi ya Fountain Gate.

Namungo FC

Namungo ambayo haijapoteza mchezo wowote hadi sasa chini ya kocha Juma Mgunda inakamata nafasi ya tano ikiwa na alama nne baada ya kutoka sare na timu ya Pamba Jiji huku ikiifunga timu ya Tanzania Prisons.