Category: STORY

Ratiba ya Ligi Kuu ya NBC 2025/2026

TAARIFA YA MCHEZO WA TRA DHIDI YA SIMBA.

BODI ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) inautaarifu umma kuwa mchezo namba saba (7) wa Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2025/2026 (TRA United FC vs Simba SC), utafanyika kwenye uwanja wa Sheikh Amri Abeid jijini Arusha Aprili 9, 2026 kuanzia saa 10:00 alasiri.

Aidha, Bodi inatoa taarifa kuwa mashabiki wote ambao walinunua tiketi kwa ajili ya mchezo huo ambao uliahirishwa Machi 14, 2026 baada ya mvua kubwa kunyesha jijini Arusha na kusababisha uwanja kukosa sifa za kisheria, watatumia tiketi hizo kuingia uwanjani katika mchezo wa Aprili 9, 2026, ambapo shabiki atalazimika kuwa na kadi (N-CARD) ambayo aliitumia kununua tiketi ya mchezo ulioahirishwa, kwa ajili ya uhakiki getini.

Tayari wauzaji wa tiketi za mchezo huo, National Internet Data Center (NIDC) wamerejesha tiketi zote zilizonunuliwa, kwenye kadi za mashabiki hao bila kujali shabiki alikuwa ameshaingia uwanjani ama hakuingia kabisa, na kwamba mashabiki hao hawatapaswa kununua tena tiketi.Tiketi ambazo ziliuzwa katika mchezo huo ni VVIP 95, VIP 567 na Mzunguko 3,215.

Bodi inawakumbusha mashabiki ambao hawakununua tiketi kwenye mchezoulioahirishwa, kuwa tiketi zinapatikana (zinauzwa) kwenye vituo vya N-CARD vya kuuzia tiketi na kupitia mitandao ya simu kwa gharama zifuatazo; VVIP – 50,000, VIP (Wing A & B) – 30,000 na Mzunguko – 10,000

Bodi ya Ligi inawashukuru sana mashabiki wa mpira wa miguu kwa ushirikiano mkubwa wanaoendelea kuutoa kwa Bodi na klabu zake, ikiwemo kununua tiketi na kuingia viwanjani kuziunga mkono klabu zetu.

Imetolewa na;

Idara ya Habari na Mawasiliano

Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB)

SINGIDA KUIKARIBISHA KMC, PAMBA, YOUNG AFRICANS KUKIPIGA KIRUMBA.

LIGI Kuu ya NBC itaendelea leo kwa michezo miwili itakayopigwa kwenye viwanja vya Airtel mkoani Singida ambapo Singida Black Stars itaialika KMC na CCM Kirumba mkoani Mwanza timu ya Pamba Jiji itaikaribisha timu ya Young Africans.

Wachezaji wa Singida Black Stars wakishangilia.

Michezo hiyo ni muhimu kwa timu zote kutokana na namna Ligi hiyo inavyozidi kupamba moto, Singida Black Stars iliyopo nafasi ya sita inacheza majira ya saa nane mchana huku ikiwa imeshinda michezo saba sare nne na kufungwa michezo sita huku ikikusanya alama 25.

DARUESHI SALIBOKO - KMC
DARUESHI SALIBOKO – KMC

Kwa upande wa KMC inashika nafasi ya mwisho (16) katika msimamo ikicheza michezo 17 na kushinda miwili, sare mbili na kufungwa 13 huku ikikusanya alama 8.

Wachezaji wa Pamba Jiji wakishangilia.

Mchezo wa pili ni muhimu kwa Pamba Jiji ikitaka kuendeleza rekodi ya kutokufungwa mchezo wowote katika uwanja wao wa nyumbani katika michezo tisa timu hiyo imeshinda michezo mitano na sare nne huku Young Africans ikitaka kuendeleza kukusanya alama ili iwe katika nafasi nzuri ya kutetea ubingwa wa Ligi Kuu ya NBC.

Pamba ambayo iPo nafasi ya tano katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC imecheza michezo 17 ikishinda michezo sita sare nane na kufungwa michezo mitatu huku ikiweza kukusanya alama 26.

Wachezaji wa Young Africans.

Kwa upande wa Young Africans ipo nafasi ya kwanza katika msimamo ikiwa imecheza michezo 17 kushinda michezo 12 na sare tano huku ikiwa imekusanya alama 41.

MZIZIMA DERBY KUNOGESHA LIGI KUU YA NBC LEO.

MACHO na masikio ya mashabiki wa soka Tanzania leo yataelekezwa Azam Complex, Chamazi, ambapo vigogo wa Dar es Salaam, Azam na Simba watakutana katika pambano kubwa linalojulikana kama Mzizima Derby.

Mchezo huu unasubiriwa kwa hamu kubwa kutokana na ushindani wa kihistoria wa timu hizi mbili na umuhimu wake kwenye mbio za juu ya msimamo wa Ligi Kuu ya NBC.

Azam FC wanaingia kwenye mchezo huu wakiwa na morali kubwa baada ya ushindi wao wa mabao 2-1 dhidi ya Singida Black Stars, huku Simba SC nao wakija na kujiamini kufuatia ushindi wa 2-0 walioupata dhidi ya Coastal Union katika mchezo wao uliopita.

Hali hiyo inafanya mechi ya leo kutabirika kuwa ya ushindani mkali, presha kubwa na vita ya mbinu kutoka makocha na mabenchi ya ufundi ya timu zote.

Kwa upande wa msimamo, Simba wanaonekana kuwa na presha ya kutafuta ushindi ili kuendelea kusogea karibu na kileleni, wakati Azam wakitaka kutumia faida ya kucheza nyumbani kuimarisha nafasi yao kwenye timu za juu.

Hii si mechi ya kawaida, bali ni mchezo wenye uzito wa alama tatu ambazo zinaweza kubadili kabisa sura ya mbio za ubingwa wa Ligi Kuu ya NBC msimu huu.

Historia ya timu hizi imekuwa na ushindani wa hali ya juu, huku Simba mara nyingi wakiwa na rekodi nzuri zaidi kwenye mechi zao za ligi dhidi ya Azam.

Hata hivyo, Azam walionyesha ubora kwenye mchezo wa mzunguko wa kwanza baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 2-0 yaliyofungwa na Japhte Kitambala ma Iddy Seleman jambo ambalo linaifanya Simba kuingia leo wakiwa na kiu ya kulipa kisasi mbele ya mashabiki wao ugenini.

Kinachoongeza ladha zaidi ni ubora wa vikosi vya timu zote mbili ambapo Simba wanaingia na nguvu ya safu yao ya ushambuliaji pamoja na uzoefu mkubwa wa mechi za presha, wakati Azam wana kikosi chenye nidhamu ya kiufundi na uwezo mkubwa wa kumiliki mpira, jambo linaloweza kufanya mchezo huu kuamuliwa kwa makosa madogo sana.

Kwa kifupi, leo Chamazi kutakuwa hapatoshi. Ni mechi ya heshima, pointi na tambo za Dar es Salaam. Mashabiki wanatarajia kuona soka la kiwango cha juu, mabao, kasi na ‘udambwi’ wa derby halisi ya Mzizima.

Wakati huo huo mkoani Arusha kwenye uwanja wa Sheikh Amri Abeid timu ya TRA itaialika Singida Black Stars kwenye mchezo wa mapema saa 10:00 alasiri ikiwa ni sambamba na mchezo wa Mzizima Derby utakaopigwa usiku.

YOUNG AFRICANS YAPAA KWA KISHINDO, NAMUNGO, MASHUJAA ZABANWA NYUMBANI LIGI KUU YA NBC.

Mzunguko wa Ligi Kuu ya NBC uliendelea kwa michezo mitatu iliyotoa burudani, ushindani mkubwa na matokeo yenye athari kwenye msimamo wa ligi hiyo huku Young Africans ikiendelea kuonyesha ubora wake kwa ushindi mnono wa mabao 3-0 na kuwa timu pekee iliyopata matokeo ya ushindi kwa siku ya jana.

Katika mchezo uliovuta hisia za mashabiki wengi, Young Africans iliitandika Tanzania Prisons mabao 3-0 katika mechi ambayo mabingwa hao watetezi walionyesha tofauti mkubwa wa ubora kuanzia dakika za kwanza hadi mwisho.

Baada ya kipindi cha kwanza kumalizika bila mabao Young Africans ilirejea kwa kasi kubwa kipindi cha pili na kufungua pazia dakika ya 50 kupitia kwa Allan Okello raia wa Uganda aliyemalizia vizuri krosi ya Israh Mwenda.

Dakika ya 68 Mudathir Yahya aliandika bao la pili kabla ya Pacome Zouzoua kuweka msumari wa mwisho dakika ya 86 na kufanya matokeo kuwa 3-0 huku golikipa wa Young Africans Abutwalib Mshery akiondoka bila kuruhusu bao.

Ushindi huo unaendelea kuipa Yanga nguvu kubwa katika mbio za ubingwa ikifikisha alama 41 huku ukiweka presha kwa wapinzani wao wa karibu kwenye kilele cha msimamo.

Katika mchezo mwingine uliokuwa na ushindani mkali, Namungo ililazimishwa sare ya mabao 2-2 na JKT Tanzania kwenye mechi iliyokuwa na mabadiliko ya mara kwa mara ya matokeo.

Namungo walikuwa wa kwanza kupata bao kupitia Jacob Masawe dakika ya 25, kabla ya JKT Tanzania kusawazisha kupitia Salehe Karabaka dakika ya 66.

Namungo walionekana kurudi mchezoni tena baada ya Herbert Lukindo kufunga bao la pili dakika ya 63 lakini JKT Tanzania hawakukata tamaa na walipata bao muhimu la kusawazisha kupitia Valentino Mashaka dakika ya 90+4 bao lililozima furaha ya wenyeji na kuwafanya wagawane alama muhimu.

Katika mechi ya tatu timu ya Mashujaa na Pamba Jiji walitoka sare tasa ya 0-0 matokeo ambayo yanaonyesha jinsi timu zote zilivyokuwa na tahadhari kubwa zaidi kuliko hatari langoni.

Licha ya kila upande kupata nafasi chache za kufunga umakini wa safu za ulinzi na makipa ulifanya mchezo huo kumalizika bila mshindi.

Kwa ujumla, mechi za jana zimeendelea kuongeza joto la Ligi Kuu ya NBC hasa katika mbio za ubingwa na vita ya kujiokoa mkiani.

Ushindi wa Young Africans unaendelea kuwatengenezea mazingira mazuri ya kutetea taji lao, wakati sare za Namungo na Mashujaa zinaacha maswali kwa timu hizo kuhusu uwezo wao wa kutumia vyema mechi za nyumbani.

Kadri ligi inavyozidi kuelekea mwisho, kila alama imekuwa ya thamani kubwa, na matokeo ya jana ni ishara kuwa ushindani bado ni mkali sana katika kila nafasi ya msimamo.

MASHUJAA, YOUNG AFRICANS, NAMUNGO, VITANI LEO LIGI KUU YA NBC.

VIWANJA vitatu vya Ligi Kuu NBC vinaendelea kutoa burudani leo kwa ratiba ya michezo mitatu inayotarajiwa kuwa na ushindani mkubwa huku kila timu ikihitaji alama kwa malengo tofauti msimu huu.

Macho mengi yataelekezwa katika viwanja vya Lake Tanganyika, Kigoma, KMC Complex, Dar es Salaam na Majaliwa, Lindi ambako mapambano ya kibingwa yanayohusisha vita ya nafasi za juu pamoja na presha ya kushuka daraja kupamba moto.

Katika mchezo wa mapema utakaochezwa saa 10:00 jioni kwenye Uwanja wa Lake Tanganyika, Mashujaa FC watawakaribisha Pamba Jiji kwenye mechi inayobeba uzito mkubwa kwa timu zote mbili.

Mashujaa wakiwa nyumbani watataka kutumia faida ya mashabiki wao kutafuta ushindi muhimu baada ya kushindwa kupata matokeo mchezo uliopita dhidi ya Fountain Gate huku Pamba Jiji wakisaka matokeo chanya yatakayowaweka kwenye nafasi salama zaidi kwenye msimamo wa ligi.

Mechi hii inatarajiwa kuwa ya nguvu nyingi katikati ya uwanja kutokana na timu zote kupenda kucheza kwa presha huku wakitumia zaidi viungo wa kati kuliko viungo wa pembeni.

Mchezo mwingine mkubwa wa leo utakuwa kati ya Young Africans watakapowakaribisha Tanzania Prisons katika uwanja wa KMC Complex, Dar es Salaam saa 12:30 jioni.

Young Africans wakiwa kwenye mbio za kuwania ubingwa hawana nafasi ya kupoteza alama na ushindi wa leo unaweza kuongeza presha kwa wapinzani wao kwenye kilele cha msimamo.

Tanzania Prisons nao wanakuja na morali ya kutafuta matokeo ya kushtua wakifahamu kupata alama dhidi ya timu kubwa kunaweza kubadili kabisa mwenendo wao wa msimu huu.

Usiku wa leo saa 3:00 usiku timu ya Namungo FC itawakaribisha JKT Tanzania kwenye uwanja wa Majaliwa katika pambano jingine linalosubiriwa kwa hamu.l kukamilisha burudani za siku ya leo.

Namungo wamekuwa timu ngumu sana inapocheza nyumbani jambo linalowapa nguvu dhidi ya JKT Tanzania ambao nao mara nyingi huonekana kuwa na nidhamu kubwa ya kiuchezaji chini ya kocha Ahmad Ally ambaye pia ni kocha msaidizi wa timu ya Taifa ya Tanzania.

Hii inaweza kuwa moja ya mechi ngumu zaidi ya leo kutokana na ubora unaokaribiana kwa pande zote mbili.

Kwa ujumla, ratiba ya leo inaweza kuleta mabadiliko makubwa kwenye msimamo wa ligi hasa kwa timu zinazowania ubingwa, nafasi za juu na zile zinazokwepa hatari ya kushuka daraja.

Mashabiki wanatarajia kuona mabao, ushindani mkali na matokeo yatakayoongeza joto la NBC Premier League kuelekea hatua za mwisho za msimu huku kila timu ikitaka kumaliza kwa furaha na mafanikio.