Category: STORY

DODOMA JIJI, MBEYA CITY ZAWASHA MOTO LIGI KUU YA NBC.

LIGI Kuu NBC imeendelea jana kwa michezo miwili iliyotoa burudani ya viwango ambapo Dodoma Jiji iliichapa Fountain Gate mabao 3-0, huku Mbeya City ikiibuka na ushindi wa kusisimua wa 3-2 dhidi ya KMC.

Katika mchezo uliopigwa Airtel Stadium, Singida, wenyeji Dodoma Jiji walionyesha ubora mkubwa hasa kipindi cha pili na kuondoka na alama tatu muhimu mbele ya Fountain Gate baada ya kipindi cha kwanza kumalizika wakiwa kifua mbele kwa bao moja kupitia kwa nahodha Augustino Nsata aliyefunga dakika ya 38.

Iddi Kipagwile aliongeza bao la pili dakika ya 69 na dakika za nyongeza Yasin Mgaza alihitimisha ushindi huo kwa bao la tatu dakika ya 90+1 na kuifanya Dodoma kushinda kwa kishindo 3-0.

Ushindi huo unaifanya Dodoma kuendelea kuimarisha nafasi yao katikati ya msimamo wa ligi ikikaa nafasi saba ikiwa imekusanya alama 24.

Kwa upande mwingine, katika mchezo uliochezwa Tanzanite Kwaraa, Manyara, mashabiki walishuhudia moja ya mechi tamu zaidi za wiki hii baada ya Mbeya City kuifunga KMC 3-2.

KMC ilikuwa ya kwanza kupata bao kupitia kwa Oscar Paul dakika ya 44, na kwenda mapumziko wakiwa mbele.

Kipindi cha pili Mbeya City walibadilika kabisa, wakisawazisha kupitia Riphat Msuya dakika ya 64, kabla ya Adili Buha kufunga kwa penalti dakika ya 76 na kuwapa uongozi wenyeji.

Hata hivyo, KMC hawakukata tamaa na walifanikiwa kusawazisha dakika ya 78 kupitia Juma Shemvuni, jambo lililoongeza presha kubwa kwa wenyeji Mbeya City.

Wakati mchezo ukionekana kuelekea sare, Said Naushad alitokea kuwa shujaa wa Mbeya City kwa kufunga bao la ushindi dakika ya 86, na kuamsha shangwe kubwa Tanzanite Kwaraa. 

Matokeo hayo yana maana kubwa kwenye mbio za msimamo wa ligi, hasa kwa Mbeya City ambao walikuwa wanahitaji sana ushindi huo kujinasua kutoka maeneo ya hatari ya msimamo wa Ligi Kuu ya NBC.

Kwa ujumla, jana ilikuwa siku ya mabao 8 kwenye michezo miwili, ushindi wa kishindo kwa Dodoma Jiji na ushindi wa jasho kwa Mbeya City, matokeo ambayo yanaongeza ushindani mkubwa zaidi msimu huu.

SIMBA, COASTAL KUONYESHANA UBABE LEO LIGI KUU YA NBC.

LIGI Kuu ya NBC itaendelea tena mkoani Dar es Salaam leo ambapo timu ya Simba itaikaribisha timu ya Coastal Union katika uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo saa 1:00 usiku.

Kila timu imejiandaa vyema ikizitaka alama zote tatu ili kujiweka katika nafasi nzuri ambapo Simba inataka kujihakikishia iko kwenye mbio za ubingwa huku Coastal Union ikitaka kujiweka katika nafasi nzuri ya kusalia kwenye ligi hiyo msimu ujao.

Wachezaji wa timu ya Simba

Simba inashika nafasi ya tatu katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC ikiwa imecheza michezo 14, kushinda michezo tisa sare nne na kupoteza mchezo mmoja na kukusanya alama 31.

Wachezaji wa timu ya Coastal Union.

Kwa upande wa Coastal Union inashika nafasi ya 13 kwenye msimamo ikiwa na alama 15 katika michezo 16 iliyocheza ikishinda michezo mitatu, sare sita na kupoteza michezo saba.

FIRST LEAGUE YA MOTO! BANDARI, RHINO ‘VINARA’ MBIO ZA KUPANDA NBC CHAMPIONSHIP.

MSIMU wa First League 2025/26 umeendelea kutoa ushindani mkubwa baada ya kila timu kucheza mechi tisa huku vita ya kusaka nafasi ya kupanda Ligi ya NBC Championship ikizidi kupamba moto katika makundi yote mawili.

Kwenye kundi A timu ya Bandari Tanzania inaonekana kuwa na kasi kubwa zaidi baada ya kujikusanyia alama 20, wakiongoza msimamo mbele ya Nyumbu yenye alama 18 huku tofauti ya alama mbili pekee kati ya timu hizo ikionyesha wazi kuwa mbio za kileleni bado hazijaamuliwa na kila mchezo uliosalia utakuwa na uzito mkubwa.

Takwimu za Bandari zinaonyesha uimara mkubwa, wakiwa na ushindi kwenye michezo sita, sare mbili na kupoteza mchezo mmoja pekee, huku safu yao ya ushambuliaji ikiwa tayari imefunga mabao 17. 

Nafasi ya tatu inashikiliwa na Cosmopolitan ambayo haipo mbali baada ya kufikisha alama 16, jambo linalofanya kundi A kuwa moja ya makundi yenye ushindani mkali zaidi ambapo tofauti ndogo ya alama kati ya timu tatu za juu ikiashiria kuwa mzunguko wa pili unaweza kubadili kabisa ramani ya msimamo.

Kwa upande wa kundi B timu ya Rhino Rangers imekuwa bora zaidi hadi sasa ikiwa na alama 24 baada ya mechi 9 ikionyesha ubora mkubwa kwa kushinda michezo minane na kupoteza mmoja pekee.

Safu ya ushambuliaji ya ‘maafande’ hao imefunga jumla ya mabao 21, idadi kubwa zaidi kwenye makundi yote mawili ya First League huku wakiruhusu mabao saba pekee huku hii ikiwa sababu kubwa ya kuwa kwenye nafasi kubwa ya kumaliza kileleni na kukata tiketi ya moja kwa moja kuelekea NBC Championship. 

Timu za IAA na Endument bado wapo kwenye mbio hizo wakishika nafasi ya pili na tatu ingawa wanalazimika kuongeza kasi ili kuzuia Rhino Rangers wasiweke uwiano mkubwa wa alama zaidi kileleni.

VITA YA MTOANO NA JANGA LA KUSHUKA DARAJA.

Mbali na vita vya juu, pambano la kujiokoa kushuka daraja pia limeanza kuchangamka sana.

Katika kundi A, Dar City inaonekana kuwa kwenye kipindi kigumu zaidi baada ya kubaki mkiani na alama 4 pekee, huku ikiwa tayari imeruhusu mabao 24 na kuwa na rekodi mbaya ya safu ya ulinzi ambayo imekuwa sababu kubwa ya timu hiyo kuwa katika hatari kubwa ya kushuka daraja.

Kwa kundi B hali ni mbaya zaidi kwa ‘Wanajeshi wa mpakani’ timu ya Biashara United ambayo hadi sasa ina deni la alama -1lililotokea baada ya kushindwa kufika uwanjani kwenye michezo miwili na kupokwa alama na mamlaka za soka kitu kinachoonyesha wazi namna walivyoanza msimu vibaya na jinsi kila mchezo uliosalia utakavyokuwa wa kama fainali kwao.

MICHEZO IJAYO KUAMUA HATMA.

Ratiba ya michezo ijayo inaweza kubadilisha kabisa sura ya misimamo yote miwili hasa kwa kundi A ambapo Bandari bado wanakabiliwa na mechi ngumu dhidi ya Nyumbu, Green Warriors na Cosmopolitan. 

Kwa kundi B macho yote yataelekezwa kwa Rhino Rangers kuona kama watakuwa na muendelezo mzuri au wapinzani wao wataanza kupunguza ‘pengo’ la alama.

Kwa ujumla, First League msimu huu imeonyesha ushindani wa hali ya juu, mabao mengi, na presha kubwa kuanzia nafasi za juu hadi chini ya msimamo na endapo kasi hii itaendelea mzunguko wa pili unaweza kuwa mmoja wa misimu yenye utofauti mkubwa zaidi kuwahi kushuhudiwa.

AZAM YAONGEZA PRESHA KWENYE ‘KILELE’ CHA LIGI KUU YA NBC.

TIMU ya Azam imeonyesha ubora na ukomavu mkubwa baada ya kuibuka na ushindi muhimu wa mabao 2-1 dhidi ya Singida Black Stars kwenye mchezo wa Ligi Kuu ya NBC uliopigwa Airtel Stadium, Singida.

Baada ya kutoka sare mbili mfululizo bila kufungana, kikosi hicho cha kocha Florent Ibenge kilirejea kwa nguvu na kuonyesha dhamira ya kupambania nafasi za juu kwenye msimamo wa ligi hiyo.

Bao la kwanza la Azam lilifungwa mapema kipindi cha pili kupitia kwa nahodha Lusajo Mwaikenda aliyemalizia kwa ustadi mpira wa krosi uliotengenezwa na Iddy Seleman ‘Nado’.

Dakika chache baadaye, staa wa timu hiyo Feisal Salum “Fei Toto” aliandika bao la pili kwa shuti la utulivu baada ya kupokea pasi safi kutoka kwa ‘Nado’ bao ambalo liliongeza presha kubwa kwa wenyeji Singida.

Singida Black Stars walijitahidi kurejea mchezoni na kufanikiwa kupata bao moja kupitia kwa Ayubu Lyanga dakika ya 71, lakini juhudi zao za kusawazisha ziligonga mwamba mbele ya safu imara ya ulinzi ya ‘Matajiri wa chamazi’.

Matokeo hayo yanaifanya Azam kuendelea kuwepo kwenye mbio za ubingwa msimu huu ikikwea hadi nafasi ya pili baada ya kukusanya alama 32 huku ikionyesha kuwa bado ni tishio kubwa kwa vigogo wengine wa ligi, hasa kuelekea ‘duru’ la mwisho la Ligi Kuu ya NBC.

LIGI KUU YA NBC KUREJEA LEO.

LIGI Kuu ya NBC inarejea leo baada ya mapumziko ya michezo ya kalenda ya Fifa ambapo timu ya Singida Black Stars itaikaribisha timu ya Azam katika uwanja wa Airtel mkoani Singida saa 10:00 alasiri.

Mchezo huo ni muhimu kwa timu zote kwani zinatafuta alama tatu muhimu ili kujiweka katika nafasi nzuri ya mbio za ubingwa wa Ligi Kuu ya NBC.

Wachezaji wa timu ya Singida Black Stars.

Singida Black Stars iko nafasi ya sita katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC ikiwa imecheza michezo 15 ikishinda michezo saba sare nne na kufungwa michezo minne ikikusanya alama 25.

 Wachezaji wa Azam

Kwa upande wa Azam ipo nafasi ya tatu katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC ikicheza michezo 15 kushinda michezo saba na sare nane huku ikiwa imekusanya alama 29.