Tag: #LIGIKUU #NBCPL #AZAM #YANGA #SIMBA #KMC #JKT #MASHUJAA #KENGOLD #DODOMAJIJI #PAMBAJIJI #KAGERASUGAR #SINGIDABLACKSTARS #FOUNTAINGATE #NAMUNGO

PACOME AIBEBA YANGA IKIIFUNGA COASTAL LIGI KUU NBC

LIGI Kuu ya NBC imeendelea kwa mchezo mmoja uliochezwa uwanja wa KMC Complex ambapo timu ya  Young Africans iliikaribisha timu ya Coastal Union  kutoka Tanga.

Mchezo huo ulianza majira ya saa kumi na robo jioni ambapo timu zote zilikuwa zikishambuliana huku pia zikiimarisha ulinzi katika lango lao ili kutokuruhusu bao lolote.

Ilimchukua dakika 34 mchezaji wa Young Africans Pacome Zouzoua kufungua ukurasa wa mabao hivyo kuifanya timu yake kwenda mapumziko ikiwa mbele kwa bao moja.

Kipindi cha pili kilianza ambapo timu zote zilionekana zikitaka alama  tatu  muhimu ambapo hata hivyo mchezo  ulitamatika kwa Young Africans kuibuka na ushindi wa bao 1-0.

Youn Africans imezidi kujiweka katika nafasi nzuri ya kuwania ubingwa baada ya kufikisha alama 64 huku wakiwa wamecheza michezo 24  na wakiendelea kuongoza katika msimamo wa Ligi Kuu  huku timu ya  Coastal Union ipo nafasi ya13  katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC ikiwa na alama 25.

 

 

 

KASEJA AIFUFUA UPYA KAGERA SUGAR

TIMU ya Kagera Sugar imeanza kujipata katika michezo ya Ligi Kuu ya NBC baada ya kushinda mechi tatu walizocheza hivi karibuni chini ya uongozi wa Kocha wao mpya Juma Kaseja ambaye pia ni golikipa aliyecheza kwa mafanikio makubwa timu ya taifa na timu mbalimbali za Ligi Kuu .

Kaseja ambae alichukua mikoba kutoka kwa Kocha Melis Medo ambae ametimkia katika timu ya Singida Black Stars  aliiongoza timu yake katika mchezo miwili huku mchezo wa kwanza  dhidi ya Pamba Jiji  alifanikiwa kushinda mabao 2-1.

Mchezo mwingine ulichezwa jana April 3 alifanikiwa kuifunga timu ya Coastal Union kwa mabao 2-1 ambapo mabao ya Kagera Sugar yalifungwa na Ally Msangi wa Coastal Union aliyejifunga bao  dakika ya 59 na Mohamed Jecha dakika ya 90  huku mchezaji Lucas Kikoti akiipatia Coastal Union bao dakika ya 84 ya mchezo huo.

Kagera Sugar imefikisha alama 22 ikiwa nafasi ya 14 kwenye msimamo baada ya kucheza michezo 24 wakifunga mabao 20 na kufungwa mabao 32.

LIGI KUU NBC ‘KUCHANJA MBUGA’ VIWANJA VITATU,CHAMPIONSHIP MAMBO YAZIDI KUWA MOTO.

MZUNGUKO wa 24 wa Ligi Kuu ya NBC utaendelea kushika kasi  ambapo michezo mitatu itachezwa katika mikoa ya Kagera,Dar es Salaam na Mbeya hivyo kufanya mbio za ubingwa kuzidi kufikia mahali patamu zaidi kwani mmoja anapambana angalau apate alama  ili aweze kubeba ubingwa ama aendelee kubaki msimu ujao .

JKT Tanzania ambayo ipo nafasi ya sita kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC itakuwa mwenyeji wa Dodoma Jiji  iliyopo nafasi ya nane katika uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo  uliopo Mbweni Dar es Salaam majira ya saa kumi jioni.

KenGold iliyopo nafasi ya 16   katika msimamo wa Ligi Kuu  ya NBC itakawakaribisha timu ya Azam katika uwanja wa Sokoine mkoani Mbeya majira ya saa kumi jioni huku Kagera Sugar atakuwa mwenyeji wa Coastal Union katika uwanja wa Kaitaba mkoani Kagera majira ya saa moja usiku.

Kwa upande wa Ligi ya Championship ya NBC timu ya Songea United itaikaribisha timu Biashara United katika uwanja wa Majimaji mkoani Ruvuma majira ya saa kumi jionI ikiwa ni mzunguko wa 25 wa Ligi hiyo.

MOUSSA CAMARA ANA JAMBO LAKE LIGI KUU YA NBC.

IKISALIA mizunguko saba kutamatika kwa Ligi Kuu ya NBC ‘Mlinda lango’ wa timu ya Simba Moussa Pinpin Camara ameendelea kushikilia usukani wa vinara ambao hawajaruhusu mabao kwenye ligi hiyo.

Camara hadi sasa amefikisha idadi ya michezo 15 aliyocheza bila kuruhusu nyavu zake kuguswa huku timu yake ikifungwa mabao nane pekee hadi sasa.

Golikipa huyo wa Simba amemzidi michezo minne mpinzani wake Djigui Diarra wa Yanga anayemfuatia kwa karibu akiwa amekusanya jumla ya michezo 11 bila kuruhusu bao.

Patrick Munthali wa timu ya Mashujaa iliyoruhusu mabao 28 hadi sasa anashika nafasi ya tatu akiwa na michezo 10 bila kuruhusu bao huku idadi hiyo ikiwa sawa na golikipa wa Azam Mohammed Mustapha huku Azam ikiruhusu mabao 12 hadi sasa ikisalia na michezo saba kutamatisha msimu.

LADHA ZA LIGI KUU YA NBC KUREJEA APRIL MOSI

LIGI Kuu ya NBC inatarajia kurejea mapema mwezi ujao baada ya mapumziko ya takribani wiki mbili  kupisha michezo ya kufuzu Fainali za Kombe la Dunia 2026.

Kurejea kwa Ligi Kuu ya NBC ni mwanzo wa mzunguko wa  24  huku ikibaki mizunguko takribani sita ligi hiyo kutamatika.

April mosi Tabora United  itawakaribisha ‘watoto wa Jangwani’ Young Africans kwenye uwanja wa Ali Hassan Mwinyi  mkoani Tabora mchezo utakaochezwa majira ya saa kumi alasiri.

April mbili itapigwa michezo mitatu Pamba Jiji itaikaribisha Namungo majira ya saa 8:00 mchana katika  uwanja wa CCM Kirumba huku KMC ikiwaalika Tanzania Prisons kwenye uwanja wa KMC Complex mkoani Dar es Salaam majira ya saa 10:15 na mchezo wa mwisho utapigwa Tanzanite Kwaraa kati ya Fountain Gate itakayoikaribisha Singida Black Stars saa 10:15 alasiri.

April tatu itaanzia katika uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo JKT Tanzania ikiwakaribisha Dodoma Jiji, Ken Gold ikiwaalika Azam katika uwanja wa Sokoine michezo yote ikichezwa saa 10:00 alasiri huku Kagera Sugar ikiwaalika Coastal Union katika uwanja wa Kaitaba majira ya saa 1:00 usiku.

Mchezo wa Simba na Mashujaa utachezwa Mei mbili kutokana na timu ya Simba kukabiliwa na michuano ya Kombe la Shirikisho barani Afrika ambayo kwa sasa ipo katika batua ya robo fainali.