Tag: #LIGIKUU #NBCPL #AZAM #YANGA #SIMBA #KMC #JKT #MASHUJAA #KENGOLD #DODOMAJIJI #PAMBAJIJI #KAGERASUGAR #SINGIDABLACKSTARS #FOUNTAINGATE #NAMUNGO

KENGOLD YAAGA RASMI LIGI KUU YA NBC.

TIMU ya KenGold imekuwa timu ya kwanza kuaga Ligi Kuu ya NBC msimu wa 2024/25 na kushuka daraja baada ya kupoteza jana kwa mabao 2-1 dhidi ya Coastal Union ya Tanga kwenye uwanja wa Mkwakwani, Tanga.

KenGold iliyokuwa bingwa wa Ligi ya Championship ya NBC msimu wa 2023/24 na kufanikiwa kupanda ligi kuu imedumu kwa msimu mmoja pekee na kurejea tena kwenye ligi ya Championship.

Hadi sasa mabingwa hao waliopita wa Championship wameshinda michezo mitatu pekee ya Ligi Kuu ya NBC wakifungwa 17, huku wakitoka sare michezo saba na kukusanya alama 16 pekee huku ikisalia michezo mitatu kukamilika kwa msimu.

KenGold hadi sasa imeruhusu mabao 50 na kufunga 22 huku ikiwa timu ya pili kuruhusu mabao mengi nyuma ya Fountain Gate ya Manyara iliyofungwa mabao 51 hadi sasa.

MUKWALA,FADLU WANG’ARA TUZO ZA MWEZI

MSHAMBULIAJI wa timu ya Simba ya Dar es Salaam, Steven Mukwala amechaguliwa kuwa Mchezaji Bora wa mwezi Machi wa Ligi Kuu ya NBC msimu wa mwaka 2024/25, huku Fadlu Davids pia wa Simba akichaguliwa Kocha Bora wa ligi hiyo kwa mwezi huo.

Mukwala alionesha kiwango kizuri chenye mwendelezo akiwashinda Elie Mpanzu wa Simba na Paschal Msindo wa Azam alioingia nao fainali katika mchakato wa Tuzo za Mwezi uliofanywa na Kamati ya Tuzo za Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF).

Mchezaji huyo alitoa mchango mkubwa kwa timu yake katika michezo miwili ambayo Simba ilicheza mwezi huo na kufunga mabao manne, huku matatu akifunga katika mchezo mmoja (hat-trick). Mukwala alicheza dakika 152 za michezo miwili.

Kwa upande wa kocha Davids aliyeingia fainali na Rachid Taoussi wa Azam na David Ouma wa Singida Black Stars, aliiongoza Simba kushinda michezo yote miwili iliyocheza mwezi huo. Simba iliifunga Dodoma Jiji mabao 6-0 na Coastal Union mabao 0-3, hivyo kuendelea kubaki nafasi ya pili kwenye msimamo wa ligi.

Pia Kamati ya Tuzo imemchagua Meneja wa Uwanja wa Sokoine Mbeya, Modestus Mwaluka kuwa Meneja Bora wa Uwanja kwa mwezi Machi kutokana na kufanya vizuri katika menejimenti ya matukio ya michezo pamoja na masuala yanayohusu miundombinu uwanjani.

Wakati huo huo Kamati ya Tuzo za TFF, imemchagua Mwani Thobias wa Mbeya City kuwa Mchezaji Bora wa Mwezi Machi wa Ligi ya NBC Championship 2024/25, huku Awadh Juma wa Mtibwa Sugar akichaguliwa Kocha Bora wa mwezi huo.

Thobias aliyeingia fainali na Magata Charles wa Mtibwa Sugar na Selemani Richard wa Stand United, alionesha kiwango chenye mwendelezo, ikiwa ni pamoja na kufunga mabao matano kwa dakika 325 alizocheza za michezo minne.

Kwa upande wa Awadh aliyeingia fainali na Mohamed Ismail wa TMA na Juma Hussein wa Stand United, aliiongoza Mtibwa Sugar kushinda michezo mitatu kati ya minne iliyocheza na kuendelea kubaki kileleni kwenye msimamo wa ligi

DUBE,AHOUA HAPATOSHI UFUNGAJI BORA LIGI KUU NBC.

VITA ufungaji bora imeanza upya ndivyo unavyoweza kusema baada ya mshambuliaji wa Young Africans Prince Dube kumfikia  idadi ya mabao kiungo wa Simba,Jean Ahoua huku Ligi Kuu ya NBC ambayo ni Ligi namba nne kwa ubora barani Africa ikielekea ukingoni.

Dube ambaye amefunga mabao 12 na kutoa pasi za mwisho nane katika michezo 25 ambayo timu yake imeshacheza mpaka sasa katika Ligi Kuu ya NBC sawa na Ahoua wa timu ya Simba ambaye amefanikiwa kufunga mabao 12  na kutoa pasi za mwisho saba katika michezo 22 ambayo timu yake imeshacheza.

Young Africans imebakisha michezo mitano ikiwa imeshacheza michezo 25 huku Simba ikiwa imebakisha michezo minane baada ya kucheza mechi 22 hivyo njia inaweza kuwa nyepesi kwa wachezaji hao na wengine wanaowakaribia kuibuka na ufungaji bora wa Ligi Kuu mara baada ya kufikia ukingoni.

 

COASTAL UNION WAIZINDUA MKWAKWANI KIBABE LIGI KUU NBC

LIGI Kuu ya NBC inaendelea kushika kasi ambapo jana Coastal Union iliwakaribisha timu ya Singida Black Stars katika uwanja wa Mkwakwani Tanga ikiwa ni mechi ya kwanza tangu kuboreshwa kwa uwanja huo.

Mchezo huo ulianza majira ya saa 10:00 alasiri ambapo timu zote zilikuwa na shauku ya kuchukua alama ili kujiweka katika mazingira mazuri Coastal Union wakiendelea kujinasua kutoka nafasi za chini kwenye msimamo na Singida wakipambania nafasi nne za juu kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC.

Dakika 47 ziliwatosha Coastal Union kuongoza mchezo baada ya kupata bao la kwanza baada ya mchezaji wa Singida Josephat Bada kujifunga hivyo kuwafanya wana mangushi kwenda mapumziko na uongozi wa 1-0.

Kipindi cha pili kilianza kwa kasi na dakika ya 76 mshambuliaji wa Singida, Jonathan Sowah aliipatia timu yake bao kupitia mkwaju wa penati na dakika ya 82 mchezaji wa Coastal union, Bakari Msimu aliongeza bao hivyo mchezo kutamatika kwa 2-1.

Matokeo hayo yanaipeleka Coastal hadi nafasi ya 10 na alama 28 huku Singida ikisalia nafasi ya nne ikiwa na alama 50.

YOUNG AFRICANS WABABE WA DABI YA DAR

LIGI Kuu ya NBC imeendelea jana ambapo mchezo wa Dabi ya Dar es Salaam ambapo Azam iliwakaribisha Young Africans uliochezwa katika uwanja wa Azam Complex majira ya saa moja usiku.

Mchezo huo ulianza kwa kasi kubwa huku Young Africans wakionekana kushambulia kwa kasi kubwa  huku Azam wakionekana kuzuia kwa kasi ya wapinzani wao.

Ilimchukua dakika 11 tu kiungo wa Young Africans Pacome Zouzoua  kufungua ukurasa wa mabao ambapo aliitanguliza timu yake huku Prince Dube akiongeza bao dakika ya 34 ya mchezo huo  na kufanya timu hiyo kwenda mapumziko wakiwa wako mbele kwa mabao 0-2.

Kipindi cha pili mchezo uliendelea kwa timu zote kusaka mabao ili kujiweka katika nafasi nzuri zaidi na dakika ya 81 beki wa Azam Lusajo Mwaikenda alifungua ukurasa wa mabao kwa timu yake hivyo kufanya mchezo kuwa wa kasi ya kushambuliana zaidi ambapo dakika 90 zilitamatika kwa matokeo ya 1-2.

Mshambuliaji wa Young Africans Prince Dube alichaguliwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo baada ya kuisaidia timu yake kupata ushindi.