Tag: #LIGIKUU #NBCPL #AZAM #YANGA #SIMBA #KMC #JKT #MASHUJAA #KENGOLD #DODOMAJIJI #PAMBAJIJI #KAGERASUGAR #SINGIDABLACKSTARS #FOUNTAINGATE #NAMUNGO

SIMBA YAREJEA KILELENI KIBABE,TABORA UNITED HAISHIKIKI LIGI KUU NBC

LIGI Kuu ya NBC iliendelea jana kwa michezo mitatu iliyochezwa katika viwanja mbalimbali nchini kuanzia saa kumi alasiri na mchezo wa mwisho ukichezwa saa moja jioni.

Simba waliwakaribisha timu ya Tanzania Prisons katika uwanja wa KMC Complex majira ya saa kumi alasiri ambapo mchezo ulianza timu zote zikicheza kwa tahadhari kubwa hususan Simba .

Dakika ya 29 Jean Ahoua alifungua ukurasa wa mabao  kwa timu yake akipokea pasi ya upendo kutoka kwa beki wa timu hiyo Shomari Kapombe,winga wa timu hiyo Ellie Mpanzu nae aliongeza bao la pili dakika ya 44 huku Ladack akifunga bao la tatu na kuwafanya Simba kwenda mapumziko wakiwa kifua mbele kwa mabao 3-0.

Kipindi cha pili kilianza ambapo timu ya Tanzania Prisons walifanya mabadiliko na kuamua kucheza kwa kujilinda zaidi ambapo waliweza kufanikiwa lengo lao kutoruhusu bao lolote kipindi cha pili hivyo mchezo kuisha kwa Simba kufanikiwa kubeba alama zote tatu hivyo kupanda kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu.

Beki wa Simba Shomari Kapombe alichaguliwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo baada ya kutoa pasi mbili za mabao kwa Jean Ahoua na Ladack Chasambi.

Mchezo mwingine  ulikuwa ni timu ya  Mashujaa iliwakaribisha timu ya Coastal Union katika uwanja wa Lake Tanganyika mkoani Kigoma.

Katika mchezo huo timu zote zilicheza kwa tahadhari kubwa kwa sababu ya kuzitaka alama tatu  muhimu ili kujiweka katika nafasi nzuri katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC.

Mpaka dakika 90 za mchezo huo zinatamatika ubao wa matokeo ulikuwa unasomeka 0-0. Mchezaji wa Mashujaa Idrisa Stambuli alichaguliwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo.

Mchezo wa mwisho ulichezwa saa moja jioni mkoani Kagera ambapo Kagera Sugar iliwakaribisha timu ya Tabora United katika uwanja wa Kaitaba.

Mchezo ulianza vyema huku wachezaji wote wakionyesha ari ya kuzipambania timu zao  ambapo dakika 45 za mchezo huo zilitamatika kwa sare ya kutokufungana .

Kipindi cha pili kilianza ambapo dakika ya 52 mchezaji wa Tabora United, Offen Chikola alifungua ukurasa wa mabao na dakika ya 77 mchezaji  Andy Bikoko aliiongezea bao timu yake ya Tabora United  na dakika chache kabla ya mchezo kutamatika mchezaji wa Kagera Sugar, Cleophace Mkandala aliifungia timu yake bao la kufutia machozi hivyo mchezo kutamatika kwa 2-1.

Mchezaji wa Tabora United Offen Chikola alichaguliwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo baada ya kufunga bao moja na kutoa pasi ya mwisho katika mchezo huo.

Ligi Kuu ya NBC itaendelea kesho kwa mchezo mmoja ambapo timu ya JKT Tanzania itawakaribisha timu ya Singida Black Stars katika uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo uliopo Mbweni mkoani Dar es Salaam.

 

 

KMC YAREJEA NYUMBANI KIBABE LIGI KUU YA NBC.

TIMU ya KMC ya Dar es Salaam imefanikiwa kupata ushindi wa kwanza nyumbani dhidi ya Singida Black Stars kwa mabao 2-0 tangu kurejea kwa Ligi Kuu ya NBC iliyokuwa kwenye mapumziko mafupi.

Mabao mawili yaliyofungwa na Oscar Paulo kipindi cha kwanza yalitosha kuzamisha jahazi la Singida BS ambayo haijapata ushindi tangu kurejea kwa ligi hiyo.

KMC imefanikiwa kupata ushindi baada ya kupoteza mchezo uliopita ugenini dhidi ya Coastal Union kwa mabao 2-1 huku Singida ikilazimishwa sare ya 2-2 mchezo uliopita dhidi ya Kagera Sugar.

KMC imefikisha alama 22 na ‘kukwea’ hadi nafasi ya sita kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC huku Singida BS ikisalia nafasi ya nne na alama 31.

JKT, YOUNG AFRICANS  HAKUNA MBABE

LIGI Kuu ya NBC imezidi kushika kasi   JKT Tanzania iliwakaribisha timu ya Young Africans katika uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo mkoani Dar es Salaam jana.

Mchezo huo ulipigwa majira ya saa kumi na robo ambapo timu zote zilionekana kuzitaka alama zote ili ziweze kuwa katika  nafasi nzuri

Yanga walizitaka alama hizo ili waweze kuendelea kukaa kileleni huku JKT ikitamani  kujiweka katika nafasi nzuri katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC.

Mpaka dakika 45 zinatamatika timu zote zilienda mapumziko bila ya kufungana hivyo kuwapa kazi ngumu makocha wao kujiuliza nini cha kufanya kwa kipindi cha pili ili kuweza kupata matokeo.

Kipindi cha pili kilianza kwa kasi na timu zote zilifanya mabadiliko ya vikosi mara kwa mara ili kuweza kuona kama wanaweza kushinda mchezo huo.

Mpaka dakika 90 za mchezo huo zinatamatika sio wenyeji JKT Tanzania ama wageni Young Africans walioambulia goli lolote hivyo mchezo kumalizika kwa sare pacha ya kutokufungana ikiwa ni msimu wa pili kwa Young Africans kutokushinda katika Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo.

Ligi Kuu ya NBC itaendelea leo kwa michezo mitatu ambapo Mashujaa watawakaribisha Coastal  Union katika uwanja wa Lake Tanganyika,Simba ikiumana na Tanzania Prisons uwanja wa KMC Complex na Kagera Sugar watakuwa wenyeji wa Tabora United uwanjani Kaitaba mkoani Kagera.

PAMBA JIJI YAWADUWAZA AZAM, NAMUNGO YATOSHANA NGUVU NA DODOMA JIJI.

LIGI Kuu ya NBC iliendelea jana kwa michezo miwili ambapo Pamba Jiji iliwakaribisha timu ya Azam katika mchezo uliochezwa uwanja wa CCM Kirumba Mwanza na Namungo iliwakaribisha Dodoma Jiji uwanja wa Majaliwa mkoani Lindi.

Mchezo wa Pamba Jiji ulianza majira ya saa kumi alasiri ambapo timu zote zilikuwa zikishambuliana kwa kasi na kuonyesha nia ya kuzitaka alama zote tatu mhimu za mchezo huo hivyo kwenda mapumziko wakiwa suluhu ya kutokufungana bao lolote.

Kipindi cha pili kilianza ambapo Pamba Jiji ilionekana kurejea kwa kasi zaidi huku ikizima mashambulizi yaliyokuwa wakianzishwa na Azam mara kwa mara na dakika ya 86 ya mchezo huo Pamba Jiji walipata bao kupitia mchezaji wao Deus Kaseke ambae aliingia dakika chache kabla ya kufunga bao hilo pekee lililopeleka kilio kwa ‘matajiri wa jiji la Dar es Salaam’ baada ya mchezo kuisha kwa Pamba 1-0.

Mchezo wa pili ulianza majira ya saa moja jioni ambapo Namungo ‘Wauaji wa Kusini’ iliwakaribisha Dodoma Jiji huku timu ya Namungo ikionekana kushambulia zaidi.

Iliwachukua dakika 21 timu ya Dodoma Jiji kupitia mchezaji wao Paul Peter kufungua ukurasa wa mabao na dakika kumi mbele Apolo Otieno aliiongezea bao la pili Dodoma Jiji na dakika ya 44 Namungo  walipata bao kupitia mchezaji wao Pius Buswita hivyo kwenda mapumziko ubao ukisoma 1-2.

Kipindi cha pili kilianza kwa kasi kwa Namungo wakisaka bao la kusawazisha huku Dodoma Jiji wakisaka bao zaidi, dakika ya 56 ya mchezo huo mchezaji wa Namungo Erasto Nyoni aliiongezea timu yake bao la pili kupitia mkwaju wa penati  hivyo matokeo kuwa 2-2 mpaka mwisho wa mchezo.

Ligi Kuu ya NBC itaendelea leo katika viwanja vitatu ambapo KenGold watawakaribisha Fountain Gate katika uwanja  wa Sokoine jijini Mbeya na mkoani Dar es Salaam KMC watawakaribisha Singida Black Stars huku JKT wakiwakaribisha Young Africans uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo.

SILLAH AWALIZA ‘WATOTO WA MJINI’ LIGI KUU NBC

MCHEZAJI wa Azam Gibril Sillah amepeleka kilio kwa KMC ‘Watoto wa mjini’ baada ya kufunga mabao mawili kwenye mchezo wa Ligi Kuu ya NBC uliochezwa uwanja wa Azam Complex, Dar es Salaam.

Azam ilizitafuta kwa nguvu alama tatu ikicheza kwa kasi huku KMC  ikicheza kwa tahadhari kubwa na kujilinda ingawa Ilimchukua dakika 26 mchezaji wa Azam Gibril Sillah kufungua akaunti ya mabao na hadi mapumziko Azam ilienda kifua mbele ikiongoza kwa bao 1-0.

Kipindi cha pili kilianza kwa kasi huku KMC ikionekana kutaka kusawazisha kwa kuwashambulia Azam ambao muda wote waliziba njia na mipango ya KMC na dakika ya 65 Sillah alirejea tena ‘kambani’  na kufanya ubao kusomeka 2-0.

Mpaka mchezo huo unatamatika Azam ilifanikiwa kubakisha alama tatu muhimu za mchezo huo wakiendelea kuwa nafasi ya tatu na alama 39 katika msimamo huo.

Matokeo hayo yanaifanya Azam kupata ushindi kwenye michezo yote miwili iliyocheza dhidi ya KMC msimu huu baada ya mzunguko wa kwanza kuifunga mabao 4-0 kwenye uwanja wa KMC Complex, Dar.