Author: Loveness Bernard

KIPAGWILE,HAMDI WANG’ARA TUZO ZA MWEZI APRIL LIGI KUU NBC

MSHAMBULIAJI wa timu ya Dodoma Jiji, Iddi Kipwagile amechaguliwa kuwa Mchezaji Bora wa mwezi Aprili wa Ligi Kuu ya NBC msimu wa mwaka 2024/25, huku Miloud Hamdi wa Yanga, akichaguliwa kuwa Kocha Bora wa ligi hiyo kwa mwezi huo.

Kipwagile alionesha kiwango kizuri chenye mwendelezo akiwashinda Pacome Zouzoua wa Yanga na Haruni Chanongo wa Tanzania Prisons, alioingia nao fainali katika mchakato wa Tuzo za Mwezi uliofanywa na Kamati ya Tuzo za Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF).

Mchezaji huyo alitoa mchango mkubwa kwa timu yake katika michezo minne ambayo Dodoma Jiji ilicheza mwezi huo na kufunga mabao matatu na kuhusika na mengine matatu kwa dakika 320 alizocheza.

Kwa upande wa Hamdi aliyeingia fainali na Amani Josiah wa Tanzania Prisons na David Ouma wa Singida Black Stars, aliiongoza Yanga kushinda michezo yote minne iliyocheza mwezi huo na kuendelea kubaki kileleni mwa msimamo wa ligi Kuu ya NBC. Yanga ilizifunga Tabora United (0-3), Coastal Union (1-0), Azam (1-2) na Fountain Gate (0-4).

Pia Kamati ya Tuzo imemchagua Meneja wa Uwanja wa Isamuhyo uliopo Dar es Salaam, Ashraf Omar kuwa Meneja Bora wa Uwanja kwa mwezi Aprili kutokana na kufanya vizuri katika menejimenti ya matukio ya michezo pamoja na masuala yanayohusu miundombinu uwanjani.

Wakati huohuo Kamati ya Tuzo za TFF, imemchagua Emmanuel Maziku wa Stand United kuwa Mchezaji Bora wa Mwezi Aprili wa Ligi ya NBC Championship 2024/25, huku Ramadhan Ahmada wa Transit Camp akichaguliwa kuwa Kocha Bora wa mwezi huo.

Maziku aliyeingia fainali na Mohammed Hassan wa Transit Camp na Ramadhan Kipalamoto wa Songea United, alionesha kiwango chenye mwendelezo, ikiwa ni pamoja na kufunga mabao manne kwa dakika 194 alizocheza kwenye michezo mitatu.

Kwa upande wa Ahmada aliyeingia fainali na Malale Hamsini wa Mbeya City na Awadh Juma wa Mtibwa, aliiongoza timu yake kushinda michezo yote mitatu iliyocheza na kupanda kutoka nafasi ya 15 hadi ya 13 kwenye msimamo wa ligi hiyo.

SIMBA ‘YATAKATA’ DHIDI YA MASHUJAA LIGI KUU YA NBC

LIGI Kuu ya NBC imeendelea leo kwa mchezo mmoja uliochezwa majira ya saa kumi jioni katika uwanja wa KMC mkoani Dar es Salaam ambapo Simba waliwakaribisha timu ya Mashujaa kutoka mkoani Kigoma.

Mchezo ulianza kwa kasi ambapo kila timu ilionyesha ikitaka kupata alama tatu  ambapo iliwachukua dakika tano timu ya Mashujaa kufungua ukurasa wa mabao kupitia mchezaji wao Jafary Kibaya ambapo mpaka wakati wa kwenda mapumziko matokeo yalikuwa 0-1 licha ya Simba tupambana kusawazisha .

Kipindi cha pili kilianza kwa kasi huku Simba wakiwa na uchu zaidi wa kufika langoni mwa mpinzani wao licha ya kukutana na upinzani mkali kutoka kwa wachezaji wa timu ya mashujaa ambapo hata hivyo dakika ya 65 ya mchezo huo Leonel Ateba alifungua akaunti ya mabao kwa Simba kupitia mkwaju wa penati na kufanya ubao kusomeka 1-1 na alirejea tena nyavuni kupitia mkwaju wa penati ya pili hivyo kufanya ubao kusomeka 2-1 matokeo yaliyobaki hadi mwisho wa mchezo huo na kuwafanya Simba kubeba alama zote tatu .

 

SIMBA ‘KUKIWASHA’ NA MASHUJAA LEO LIGI KUU NBC

LIGI Kuu ya NBC inarejea rasmi leo ambapo mchezo mmoja utachezwa katika uwanja wa KMC Complex uliopo Mwenge mkoani Dar es Salaam timu ya Simba ikiikaribisha timu ya Mashujaa kutoka mkoani Kigoma.

Mchezo huo utachezwa majira ya saa kumi jioni ikiwa ni mchezo wa kiporo cha mzunguko wa 24 wa Ligi Kuu ya NBC ambao haukuchezwa kutokana na Simba kuwa na michezo ya Kombe la Shirikisho Afrika ambapo wamefanikiwa kufuzu fainali ya michuano hiyo.

Simba ipo nafasi ya pili kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC ikiwa na alama 57 ikifanikiwa kufunga mabao 52 na kuruhusu mabao 8 ikiwa ni timu iliyoruhusu mabao machache kuliko timu zote ikiwa timu hiyo imeshacheza michezo 22.

Mashujaa ipo nafasi ya 10 kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC ikiwa imefanikiwa  kufunga mabao 26 ikiruhusu mabao 30 katika michezo 26 ambayo timu hiyo imeshacheza.

MBEYA CITY YAREJEA LIGI KUU YA NBC

TIMU ya Mbeya City imerejea rasmi Ligi Kuu ya NBC ambayo ni Ligi namba nne kwa ubora barani Afrika  wakitokea Ligi ya Championship ya NBC baada ya kufanikiwa kufikisha alama 65 baada ya kuifunga timu ya Cosmopolitan mabao 5-0 huku ikiwa na mchezo mmoja ikiwa ni wiki moja baada ya Mtibwa Sugar kufanikiwa kurejea Ligi Kuu ya NBC.

Mbeya City ilishuka  na sasa wamerejea rasmi huku ikiwa imeweka rekodi ya kufunga mabao mengi ksatika Ligi ya Championship baada ya kufunga mabao 63 katika michezo 29 ambayo timu hiyo imeshacheza mpaka sasa huku katika michezo yao  14 ya nyumbani wakishinda 11 na sare 3 na ugenini  michezo 15 wakishinda michezo nane sare tano na kufungwa michezo miwili

 

Aidha timu hiyo imefanikiwa kufunga mabao 63 kuruhusu mabao 26 katika michezo timu hiyo  iliyocheza huku wakiwa wamebaki na mchezo mmoja ili kuweza kutamatika kwa Ligi ya Championship ya NBC ambao pia utaamua nani bingwa wa Ligi hiyo kati ya Mtibwa Sugar wenye alama 68 au Mbeya City wenye alama 65.

Ratiba ya Ligi Kuu ya NBC 2025/2026

MAHAKAMA YA KIMATAIFA YA USULUHISHI WA MICHEZO CAS YATUPILIA MBALI RUFANI YA YOUNG AFRICAN

MAHAKAMA ya Kimataifa ya Usuluhishi wa Michezo (CAS) imetupa rufani ya klabu ya Yanga yenye kumbukumbu namba CAS 2025/A/11298 ambayo klabu hiyo iliifungua dhidi ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kuhusiana na mchezo namba 184 wa Ligi Kuu ya NBC (Young Africans SC vs Simba SC).

Walalamikiwa wengine katika shauri hilo ambapo pamoja na mengine, klabu ya Yanga iliomba mechi tajwa hapo juu isipangiwe tarehe mpaka litakapotolewa uamuzi, ni Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB), na klabu ya Simba.

Kutokana na uamuzi huo wa CAS, Bodi ya Ligi Kuu Tanzania inaendelea na maandalizi yake ya kuhitimisha msimu wa Ligi Kuu ya NBC 2024/2025 na kufanya maboresho ya ratiba ya Ligi (ukiwemo mchezo namba 184 – Young Africans vs Simba SC) kisha kutangaza ratiba mpya mapema iwezekanavyo.