Author: Loveness Bernard

HAYA HAPA MABORESHO RATIBA YA LIGI KUU YA NBC

BODI ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) imefanya maboresho ya ratiba ya Ligi Kuu ya NBC kuanzia mzunguko wa 28 hadi 30 ikiwa ni ratiba ya kukamilisha msimu wa 2024/2025.

Michezo nane ya mzunguko wa 28 inataarajiwa kuchezwa kuanzia mei 12 hadi mei 14 huu timu ya Simba ikicheza dhidi ya Singida Black Stars mei 28 ikiwa ni baada ya mchezo wao wa Fainali ya Kombe la Shirikisho.

Michezo yote nane ya mzunguko wa 29 wa Ligi Kuu ya NBC itachezwa June 18 saa 10:00 alasiri na michezo ya mzunguko wa 30 itapigwa June 22 ambayo itakuwa siku ya kuhitimisha msimu wa 2024/2025.

NGOMA AWALIZA JKT LIGI KUU YA NBC

LIGI Kuu ya NBC imeendelea kwa mchezo mmoja ulioikutanisha timu ya JKT Tanzania na timu ya Simba katika uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo majira ya saa kumi jioni ulioshuhudia Simba ikishinda kwa bao moja.

Iliwachukua dakika 45 Simba kuandika bao kupitia kwa kiungo wake Fabrice Ngoma baada ya kupokea pasi kutoka kwa mshambuliaji Steven Mukwala na kuifanya Simba kwenda mapumziko ikiwa inaongoza bao moja.

Kipindi cha pili kilianza ambapo JKT Tanzania walijitahidi kulisaka lango la Simba bila kupata bao na hadi mchezo unatamatika ‘Mnyama’ alikuwa mbele kwa bao la Ngoma.

Simba ilifanikiwa kubeba alama zote tatu na kufikisha alama 63 katika michezo 25 iliyocheza huku ikiendelea kusalia katika nafasi ya pili katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC

JKT KUWAKARIBISHA SIMBA ISAMUHYO LIGI KUU YA NBC

LIGI Kuu ya NBC itaendelea kesho kwa mchezo mmoja ambapo timu ya JKT Tanzania itaikaribisha timu ya Simba katika uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo uliopo Mbweni mkoani Dar es Salaam  majira ya saa kumi jioni.

Mchezo huo ambao ni mchezo wa mzunguko wa 25 ulishindwa kufanyika hapo awali kutokana na ugumu wa ratiba ya Simba iliyokuwa  na michezo ya Kombe la Shirikisho barani Afrika.

JKT Tanzania ipo nafasi ya saba katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC ikiwa imefanikiwa kufunga mabao 24 na kuruhusu mabao 24 katika michezo 26 ambayo timu hiyo imeshacheza mpaka sasa huku ikikusanya alama 32.

Simba ipo nafasi ya pili kwenye msimamo  wa Ligi  Kuu ya NBC ikiwa imekusanya alama 60 katika michezo 23 ikifunga mabao 54 na kuruhusu mabao tisa .

KIPAGWILE,HAMDI WANG’ARA TUZO ZA MWEZI APRIL LIGI KUU NBC

MSHAMBULIAJI wa timu ya Dodoma Jiji, Iddi Kipwagile amechaguliwa kuwa Mchezaji Bora wa mwezi Aprili wa Ligi Kuu ya NBC msimu wa mwaka 2024/25, huku Miloud Hamdi wa Yanga, akichaguliwa kuwa Kocha Bora wa ligi hiyo kwa mwezi huo.

Kipwagile alionesha kiwango kizuri chenye mwendelezo akiwashinda Pacome Zouzoua wa Yanga na Haruni Chanongo wa Tanzania Prisons, alioingia nao fainali katika mchakato wa Tuzo za Mwezi uliofanywa na Kamati ya Tuzo za Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF).

Mchezaji huyo alitoa mchango mkubwa kwa timu yake katika michezo minne ambayo Dodoma Jiji ilicheza mwezi huo na kufunga mabao matatu na kuhusika na mengine matatu kwa dakika 320 alizocheza.

Kwa upande wa Hamdi aliyeingia fainali na Amani Josiah wa Tanzania Prisons na David Ouma wa Singida Black Stars, aliiongoza Yanga kushinda michezo yote minne iliyocheza mwezi huo na kuendelea kubaki kileleni mwa msimamo wa ligi Kuu ya NBC. Yanga ilizifunga Tabora United (0-3), Coastal Union (1-0), Azam (1-2) na Fountain Gate (0-4).

Pia Kamati ya Tuzo imemchagua Meneja wa Uwanja wa Isamuhyo uliopo Dar es Salaam, Ashraf Omar kuwa Meneja Bora wa Uwanja kwa mwezi Aprili kutokana na kufanya vizuri katika menejimenti ya matukio ya michezo pamoja na masuala yanayohusu miundombinu uwanjani.

Wakati huohuo Kamati ya Tuzo za TFF, imemchagua Emmanuel Maziku wa Stand United kuwa Mchezaji Bora wa Mwezi Aprili wa Ligi ya NBC Championship 2024/25, huku Ramadhan Ahmada wa Transit Camp akichaguliwa kuwa Kocha Bora wa mwezi huo.

Maziku aliyeingia fainali na Mohammed Hassan wa Transit Camp na Ramadhan Kipalamoto wa Songea United, alionesha kiwango chenye mwendelezo, ikiwa ni pamoja na kufunga mabao manne kwa dakika 194 alizocheza kwenye michezo mitatu.

Kwa upande wa Ahmada aliyeingia fainali na Malale Hamsini wa Mbeya City na Awadh Juma wa Mtibwa, aliiongoza timu yake kushinda michezo yote mitatu iliyocheza na kupanda kutoka nafasi ya 15 hadi ya 13 kwenye msimamo wa ligi hiyo.

SIMBA ‘YATAKATA’ DHIDI YA MASHUJAA LIGI KUU YA NBC

LIGI Kuu ya NBC imeendelea leo kwa mchezo mmoja uliochezwa majira ya saa kumi jioni katika uwanja wa KMC mkoani Dar es Salaam ambapo Simba waliwakaribisha timu ya Mashujaa kutoka mkoani Kigoma.

Mchezo ulianza kwa kasi ambapo kila timu ilionyesha ikitaka kupata alama tatu  ambapo iliwachukua dakika tano timu ya Mashujaa kufungua ukurasa wa mabao kupitia mchezaji wao Jafary Kibaya ambapo mpaka wakati wa kwenda mapumziko matokeo yalikuwa 0-1 licha ya Simba tupambana kusawazisha .

Kipindi cha pili kilianza kwa kasi huku Simba wakiwa na uchu zaidi wa kufika langoni mwa mpinzani wao licha ya kukutana na upinzani mkali kutoka kwa wachezaji wa timu ya mashujaa ambapo hata hivyo dakika ya 65 ya mchezo huo Leonel Ateba alifungua akaunti ya mabao kwa Simba kupitia mkwaju wa penati na kufanya ubao kusomeka 1-1 na alirejea tena nyavuni kupitia mkwaju wa penati ya pili hivyo kufanya ubao kusomeka 2-1 matokeo yaliyobaki hadi mwisho wa mchezo huo na kuwafanya Simba kubeba alama zote tatu .