Category: STORY

MUKWALA,FADLU WANG’ARA TUZO ZA MWEZI

MSHAMBULIAJI wa timu ya Simba ya Dar es Salaam, Steven Mukwala amechaguliwa kuwa Mchezaji Bora wa mwezi Machi wa Ligi Kuu ya NBC msimu wa mwaka 2024/25, huku Fadlu Davids pia wa Simba akichaguliwa Kocha Bora wa ligi hiyo kwa mwezi huo.

Mukwala alionesha kiwango kizuri chenye mwendelezo akiwashinda Elie Mpanzu wa Simba na Paschal Msindo wa Azam alioingia nao fainali katika mchakato wa Tuzo za Mwezi uliofanywa na Kamati ya Tuzo za Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF).

Mchezaji huyo alitoa mchango mkubwa kwa timu yake katika michezo miwili ambayo Simba ilicheza mwezi huo na kufunga mabao manne, huku matatu akifunga katika mchezo mmoja (hat-trick). Mukwala alicheza dakika 152 za michezo miwili.

Kwa upande wa kocha Davids aliyeingia fainali na Rachid Taoussi wa Azam na David Ouma wa Singida Black Stars, aliiongoza Simba kushinda michezo yote miwili iliyocheza mwezi huo. Simba iliifunga Dodoma Jiji mabao 6-0 na Coastal Union mabao 0-3, hivyo kuendelea kubaki nafasi ya pili kwenye msimamo wa ligi.

Pia Kamati ya Tuzo imemchagua Meneja wa Uwanja wa Sokoine Mbeya, Modestus Mwaluka kuwa Meneja Bora wa Uwanja kwa mwezi Machi kutokana na kufanya vizuri katika menejimenti ya matukio ya michezo pamoja na masuala yanayohusu miundombinu uwanjani.

Wakati huo huo Kamati ya Tuzo za TFF, imemchagua Mwani Thobias wa Mbeya City kuwa Mchezaji Bora wa Mwezi Machi wa Ligi ya NBC Championship 2024/25, huku Awadh Juma wa Mtibwa Sugar akichaguliwa Kocha Bora wa mwezi huo.

Thobias aliyeingia fainali na Magata Charles wa Mtibwa Sugar na Selemani Richard wa Stand United, alionesha kiwango chenye mwendelezo, ikiwa ni pamoja na kufunga mabao matano kwa dakika 325 alizocheza za michezo minne.

Kwa upande wa Awadh aliyeingia fainali na Mohamed Ismail wa TMA na Juma Hussein wa Stand United, aliiongoza Mtibwa Sugar kushinda michezo mitatu kati ya minne iliyocheza na kuendelea kubaki kileleni kwenye msimamo wa ligi

DUBE,AHOUA HAPATOSHI UFUNGAJI BORA LIGI KUU NBC.

VITA ufungaji bora imeanza upya ndivyo unavyoweza kusema baada ya mshambuliaji wa Young Africans Prince Dube kumfikia  idadi ya mabao kiungo wa Simba,Jean Ahoua huku Ligi Kuu ya NBC ambayo ni Ligi namba nne kwa ubora barani Africa ikielekea ukingoni.

Dube ambaye amefunga mabao 12 na kutoa pasi za mwisho nane katika michezo 25 ambayo timu yake imeshacheza mpaka sasa katika Ligi Kuu ya NBC sawa na Ahoua wa timu ya Simba ambaye amefanikiwa kufunga mabao 12  na kutoa pasi za mwisho saba katika michezo 22 ambayo timu yake imeshacheza.

Young Africans imebakisha michezo mitano ikiwa imeshacheza michezo 25 huku Simba ikiwa imebakisha michezo minane baada ya kucheza mechi 22 hivyo njia inaweza kuwa nyepesi kwa wachezaji hao na wengine wanaowakaribia kuibuka na ufungaji bora wa Ligi Kuu mara baada ya kufikia ukingoni.

 

COASTAL UNION WAIZINDUA MKWAKWANI KIBABE LIGI KUU NBC

LIGI Kuu ya NBC inaendelea kushika kasi ambapo jana Coastal Union iliwakaribisha timu ya Singida Black Stars katika uwanja wa Mkwakwani Tanga ikiwa ni mechi ya kwanza tangu kuboreshwa kwa uwanja huo.

Mchezo huo ulianza majira ya saa 10:00 alasiri ambapo timu zote zilikuwa na shauku ya kuchukua alama ili kujiweka katika mazingira mazuri Coastal Union wakiendelea kujinasua kutoka nafasi za chini kwenye msimamo na Singida wakipambania nafasi nne za juu kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC.

Dakika 47 ziliwatosha Coastal Union kuongoza mchezo baada ya kupata bao la kwanza baada ya mchezaji wa Singida Josephat Bada kujifunga hivyo kuwafanya wana mangushi kwenda mapumziko na uongozi wa 1-0.

Kipindi cha pili kilianza kwa kasi na dakika ya 76 mshambuliaji wa Singida, Jonathan Sowah aliipatia timu yake bao kupitia mkwaju wa penati na dakika ya 82 mchezaji wa Coastal union, Bakari Msimu aliongeza bao hivyo mchezo kutamatika kwa 2-1.

Matokeo hayo yanaipeleka Coastal hadi nafasi ya 10 na alama 28 huku Singida ikisalia nafasi ya nne ikiwa na alama 50.

‘MBUNGI’ TATU MIKOA MITATU NBC CHAMPIONSHIP LEO.

MICHEZO mitatu ya Ligi ya Championship ya NBC itachezwa leo Aprili 10 kwenye mikoa ya Songea, Pwani na Tanga ikichezwa kuanzia saa 10:00 alasiri.

Mkoani Songea, timu ya Songea United inaialika Stand United kwenye uwanja wa Majimaji.

Songea inashika nafasi ya saba kwenye msimamo wa Ligi hiyo ikiwa na alama 43 huku Stand United ikiwa nafasi ya tatu na alama 52.

Kiluvya ya mkoani Pwani itakuwa mwenyeji wa Mbeya Kwanza ya mkoani Mtwara kwenye uwanja wa Mabatini mkoani Pwani huku mchezo wa duru la kwanza Mbeya kwanza iliifunga kiluvya kwa mabao 2-1 mchezo uliopigwa kwenye uwanja wa Nangwanda Sijaona mkoani Mtwara.

Mchezo wa mwisho leo unazikutanisha African Sports dhidi ya TMA kwenye uwanja wa CCM Mkwakwani mkoani Tanga.

Hii ni kwa mara ya kwanza msimu huu African Sports inautumia uwanja wa CCM Mkwakwani kama uwanja wake wa nyumbani tangu ulipofanyiwa marekebisho makubwa.

Mapema wiki hii mzunguko wa 26 ulianza kwa mchezo kati ya Biashara United na Mbeya City ambapo mchezo huo ulimalizika kwa sare ya bao moja.

NAMUNGO,JKT TANZANIA HAKUNA MBABE

LIGI Kuu ya NBC imeendelea ambapo JKT Tanzania waliikaribisha Namungo uwanja wa Isamuhyo mchezo uliochezwa saa nane mchana na kumalizika kwa sare ya 2-2.

Mchezo ulianza kwa kasi ambapo  Namungo walishambulia lango la JKT na dakika ya 18 Saleh Karabaka aliipatia timu yake bao la kwanza kabla ya dakika ya 49 Fabrice Ngoy kuongeza bao la pili.

Kipindi cha pili JKT Tanzania walirudi kwa kasi baada ya kutambua makosa yao na dakika ya 63  Maka Edward akaipatia JKT bao la kwanza na dakika ya 69 wakaongeza bao la pili lililofungwa na  Shiza Kichuya.

Katika mchezo huo mchezaji bora alikuwa  Shiza Kichuya wa JKT Tanzania aliyetengeneza bao la kwanza kwa mpira wa kona huku akifunga bao la kusawazisha kwa timu yake.

Kwa matokeo hayo JKT inafikisha alama 32 na kushika nafasi ya saba huku Namungo ikishika nafasi ya 11 baada ya kukusanya jumla ya alama 28.