Category: STORY

LIGI YA CHAMPIONSHIP YA NBC KINAPIGWA SANA

LIGI YA CHAMPIONSHIP YA NBC ‘KINAPIGWA’ SANA

TAYARI mizunguko 19 ya Ligi ya Championship ya NBC imeshachezwa hadi sasa na kushuhudiwa kwa ushindani mkubwa wa nafasi kwenye msimamo wa ligi hiyo.

Mtibwa Sugar inaendelea kusalia kileleni mwa msimamo wa Ligi hiyo ikiwa na alama 45 ikifuatiwa na Geita Gold kwenye nafasi ya pili ikiwa na alama 42, Stand United ipo nafasi ya tatu ikiwa na alama 39 huku nafasi ya nne ikishikiliwa na Mbeya City ikiwa na alama 39.

Biashara United inashika nafasi ya mwisho kwenye msimamo wa Ligi ya Championship ya NBC ikiwa na alama nne pekee hadi sasa, Cosmopolitan inashikilia nafasi ya 15 moja kutoka mwisho ikiwa na alama tisa.

Timu mbili za juu kwenye msimamo wa Ligi ya Championship ya NBC zinapanda moja kwa moja Ligi Kuu ya NBC huku zile mbili za mwisho zikishuka moja kwa moja hadi First League.

Yanga yarejea kileleni ligi kuu ya nbc

YANGA YAREJEA KILELENI, KAGERA GARI LIMEWAKA.

LIGI Kuu ya NBC iliendelea jana Februari 14, 2025 kwa michezo minne kupigwa kwenye mikoa ya Tabora, Dar es Saalam, Mbeya na Kagera.

Mchezo wa mapema saa 8:00 Mchana ulizikutanisha Tabora United dhidi ya Kengold na kumalizika kwa sare ya bao moja, Bao kwa upande wa Kengold likifungwa na Selemani Bwenzi kwa mkwaju wa penati na kufikisha mabao matatu kwenye michezo mitatu ya Ligi Kuu ya NBC aliyocheza mpaka sasa huku bao la Tabora United la kusawazisha likifungwa na Heritier Makambo na kufikisha jumla ya mabao sita kwenye Ligi Kuu ya NBC mpaka sasa.

Mkoani Mbeya, Tanzania Prisons ikaialika Namungo kwenye uwanja wa  Sokoine saa 10:00 alasiri na kumalizika kwa Namungo kuibuka na ushindi wa bao moja, ushindi huo unaipandisha Namungo hadi nafasi ya nane kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC ikifikisha Alama 21.

Young Africans ikiwa ugenini KMC Complex, Dar es Salaam ikaibuka na ushindi mnono wa mabao 1-6 dhidi ya KMC na kurejea kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu ya NBC ikifikisha alama 49 kwenye michezo 19 ya Ligi Kuu ya NBC, Young Africans imefunga jumla ya mabao 48 mengi zaidi kuliko timu yoyote kwenye Ligi Kuu ya NBC mpaka sasa.

Kagera Sugar ikiwa katika uwanja wake wa nyumbani Kaitaba mkoani Kagera, imepata ushindi mnono wa mabao 3-0 dhidi ya Fountain Gate, imewachukua takribani siku 102 kwa Kagera Sugar kupata ushindi kwenye uwanja wake wa nyumbani kwenye Ligi Kuu ya NBC msimu huu, Mara ya mwisho Kagera kupata ushindi ilikuwa ni Novemba 4, 2024 dhidi ya Dodoma Jiji ambapo iliibuka na ushindi wa mabao 2-1.

Ligi hiyo inaendele leo Februari 15, 2025 kwa michezo miwili, mchezo wa kwanza ukizikutanisha Pamba Jiji dhidi ya Coastal Union saa 10:00 alasiri kwenye uwanja wa CCM Kirumba Mwanza huku Mchezo wa pili na wa mwisho ukizikutanisha Azam FC dhidi ya Mashujaa kwenye uwanja wa Azam Complex saa 1:00 usiku.

SINGIDA YABEBA ALAMA TATU LIGI KUU YA NBC.

 

LIGI Kuu ya NBC imeendelea leo Februari 13, 2025 kwa mchezo mmoja kwenye uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, ukizikutanisha JKT Tanzania dhidi ya Singida Black Stars na kumalizika kwa Singida kushinda kwa bao 1.

Bao pekee la Singida Black Stars hii leo limefungwa na Jonathan Sowah dakika ya 52 ya mchezo akimalizia kazı iliyofanywa na Arthur Bada.

Kwa ushindi huo Singida Black Stars inaendelea kusalia nafasi ya 4 kwenye msimamo ikifikisha alama 37 baada ya michezo 19.

Katika hatua nyengine mchezaji Jonathan Sowah amechaguliwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo kutokana na mchango wake mkubwa kwa timu yake kuondoka na alama tatu akifunga bao pekee na la ushindi kwa Black Stars.

SIMBA, DODOMA KUPANGIWA TAREHE MPYA LIGI KUU YA NBC.

BODI ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB), imeahirisha mchezo namba 148 wa Ligi Kuu ya NBC kati ya Simba SC na Dodoma Jiji ulipangwa kufanyika kwenye uwanja wa KMC Complex Februari 15, 2025 saa 10:00 alasiri.

Sababu ya kuahirishwa kwa mchezo huo ni baadhi ya wachezaji na maofisa wa ufundi wa klabu ya Dodoma Jiji kutokuwa katika hali nzuri kiafya baada ya basi la klabu hiyo walilokuwa wakisafiria kutoka Ruangwa mkoani Lindi, kupata ajali mkoani humo.

Ajali hiyo imesababisha athari hasi kwa klabu ya Dodoma Jiji kwa kuchelewesha safari yake ya kuelekea mkoani Dar es Salaam pamoja na kuathiri maandalizi ya kiufundi kwa kuwakosa wachezaji na maofisa wa ufundi ambao walipata majeraha katika ajali hiyo.

Ajali hiyo imepelekea Bodi ya Ligi Kuu Tanzania kuahirisha mchezo huo na itatangaza tarehe mpya hivi karibuni.

SIMBA YAREJEA KILELENI KIBABE,TABORA UNITED HAISHIKIKI LIGI KUU NBC

LIGI Kuu ya NBC iliendelea jana kwa michezo mitatu iliyochezwa katika viwanja mbalimbali nchini kuanzia saa kumi alasiri na mchezo wa mwisho ukichezwa saa moja jioni.

Simba waliwakaribisha timu ya Tanzania Prisons katika uwanja wa KMC Complex majira ya saa kumi alasiri ambapo mchezo ulianza timu zote zikicheza kwa tahadhari kubwa hususan Simba .

Dakika ya 29 Jean Ahoua alifungua ukurasa wa mabao  kwa timu yake akipokea pasi ya upendo kutoka kwa beki wa timu hiyo Shomari Kapombe,winga wa timu hiyo Ellie Mpanzu nae aliongeza bao la pili dakika ya 44 huku Ladack akifunga bao la tatu na kuwafanya Simba kwenda mapumziko wakiwa kifua mbele kwa mabao 3-0.

Kipindi cha pili kilianza ambapo timu ya Tanzania Prisons walifanya mabadiliko na kuamua kucheza kwa kujilinda zaidi ambapo waliweza kufanikiwa lengo lao kutoruhusu bao lolote kipindi cha pili hivyo mchezo kuisha kwa Simba kufanikiwa kubeba alama zote tatu hivyo kupanda kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu.

Beki wa Simba Shomari Kapombe alichaguliwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo baada ya kutoa pasi mbili za mabao kwa Jean Ahoua na Ladack Chasambi.

Mchezo mwingine  ulikuwa ni timu ya  Mashujaa iliwakaribisha timu ya Coastal Union katika uwanja wa Lake Tanganyika mkoani Kigoma.

Katika mchezo huo timu zote zilicheza kwa tahadhari kubwa kwa sababu ya kuzitaka alama tatu  muhimu ili kujiweka katika nafasi nzuri katika msimamo wa Ligi Kuu ya NBC.

Mpaka dakika 90 za mchezo huo zinatamatika ubao wa matokeo ulikuwa unasomeka 0-0. Mchezaji wa Mashujaa Idrisa Stambuli alichaguliwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo.

Mchezo wa mwisho ulichezwa saa moja jioni mkoani Kagera ambapo Kagera Sugar iliwakaribisha timu ya Tabora United katika uwanja wa Kaitaba.

Mchezo ulianza vyema huku wachezaji wote wakionyesha ari ya kuzipambania timu zao  ambapo dakika 45 za mchezo huo zilitamatika kwa sare ya kutokufungana .

Kipindi cha pili kilianza ambapo dakika ya 52 mchezaji wa Tabora United, Offen Chikola alifungua ukurasa wa mabao na dakika ya 77 mchezaji  Andy Bikoko aliiongezea bao timu yake ya Tabora United  na dakika chache kabla ya mchezo kutamatika mchezaji wa Kagera Sugar, Cleophace Mkandala aliifungia timu yake bao la kufutia machozi hivyo mchezo kutamatika kwa 2-1.

Mchezaji wa Tabora United Offen Chikola alichaguliwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo baada ya kufunga bao moja na kutoa pasi ya mwisho katika mchezo huo.

Ligi Kuu ya NBC itaendelea kesho kwa mchezo mmoja ambapo timu ya JKT Tanzania itawakaribisha timu ya Singida Black Stars katika uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo uliopo Mbweni mkoani Dar es Salaam.