Tag: #NBCPL#STORY

LIGI YA CHAMPIONSHIP YA NBC KINAPIGWA SANA

LIGI YA CHAMPIONSHIP YA NBC ‘KINAPIGWA’ SANA

TAYARI mizunguko 19 ya Ligi ya Championship ya NBC imeshachezwa hadi sasa na kushuhudiwa kwa ushindani mkubwa wa nafasi kwenye msimamo wa ligi hiyo.

Mtibwa Sugar inaendelea kusalia kileleni mwa msimamo wa Ligi hiyo ikiwa na alama 45 ikifuatiwa na Geita Gold kwenye nafasi ya pili ikiwa na alama 42, Stand United ipo nafasi ya tatu ikiwa na alama 39 huku nafasi ya nne ikishikiliwa na Mbeya City ikiwa na alama 39.

Biashara United inashika nafasi ya mwisho kwenye msimamo wa Ligi ya Championship ya NBC ikiwa na alama nne pekee hadi sasa, Cosmopolitan inashikilia nafasi ya 15 moja kutoka mwisho ikiwa na alama tisa.

Timu mbili za juu kwenye msimamo wa Ligi ya Championship ya NBC zinapanda moja kwa moja Ligi Kuu ya NBC huku zile mbili za mwisho zikishuka moja kwa moja hadi First League.

DODOMA JIJI YASHINDWA KUTAMBA NYUMBANI.

TIMU ya Dodoma Jiji imepoteza mchezo wake wa kwanza wa Ligi Kuu ya NBC baada ya kurejea kutoka kwenye mapumziko mafupi kwa bao moja kutoka kwa Pamba Jiji ya mkoani Mwanza.

Mchezo huo uliokutanisha timu zilizopo chini ya manispaa za jiji ulipigwa kwenye uwanja wa Jamhuri, Dodoma na kushuhudia bao lililofungwa kipindi cha kwanza na Mathew Tigisi likiizamisha Dodoma nyumbani.

Huu ni mchezo wa tatu kwa timu ya Pamba kushinda kwenye Ligi Kuu ya NBC msimu huu huku ikishinda miwili ugenini na mmoja pekee ikishinda kwenye uwanja wake wa nyumbani.

Dodoma imepoteza mchezo wa nane msimu huu idadi sawa na timu ya Pamba jiji huku Dodoma ikisalia nafasi ya tisa na alama 19 nne zaidi ya timu ya Pamba iliyofikisha alama 15 na kushika nafasi ya 14.

PRISONS YAIDUWAZA MASHUJAA LIGI KUU YA NBC.

TIMU ya Tanzania Prisons imerejea vema kwenye Ligi Kuu ya NBC baada ya kuifunga Mashujaa mabao 2-1 kwenye uwanja wa Sokoine, Mbeya.

Mabao ya Prisons yalifungwa na Beno Ngassa mdogo wa nyota wa zamani wa timu ya taifa ya Tanzania Mrisho Ngassa na Meshack Mwamita aliyefunga bao la ushindi kipindi cha pili huku bao la kufutia machozi kwa mashujaa likifungwa Seif Karihe kwa mkwaju wa penati.

Ukiwa mchezo wa kwanza kwa kocha mpya wa Prisons Amani Josiah kwenye Ligi Kuu ya NBC Prisons imesalia nafasi ya 13 ikifikisha alama 17 sawa na Namungo huku Prisons ikizidiwa kwa mabao ya kufunga.

Matokeo hayo yanaifanya timu ya Mashujaa kusalia nafasi ya saba ikiwa na alama 19 sawa na timu za JKT, Dodoma Jiji na KMC huku mashujaa ikiwa juu kwa tofauti ya mabao ya kufunga na kufungwa.

LADHA ZA LIGI KUU NBC ZAREJEA YANGA WAKIWALIZA KAGERA SUGAR

Ladha za Ligi Kuu ya NBC zimerejea rasmi leo Februari 1 kwa mchezo mmoja uliochezwa uwanja wa KMC mkoani Dar es Salaam ambapo timu ya Yanga waliwakaribisha Kagera Sugar.

Mchezo ulianza majira ya saa kumi alasiri kwa timu zote kushambuliana kwa kasi huku Yanga wakionekana kuutawala mchezo.

Ilimchukua dakika 32 mshambuliaji wa Yanga Clement Mzize kufungua akaunti ya mabao na kuifanya timu yake kwenda kifua mbele mapumziko licha ya kiungo wa timu hiyo Aziz Ki kushindwa kufunga mkwaju wa penati waliopata timu yake.

Kipindi cha pili kilianza ambapo dakika ya 60 Mudathir Yahya aliongeza bao la pili kwa Yanga huku wakionekana kuzidi kulisaka lango la mpinzani wao na kutaka mabao zaidi.

Pacome Zouzoua aliongeza bao la tatu kwa mkwaju wa penati baada ya mchezaji wa Kagera Sugar kumfanyia madhambi Max Nzengeli  kabla ya Kennedy Musonda kufunga bao la nne hivyo Yanga kufikisha alama 42 wakiwa wamefunga mabao 36 na wakiruhusu 6.Mchezaji wa Yanga Max Nzegeli amechaguliwa kuwa mchezaji bora wa mchezo huo.

Ladha za Ligi Kuu ya  NBC zitaendelea kesho mkoani Tabora ambapo timu ya Tabora United watawakaribisha Simba saa kumi alasiri katika Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi.

LIGI KUU NBC YA NNE KWA UBORA AFRIKA

Shirikisho la Kimataifa la Historia na Takwimu za Mpira wa Miguu (IFFHS) limeitangaza Ligi Kuu ya Tanzania (NBC Premier League) kuwa Ligi ya nne kwa ubora barani Afrika na ya 57 duniani kwa mwaka 2024.

Ligi hiyo imepanda kwa nafasi mbili kutoka nafasi ya sita mwaka 2023 hadi nafasi ya nne ikizipiku Ligi za Afrika Kusini na Tunisia.

Kwa mujibu wa taarifa ya IFFHS kwa upande wa Afrika nchi zilizoko chini ya Shirikisho la Soka (CAF) Ligi Kuu ya Misri inayofahamika kama Nile Premier League ndio kinara kwa ubora Afrika.

Nafasi ya pili inashikiliwa na Botola Pro ambayo ni Ligi Kuu ya Morocco huku League 1 ya Algeria ikishika nafasi ya tatu kwa ubora mwaka 2024.

Kwa upande wa Ligi Kuu ya NBC ya Tanzania imekwea hadi nafasi ya nne barani Afrika kutokana na ligi hiyo kuwa na usimamizi bora kuanzia Serikali, Shirikisho la Soka nchini (TFF), Bodi ya Ligi Kuu (TPLB), Klabu zinazoshiriki ligi hiyo, wadhamini mbalimbali wanavyounga mkono pamoja na mashabiki.